Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nimshukuru pia Mheshimiwa Kubenea kwa kunipa dakika zake tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuunga mkono maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni, lakini na yale maoni yaliyotolewa na Kamati yetu ya Ardhi, Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na upatikanaji wa fedha katika Wizara hii muhimu sana katika Taifa letu. Kumekuwa na ucheleweshwaji au kutokupelekwa kabisa kwa fedha za maendeleo katika Wizara hii. Wachangiaji wengi wameonesha umuhimu wa Wizara hii, lakini Wizara ya Fedha imekuwa haipeleki fedha za maendeleo na kufanya miradi mingi ya Wizara hii kushindwa kutekelezeka kwa wakati. Pia miradi mingi imekuwa ikitegemea wafadhili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tumwombe Waziri wa Fedha kuhakikisha kabisa zile fedha tunazozitenga hapa ndani ya Bunge ziwe zinapelekwa kwa wakati ili kuisaidia Wizara hii iweze kufanya vizuri zaidi. Amesema kaka yangu, Mheshimiwa Mbatia hapa kwamba ili ng’ombe aendelee kutoa maziwa mengi ni lazima alishwe vizuri. Kwa hiyo tunaomba fedha hizo ziwe zinakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, Kamati yetu imekuwa ikifanya ziara mbalimbali katika taasisi zilizoko chini ya Wizara hii, kwenye hifadhi zetu na hata misitu. Tumekutana na changamoto mbalimbali, mojawapo ni uhaba wa watumishi katika taasisi hizo na hasa kubwa ni askari wale wa wanyamapori. Tunajua ukubwa wa hifadhi zetu na misitu, hivyo, tuiombe Wizara sasa ihakikishe kwamba inaajiri askari wengi ambao watakwenda kuhakikisha wanalinda mali zetu, wanyama wetu na rasilimali zote zilizomo ndani ya misitu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo malalamiko ambayo tumepata kutoka kwa askari hawa wa Jeshi Usu kwamba kumekuwa na utofauti wa malipo kutoka kwa askari hawa wa Jeshi Usu wa TAWA, TANAPA, Ngorongoro na TFS. Wamekuwa wanalipwa pungufu, posho na wengine mishahara. Tunajua kazi wanazofanya ni kubwa na wanafanya kwenye mazingira magumu wote, kwa hiyo tunaomba sana Wizara ihakikishe askari wetu hawa wote wanalipwa sawasawa, yaani kusiwe na tofauti za mishahara wala posho kwa sababu kazi wanayoifanya ya kulinda rasilimali zetu ni kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, upo upungufu wa magari; tunajua mbuga zetu zilivyo kubwa, lakini pia miundombinu yake si mizuri, magari yaliyopo kule ni machakavu, yanafanya utendaji kazi wao kuwa mgumu sana. Kwa hiyo tunaomba wapate magari ya kutosha na vifaa vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile wana uhaba wa nyumba za kukaa, wanafanya kazi lakini nyumba za kukaa hawana na wanakwenda kupanga mbali na maeneo yao ya kazi. Tunaomba basi nyumba wajengewe na kama inashindikana basi wapewe housing allowances ambazo zinaweza kuwasaidia wao kutekeleza majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisemee suala la migogoro ya mipaka; suala hili limechukua muda mrefu sana na migogoro bado tunaendelea kuiona. Jana Mheshimiwa Waziri Mkuu amejibu swali kwamba ile taarifa ya zile Wizara nane imeshapelekwa kwa Mheshimiwa Rais, tunashukuru kwa hilo, lakini tunaomba taarifa hii basi itakapofanyiwa kazi na kurejeshwa kwa ajili ya kuanza kutekelezwa wawashirikishe wawakilishi wa wananchi; Wabunge pamoja na Madiwani wa maeneo yale ili kuondoa migogoro hiyo, kwa sababu ikifanywa kimyakimya migogoro hii haitaisha na itaendelea kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa tumekuwa tukiona kauli nyingi nzuri na matamko mazuri yanatolewa kwa wananchi, tunaomba yakatekelezeke yasije yakawa ni ya kisiasa kwa sababu tunakwenda kwenye uchaguzi. Tunaomba haya yakafanyike, yafanyiwe kazi vizuri, wananchi wetu waondokane na hii migogoro ya mipaka kila wakati, tupunguze vifo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale kwa askari niongeze jambo moja; tulikwenda kwenye mahafali ya hawa askari wa Jeshi Usu, tuliwaomba kwamba pamoja na mafunzo yote wanayopewa lakini wawe wanatimiza wajibu wao wasionee raia, kupiga raia bila sababu. Kwa sababu kumekuwa na malalamiko ya maaskari hawa kupiga wananchi wetu bila sababu, niwaombe sana wasimamie maadili ya kazi zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo tuliliona na imesemwa kwenye Taarifa yetu ya Kamati na ya Kambi ya Upinzani, ni kuhusu migongano ya sheria zilizopo. Mfano ni Sheria ya Ardhi Na.4 ya mwaka 1999, Sheria ya Vijiji Na.5 ya 1999, Sheria ya Wanyamapori na ile Sheria ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati yetu tumefanya ziara mbalimbali kwenye hifadhi zetu na tumeona Sheria ya Madini inaweza kutoa kibali cha kuchimba madini kwenye eneo lolote. Tulipita kwenye Hifadhi ya Manyara Bunge lililopita, tulikuta yapo machimbo watu wanachimba kule na hii ni hatari sana kwa watumishi wetu wanaofanya kazi kwenye hifadhi hizo, lakini pia kwa wanyama wetu. Mashimo yale ni makubwa sana yanaweza kuleta athari kwa wanyama wetu. Kwa hiyo niiombe Serikali, Serikali hii ni moja, sheria hizi zimetungwa ndani ya nchi hii, basi ikae kwa pamoja kuhakikisha wanapitia sheria hizi ili kuondoa huo mgongano uliopo katika sheria hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la biashara ya viumbe hai; suala hili limechukua muda mrefu sana, toka 2016, huu ni mwaka wa nne sasa. Wafanyabiashara hawa walizuiwa wakasema wanaweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba wataweza kupangiwa ili kufanya biashara zao vizuri, lakini juzi Naibu Waziri alipokuja kwenye Kamati yetu alituambia kwamba biashara hii imepigwa marufuku.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuiomba na kuishauri Serikali kwamba wafanyabiashara hawa walifuata taratibu zote zinazohusika, walikata leseni, wamelipa kodi na walishakamata wanyama hawa, wameingia gharama ya kuwatunza. Niombe, inawezekana wapo wahalifu wachache walioingilia biashara hii na kufanya wengine kuzuiliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanyama ambao tunawazungumzia siyo wale wanyama wakubwa kama tembo, twiga na swala kama wale waliosafirishwa kwenye Uwanja wa KIA wakati ule; ninaowazungumza na waliokuwa wanasafirishwa ni nyoka, mijusi, ngedere, kenge na vipepeo. Wanyama hawa kama hawatavunwa itakuwa ni hatari sana hapo baadaye kwa Taifa letu kwa sababu hawa watatuletea athari kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Waziri kubadilisha maamuzi ambayo wameyafikia na kuruhusu wafanyabiashara hawa kuendelea na biashara hiyo. Wale waliokosea basi wachukuliwe hatua za kisheria, hakuna anayekubaliana na kusafirisha wanyama hao wakubwa nje ya nchi lakini hawa wengine wadogowadogo ambao wanaweza kuleta madhara hapo baadaye waweze kuruhusiwa kuendelea na hiyo biashara. Kwa sababu tunajua hawa walilipa kodi na walifanya taratibu zingine zote na haya ndiyo maisha yao. Wengine wamekopa wanasomeshea watoto kwa hiyo kuwafungia tu hivihivi siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ninalotaka kulisemea ni lile ambalo limezungumziwa kwenye Kamati yetu kuhusu TANAPA, tozo nyingi sana. Tunaiomba Serikali kuliangalia Shirika hili la TANAPA, limekuwa likifanya kazi nzuri kusaidia wananchi wetu lakini limekuwa likirundikiwa kodi nyingi na juzi zimeongezewa tena hifadhi nyingine tano, kwa hiyo kuziendesha itakuwa ni gharama kubwa sana. Kwa hiyo tuiombe Serikali, tuiombe Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba wanaliangalia Shirika hili la TANAPA ambalo limekuwa likifanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni lile la TFS kuwa mamlaka; wamesema wenzangu, jukumu la TFS tunalijua, inalinda misitu yetu, lakini ni vizuri sasa kuifanya iwe mamlaka ili iweze kusimamia sheria zake na kufanya maamuzi kama linavyofanya Shirika la TANAPA ili nalo liweze kufanya vizuri, tunaomba ikafanyike hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Waziri pia na Naibu wake, wamesema Wajumbe wenzangu kwamba mwanzo Wizara hii ilikuwa ikija mbele ya Kamati ilikuwa ina mambo mengi, lakini wameweza kutekeleza maagizo ya Kamati, wanakwenda vizuri. Niwapongeze sana, lakini yale yote tuliyoyasema kwenye Kambi ya Upinzani na yale ya kwenye Kamati yetu, tunaomba wahakikishe wanayafanya vizuri na hususan posho kwa maaskari wetu pamoja na mishahara yao mkaiboreshe kwa sababu hawa wanalinda rasilimali zetu, ni vizuri wote wakalingana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru. (Makofi)