Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Maliasili na Utalii

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nikushukuru sana kwa kunipa nafasi niwe mchangiaji wa kwanza kwa siku ya leo. Niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri na Watendaji wote wa Wizara ya Maliasili jinsi wanavyofanya kazi, ni kweli wameitia uhai Wizara ya Maliasili na kazi wanayofanya inaonekana kwa mapana na marefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mwakilishi wa wananchi wa Jimbo la Njombe Mjini nikisimama hapa ninaongelea sana sana mazao ya misitu na mazao ya misitu ninayoongelea mimi ni mbao. Wizara hii kama ingejikita kwenye uzalishaji wa mbao laini ingeliweza kuisadia Serikali kupata mapato makubwa sana. Lakini kwa bahati mbaya sana imeacha uzalishaji wa mbao unafanywa kienyeji sana, ukiangalia jinsi miti ilivyopandwa katika Jimbo la Njombe Mjini, ukaangalia jinsi watu wanavyopasua kienyeji na kuacha west nyingi kwa maana ya kwamba upotevu wa mbao ni mkubwa sana na mbao zile kusafirishwa bila hata kufanyiwa treatment yoyote zinasafirishwa zikiwa ghafi pato kubwa la Serikali linapotea, wananchi wanakosa mapato, lakini na Serikali na yenyewe inakosa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sasa Serikali kupitia Wizara hii kwamba wahakikishe sasa wanafanya utaratibu wa kupata mashine zilizo bora ili kusaidia upasuaji wa mbao katika Jimbo la Njombe Mjini uwe wa kitaalam mbao zile tuwe kuzi-treat, tuweze kuzisafirisha na tuwe na mbao ambazo zina ubora wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiacha suala la uzalishaji wa mbao nije kwenye suala la usafirishaji. Suala la usafirishaji wa mbao limekuwa ni kero kubwa sana kwa wafanyabiashara wote wanaosafirisha mbao, lakini hata kwa matumizi binafsi ya mbao. Usafirishaji wa mbao unapakia mbao kwenye gari ukimaliza kupakia mbao hizo saa 11 jioni huwezi kusafirisha, ikifika saa 12 ukitembeza gari lenye mzigo wa mbao lazima upigwe faini.

Ndugu zangu tunakwenda na maendeleo sasa, maendeleo yetu yanakwenda kwa kasi sana, hii biashara kusimamisha magari ya mizigo saa 12 jioni yasisafiri na mzigo halafu yaanze kusafiri kesho yake saa 12 ya asubuhi tunawasimasisha kwa ajili ya nini? Na hasa hasa hizi mbao za miti ya kupandwa kwanza anayesafirisha ana leseni, ana vibali vyote, amelipa ushuru, kila kitu amefanya, lakini bado ikifika saa 12 jioni lazima asimame mzigo ulale hapo na kesho asubuhi uanze kusafiri. Yaani gari la mzigo linalala kabla kuku hawajaingia ndani na sisi tunatafuta maendeleo hatuwezi kufika kwa staili hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri unafanya kazi nzuri sana, Naibu Waziri unafanya kazi nzuri sana, Mkurugenzi wa TFS anafanya kazi nzuri sana na watu wake, lakini kwa hili kwa hili hebu angalieni mnafanyaje, vinginevyo leo shilingi hapa hamtoki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mwalikishi wa watu wa Njombe wenzangu tunaotoka Njombe na Iringa hatuwezi kukubali hili, tumekuwa tukiwaambieni mara kwa mara tunataka mbao zisafiri usiku na mchana watu wafanye biashara, biashara ifanyike, yaani haiwezekani mtu atoke na gari la mbao Njombe afike Mwanza baada ya siku nne wakati mwenzake aliyepakia viazi anafika Mwanza baada ya siku mbili hiyo haiwezekani kabisa. Lakini kwa kufanya hivyo kwa kuondoa utaratibu huo wa kutokusafiri usiku hakuna madhara ya aina yoyote kwa maana ya mapato ya Serikali, hakuna kodi itakayopungua, hakuna mapato ya aina yoyote yatakayopungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunawaombeni sana hakikisheni mnarekebisha huu utaraibu haraka iwezekanavyo ili wafanyabiashara wa mbao na mazao mengine ya misitu zikiwemo mijengo, zikiwemo kuni, ukiwemo na mkaa. Tunalalamika misitu inaharibika, lakini tunawacheleweshea watu nishati Njombe sisi tuna miti maalum ya mkaa ya kupandwa, inaitwa uoto, au milingo. Ile miti ukitengeza mkaa ndiyo unaotumika katika familia mbalimbali watu mkaa wanataka kusafirisha wapelekee watu wasio na mkaa ili waokoe misitu sehemu nyingine ninyi mnasimamisha gari isitembee mkaa unalala watu wanashindwa kupata mkaa wa miti ya kupandwa matokeo yake wanatumia nishati nyingine, lakini wanakata miti ambayo ni miti ya asili niwaombe sana,.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika zoezi hili la miti ya mkaa ningeliomba sana Wizara hii kwa sababu yenyewe ndiyo inashughulika na upandaji wa miti na ndiyo inayoshughulika kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kutokata miti ya asili kwa kuwa Njombe sasa sisi tuna miti inayofaa kwa mkaa na tumekuwa tukipanda miaka yote. Lakini sasa hatuna uwezeshaji wa aina yoyote ile tunafanya wenyewe kama wananchi tumekuwa tukijitahidi na wananchi wa Njombe niwaambieni, wananchi wa Njombe hawatumi kazi, wananchi wa Njombe wanafanya hawana kikao na mtu kwenye suala la kazi, suala la bidii, suala la kilimo, suala la upandaji wa miti hawashauriani mtu yoyote wao wanajua ratiba yao ya maisha ya kila siku ni kupanda miti kwa ajili ya maendeleo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe sasa wataalam wa TFS na Wizara hebu jikiteni Njombe mpate miti mingi ipandwe kwa ajili ya mkaa ili kusudi wananchi wa nchi hii waweze kupata mkaa kutoka kwenye miti ya kupandwa badala ya kupata mkaa kutoka kwenye miti ya asili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie tena kusisitiza suala la usafiri na usafirishaji wa mazao ya msitu ya mbao ya kupandwa. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri na watu wake wajitahidi kadri wanavyoweza leo atakapokuwa anahitimisha taarifa yake aseme lolote lile linalowezekana kuhakikisha kwamba mbao zinaweza kusafiri usiku na mchana; wakati huo wa zamani, kwanza sheria ukiangalia utaratibu huu wa kizamani sana wakati nchi haijaendelea, barabara hazijafunguka, hasa manufaaa ya kufungua barabara ni nini? Kama tumefungua barabara ya Dodoma, Iringa imekuwa ya lami lahafu unalaza mzigo Mtela maana yake nini, kuna maana ya, lazima tuone haya maendeleo mengine yaliyopatikana lazima kila Wizara sasa iyapokee iyatumie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TFS bado hamjatumia fursa hiyo ya kufunguka kwa barabara zetu, TFS hamjatumia fursa hiyo ya magari makubwa kuwepo ndani ya nchi yetu. Nakumbuka miaka ya zamani kama miaka kumi, 15 iliyopita gari kubwa kabisa lilikuwa ni Bedford au Isuzu, ilikuwa inabeba mbao 500, mabao 100, 250. Lakini leo gari inabeba bao 3,000 tumefanya maendeleo halafu unalilaza njiani tena unachelewesha maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana na kwa kufanya hivyo mtawapunguzia gharama wasafirishaji, moja kwa moja mtawapunguzia gharama wananchi, pia mtaifanya nchi ipate fedha nyingi kwa sababu gari linapotembea linakwenda lina rudi, linakwenda linarudi, linatumia mafuta na kwenye mafuta kuna ushuru wa Serikali. Kwa hiyo, mtakuwa mmeisaidia Serikali kupata mapato zaidi; kwa hiyo, niwaombe sana mlione hilo na mlifanyie kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa nafasi naunga mkono hoja, ahsante.