Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nimshukuru sana Mwenyenzi Mungu kwa kuniwezesha kusimama mbele hapa ili niweze kuhitimisha hoja yangu.

Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru sana wewe binafsi, Mheshimiwa Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge kwa uwezo na umahili mkubwa mnaounesha katika kuliendesha Bunge letu Tukufu. Nichukue nafasi hii kumpongeza sana kwa dhati Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa (Mb) na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa umakini wake wa kusimamia shughuli za Serikali hapa Bungeni. Aidha, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliopata nafasi ya kuchangia hoja yangu niliyoiwasilisha hapa Bungeni kwa michango yao mizuri na ya kina yenye lengo la kuboresha utekelezaji wa majukumu ya Wizara yangu.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingi zimetolewa, na hii ni dalili ya dhati kwamba upo mwamko mkubwa sana upande wa kuendeleza sekta ya mifugo na uvuvi ili ziweze kupiga hatua zaidi katika maendeleo. Aidha, katika michango hiyo imedhihilisha wazi kuwa kuna mahitaji makubwa ya kusimamia sekta ya mifugo na uvuvi kupitia sheria, kanuni, taratibu na miongozo mbalimbali inayoongoza Wizara yangu. Ni dhahili kuwa masuala ya kuendeleza utafiti wa mifugo na malisho ikiwa ni pamoja na kuendeleza kosafu bora za mifugo ili kuongeza tija katika uzalishaji wa maziwa, nyama, mayai na ngozi kuendana na mnyonyoro wa thamani wa uchumi na viwanda. Aidha, tafiti mbalimbali zinahitaji kuendelea kufanyika kwa nyakati tofauti zenye lengo la kujua rasilimali za uvuvi ikiwa ni tafiti katika ukanda wa bahari kuu.

Mheshimiwa Spika, napenda kutambua Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja mbalimbali katika Wizara yangu ambapo wapo jumla 46. Sitawaja majina yao lakini walichangia kwa kusimama 29 na ambao wamechangia kwa maandishi ni 17. Michango ya Waheshimiwa Wabunge wote niliowataja ilikuwa mizuri sana na iliyosheheni busara na heshima na hekima na changamoto. Aidha, si rahisi kujibu kwa kina na kutosheleza hoja zote za Waheshimiwa Wabunge kwa muda huu mfupi. Naahidi kwamba hoja zote tutazijibu kwa maandihsi na Waheshimiwa Wabunge wote watapewa.

Mheshimiwa Spika, ushauri na maoni ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji umezingatiwa.

Pia maombi ya Kambi ya Upinzani vilevile yamezingatiwa isipokuwa moja tu. Mchango wa kambi ya upinzani safari hii ulikuwa mzuri sana, isipokuwa pendekezo moja tu lililosema kwamba Wizara itumie sera za CHADEMA. Wizara haitatumia sera za CHADEMA kwa sababu sera za CCM ni nzuri na hazina mfano kwa hiyo hakuna sababu yoyote ya kutumia sera za CHADEMA, zinajitoshereza. Kwa hiyo sera hapa ni za CCM na ilani hapa itatumika ya CCM.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nizungumze kuhusu hoja za Waheshimiwa Wabunge. Hoja zilizozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge ni nyingi mno, kama nilivyosema. Kwa hiyo nitajaribu ambazo nitaweza kuzifikia ili kuweza kutoa ufafanuzi huo kwa Wabunge. Moja ni hili la Mheshimiwa Mzee wangu Lubeleje Mbunge wa Mpwapwa la kuhusu kituo cha tariri. Kilichofanyika pale hatuja hamisha kituo cha utafiti cha tariri tulichohamisha ni Makao Makuu. Makao makuu ni Mkurugenzi ni mambo ya utawala si mambo ya kiutafiti tena. Kwa maana ya kituo cha utafiti bado kipo pale, kwa hiyo mzee wangu Lubeleje hana sababu yoyote ile ya kukamata shilingi kwa hoja hiyo, kwa sababu kama wananchi wa mpwapwa kituo chao hatujakiondoa cha utafiti. Walioondoka ni hao wakurugenzi ambao wanawajibika kwa mambo ya kiutawala ndio tuliowaleta hapa.

Mheshimiwa Spika, la pili Waheshimiwa Wabunge mmezungumzia hoja mbalimbali za uvuvi na mifugo. Sasa katika hoja za uvuvi baadhi yake ikiwa mmesisitiza sana kwamba sheria kuharakisha mchakato wa kuboresha sera na sheria za uvuvi. Awali niliwaambia kwenye hotuba kwamba tumeamua kwa dhati kuhakikisha kwamba sheria ya uvuvi namba 22 ya mwaka 2003 pamoja na kanuni zake za mwaka 2009 tumekubaliana kama wizara tumezifumua na tumetembea kwa wadau kanda zote kutaka mawazo yao. Tayari sasa hivi mchakato Serikalini unaendelea.

Mheshimiwa Spika, na kama tulivyowaahidi Waheshimiwa Wabunge sheria hizi zitafika mikononi mwenu Ili muweze kutushauri kadri matakavyoweza ili tuweze kutengeza kanuni au sheria zitakazoendana wakati wa sasa na kuondoa changamoto zilizopo. Sasa sioni tatizo tena la lawama juu ya Wizara kwa sababu maamuzi ya Wizara ni maamuzi makubwa, kuamua kufumua sheria yote ili tuweze kupata maoni mengi. Lakini vilevile kuamua kufumua mpaka kanuni ili tuweze kupata maoni mengi. Kakini vilevele hata katika kufumua kanuni hiyo ndiyo maana tukaamua kwamba yapo mambo ya dharura ambayo inapaswa yafanyike sasa hivi kwa haraka sana kwa sababu yalikuwa yanakwaza sana wavuvi. Kwa hiyo nilitegemea kwamba Waheshimiwa Wabunge wengi mngeyashangilia.

Mheshimiwa Spika, Moja uvuvi wa ukanda wa bahari kuu ambao unalazimisha watu kuvua kwa kutumia nyavu za mm 10 ilikwepo kwa mijibu wa sharia; kuvua kwa tumia mm 10. Wananchi wakalalamika, Waheshimiwa Wabunge mkalalamika, Serikali ikakubali kurekebisha sheria na kanuni zimesainiwa na GN ipo tayari na leo mnondoka na GN hiyo. Wananchi wa ukanda wa pwani hawawezi tena kukamtwa kuzuiwa kuvua kwa kutumia mm nane. Sasa hizo ni achievement zenu wala si za Wizara, mliishauri Wizara, Wizara hii ya Serikali ya Awamu ya Tano ambayo ni nyenyekevu sana na sikivu imetekeleza.

Mheshimiwa Spika, lakini ukanda wa Ziwa Victoria, ukomo wa kuvua samaki wa sentimita 85; kwamba huruhusi kuvua samaki wa sentimita 85 napo Serikali imesikia. Katika kufanya hiyo tumekubali tumerekebisha, tumeondoa ukomo huo ambapo sasa wananchi wa ukanda wa ziwa victoria watavua bila ukomo. Tunahakikisha kwamba hairuhusiwi kuvua chini ya sentimita 50. Lakini huku na kuendelea kwa maana ya samaki sangara mtaendelea kuvua samaki wa urefu wowote ule. Hii ni mileage kubwa upande wetu kwa sababu viwanda vingi vitapata malighafi nyingi lakini vilevile uzalishaji wa bidhaa kama mabondo utazalishwa kwa wingi sana. Hata hivyo hili nalo ni la kwenu Wabunge mlilalamikia na kuomba Serikali ifanye na tumetekeleza, tatizo nini tena?

Mheshimiwa Spika, mmesema kwamba wananchi wanahangaika kupata leseni kila wilaya; na ninataka niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba hoja hii mmsifikie mahala mkajisahau kwamba maji yalipo kwenye eneo lako kama ni ziwa lipo pale Sengerema eti lile ziwa ni la Sengerema, msijisahau hivyo. Kama bahari ipo rufiji usijisahau ukasema hiyo bahari ni ya rufiji, hiyo bahari ni rasilimali ya taifa, ya wananchi wote, mkatushauri kama Serikali kwamba kwa nini mwananchi akate leseni kila wilaya?Wakati mwingine uko ndani ya maji, unavua hujui kama umefika chato, hujui kama umefika Sengerema. Unavua, unavua tu unaenda. Hujui kama umefika Tanga hujui kama umefika Bagamoyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kila unafika unakamatwa unaambiwa kata leseni nyingine, tukakubali tuka-amend sheria. Sasa mnataka Serikali yenye usikivu wa aina gani? Tume-amend, tumekubali tumrekebisha sheria wananchi sasa hivi watavua maji yote. Uikata leseni ya Bahari ya Hindi ukanda wa pwani utavua kote. Ukikata leseni ya kuvua ziwa victoria utavua ziwa lote. Ukikata leseni ziwa Tanganyika utavua ziwa lote; sasa hiyo ndio Serikali sikivu.

Mheshimiwa Spika, na Waheshimiwa Wabunge sisi tuko vizuri kuwasiliza sana tu. Mmezungumzia wala kukosekana wa uwiano wa sheria za uvuvi katika nchi za Afrika Mashariki. Mimi nataka kwanza Waheshimiwa Wabunge mjivunie sana na haya mafanikio, kwa sababu haya mafanikio sisi tungewafuata wenzetu. Tulipokwenda kufanya Oparesheni Sangara Ukanda wa Ziwa Victoria watu wote walisema kwamba Kenya wenyewe hawana masharti hayo na hawana sheria hizo Tanzania sisi tuna sheria hizo; sasa kama tunakwenda maana yake sisi tutakuwa looser. Nataka niwahakikishie, sisi ndio tuna maji mengi, kama ni looser sisi tungekuwa ni looser namba moja. Ziwa victoria sisi tuna asilimia 51. Hatuweze tukawa tunawafuata watu, kwamba Kenya wapo hivi lazima na sisi tuwe hivyo. Wakibadilisha leo, wanabadilisha kesho tunabalisha tena kwa sababu Kenya wamebadilisha?

Mheshimiwa Spika, lakini sisi tuka-stick tukasema lazima oparesheni ziendelee. Leo baada ya taasisi za kiutafiti za nchi zote tatu wote wanaipongeza Tanzania. Tatifi ambazo zimefanywa na TAFIRI pamoja na taasisi zingine za kitafiti za Kenya na Uganda baada ya samaki kuongezeka kwa muda mfupi sana katika Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Spika, ongezeko hilo mwaka 2016/2017 kwa samaki waliokuwepo Ziwa Victoria; uvunaji wa samaki katika ziwa victoria ulikuwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, wakati tunaanza oparasheni samaki wachanga ziwa victoria walikuwa asilimia 96.6 samaki wachanga, yaani lile ziwa lilikuwa na samaki wachanga wote. Baada ya oparasheni asilimia ya samaki wachanga imefikia asilimia 62.8, imeshuka. Vilevile samaki waliofaa kuvuliwa wakati tunaanza oparesheni Ziwa Victoria ilikuwa ni asilimia 3.3. Sasa kama ni asilimia 3.3 ndio samaki wanaofaa kuvuliwa; leo samaki wanaofaa kuliwa ziwa wamefikia asilimia 32. Sasa walikuwa wanazidi asilimia 85 ambao ndio samaki wazazi Ziwa victoria walikuwa 0.4, na leo wapo asilimia 5.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, urefu wa samaki sangara wastani ulikuwa 16 leo urefu umefikia urefu umefikia wastani wa sentimita 25.2; haya ni mafanikio makubwa. Nchi zote zinajivuni kwa hatua ambazo zimechukuliwa na Tanzania, na wanaendelea kuwekeza viwanda mbalimbali na sisi tutaenda kuwekeza viwanda, na ndiyo maana tukakubali kurekebisha hata kuruhusu kuvua samaki wa zaidi wa sentimita 85 kwa sababu moja kwamba samaki wazazi sasa hivi tunaona wengi. Sasa una 0.4 Waheshimiwa Wabunge unataka uvue kwa utaratibu unataka, una samaki wazazi 0.4 lile ziwa victoria tungefunga uvuvi isingewezekana uvuvi kufanyika, 0.4 za samaki wazazi tulikuwa tunaenda kumaliza lile ziwa. Sasa tuna asilimia 5.2, ni samaki wengi. Kwa hiyo sasahivi tunafunga uvuvi hii viwanda vingi vitajengwa na wananchi wengi watanufaika sana na uwekezaji huu.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Kuwepo kwa Faini ya Gandamizi Sisizozinga Sheria. Waheshimiwa Wabunge hakuna namna yoyote Serikali hii ya Awamu ya Tano na Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi ninayoingoza ambayo inaweza kuwavamia wananchi kwenda kwaongea bila sababu; hakuna namna yoyote ile na hatuwezi kufanya hivyo na hatuna sababu ya kufanya hivyo. Waheshimiwa Wabunge hili jambo ni vizuri likaeenda case by case. Kwa sababu mnapolileta hapa kwa ujumla wamepigwa wananchi wameumizwa bila hata kueleza ni wapi walipoumizwa na wapi walipopigwa imekuwa ikituleta changamoto sana. Mara nyingine tumekuwa tukifuatilia ukweli tunaokuta kule sio ule. Sheria za Serikali zilizopo Serikali ndizo itakazo zifuata. Sheria hizi zimetungwa na Mbunge, hili hakuna namna yoyote ya Bunge hili kuzikana hizi sheria.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Uvuvi Namba 22 ya Mwaka 2003 imetungwa na Bunge hili. Kanuni za mwaka 2009 ziliinidhishwa kutumika kulingana na sheria iliyokuwepo; kwahiyo hakuna namna yoyote ya Bunge kujitoa katika utungaji wa sheria. Kwa hiyo tunafika kwenye jambo hili, na bahati nzuri mnaweza mkawa mnatuona Naibu Waziri yupo, Makatibu wa Wakuu wapo kuchambua case by case. Sasa hivi imeripotiwa (be reported) hoja ya Tunduma, ya kwamba watu hawana leseni tu wamepigwa faini milioni mbilimbili. Lakini ukweli si huo, tumefuatilia kwa kina, wale watu wana under declaration. Mtu ana tani 20 anaandika tani tano, anaandika tani 10. Sisi mnapotuambia internally tutafuatilia kwa kina kujua kama tatizo ni la mtumishi tutamshughulikia yule mtumishi. Kama tatizo ni mambo mengine tutashughulika nayo. Kwa hiyo nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge tuwe pamoja katika ulinzi wa hizi rasilimali.

Mheshimiwa Spika, na operesheni hizi, tumesema mudawote, zimekuwa zikifanyika kwa nia njema, na katika hili hakuna atakayepona, yoyote atakamatwa kuhusu zoezi hili la watu kujishughulisha na uvuvi haramu. Sasa uvuvi haramu huu wakati mwingine nyingine hata Wabunge wengine hapa tunageukana. Akisha kamatwa ndugu yako au mtu wako wa karibu tayari unaigeuka Wizara, tayari unawageuka watumishi wa Wizara hiyo. Kwamba ni watumishi wabovu, amezungumza hapa Mheshimiwa Tizeba. Tizeba alikuwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi; amezungumza hapa, mambo mengine nitayasema baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata hili la vijana kusema wanaonea watu kwenye jimbo lake si kweli. Mheshimiwa Tizeba akiwa waziri amekuwa akipigia simu vijana wa mifugo na uvuvi kuwa-harass na kuwaambiwa hataki watu wake wakamatwe kwa ajili ya uvuvi haramu. Mheshimiwa Tizeba amekuwa akiwa-harass vijana wa uvuvi, hata sasa hivi akiwa mbunge, akisema kwamba hataki mtu wake akamtwe kwenye eneo la lake la uvuvi. Sasa ukifika hapa unabadilika inakuwa hawa vijana kwa sababu hawapo ndani ya Bunge hili wanashutumia kwa kiwango hivyo, si vizuri.

Mheshimiwa Spika, wapo vijana wetu ambao wanafanya kazi vibaya, tuletee tu tutawshughulikia. Hata hivyo vijana hawa wamefanya kazi nzuri sana. Leo tunajivunia kama taifa kupambana na uvuvi haramu, tunajivunia kama taifa kupamba na uvuvi haramu. Sasa wamefanya kazi nzuri hivyo hasa sisi vingozi wenyewe tuliozitunga sheria wenyewe, tumepewa mpaka na mamlaka kwa sababu wameguswa tu watu wako, kwa sababu limeguswa tu jimbo lako maafisa hawa wote wanakuwa ni wabaya. Twendeni case by case.

Mheshimiwa Spika, nalizungumzia hili suala la oparesheni, hizi operesheni zote, Oparesheni Sangara pamoja, Oparesheni MATT na Operesheni Jodari zimeleta mageuzi makubwa, lazima tujivunie. Uzalishaji wetu wa samaki umeongezeka, uzalishaji wetu wa mazao mbalimbali umeongezeka kwa kiwango kikubwa sana hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, mambo tuliyoyafanya baada ya oparesheni hizi; mauzo yetu ya nje ya samaki yameongezeka sana. Uzalishaji wetu wa ndani wa samaki umeongeza sana. Nilikuwa nasikiliza kwenye tv mama mmoja anahojiwa anasema mimi jambo ambalo namkumbuka Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli na kumpongeza ni moja; tulikuwa tunanunua samaki sato kwa shilingi 14,000 leo tunanunua kwa shilingi 7,000/ Tulikuwa tunanunua samaki sangara kwa kilo shilingi 9,000 leo tunanunua kwa shilingi 6,000. Samaki wapo kila sehemu wameongezeka. Ilitokea Watanzania walianza kula vifaranga; hatusahau jinsi rasilimali hii ya uvuvi ilivyovurugwa na uvuvi haramu, hatuja sahau.

Mheshimiwa Spika, Watanzania leo wanakula samaki wazuri, bora na wenye viwango, tena kwa bie ndogo, na wanapatikana kila sehemu na mauzo yetu ya nje yanazidi kuongezeka. Mlikuwa mnazungumzia mauzo kwamba mauzo yetu yanapungua; hivi unawezaje kuongeza mauzo ya samaki ilhali samaki wazazi waliobaki; kwa sababu uzalishaji wetu wa samaki takriban asilimia 90 wote ni Ziwa Victoria. Sasa samaki wazazi umabakiza 0.4, samaki wa kuvua umebakiza asilimia 3.3; utawezaje wewe kuleta mauzo makubwa nje ya nchi? Haiwezekani! Hata hivyo vilevile watu walitorosha, watu wanavua samaki wetu hapa, watu wanakuja hapa kutoka nchi mbalimbali wanapakia samaki wetu wanaondoka nao. Warwanda walikuja hapa wakapakia samaki wetu wakaondoka nao, Wakenya walikuja wakachukua samaki wetu, Warwanda walikuja hapa wakachukua samaki wetu, Waganda hivyo hivyo na nchi nyingine bila kulipa chochote; lakini leo tumewabana wanalipa; hatukatazi kuchukua rasilimali lakini tunawabana wanalipa, tatizo liko wapo?

Mheshimiwa Spika, nilitegemea Waheshimiwa Wabunge kwa makofi makubwa mngewapongeza sana vijana wangu kwa jinsi wanavyochapa kazi nzuri ya ujenzi wa taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Mabomu; hatujasahau watu walivyokufa Ukanda wa Pwani kwa kulipuliwa na mabomu, hatujasahau, watu wamepoteza maisha sana, Serikali ya Awamu ya Tano ikasema hapana tutakomesha mabomu. Watu wanavua kwa sumu, watu wanavua kwa mabomu, tuwachekelee tu, tuseme sawa tu vueni, ninyi ni wapiga kura wetu haturuhusiwi kuwakataza, hapana, hatuwezi kuwa nchi ya namna hiyo, haya lazima tuyakatae. Mwaka 2016 nchi hii mpaka wageni walianza kuikimbia wakikaa kwenye mahoteli mabomu yanalipuka, watu maskini wanaenda kuvua kwa ratiba zao kwa utaratibu wao wanalipukiwa na mabomu wanakufa.

Mheshimiwa Spika, leo mpaka tunavyozungumza uvuvi umeendelea kushuka 2017, 2018 na leo 2019, uvuvi wa kutumia mabomu wameenda ku-test sifuri, hakuna mtu anafanya uvuvi wa mabomu, lakini Waheshimiwa Wabunge, leo kwa nini hatutaki kujivunia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, meli za uvuvi kutoka nje zilikuja hapa kuvua, zimekuja hapa kuvua meli za kigeni kutoka nje ya nchi, zikavua samaki na wakaondoka. Wamefanya uvuvi haramu uliopitiliza kwenye maji yetu, tumekamata meli ya Buhanaga One, tumekamata meli, tumesimamia kesi ile, walizoea mpaka na kesi wanafanya maneuver inakuwaje sijui, sijui inakuwa vipi, tumeshinda kesi Mahakamani, kwa nini isiwe suala la kujivunia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, meli za Kigeni zimekuja hapa nchini, Meli ya Buhanaga One, ambayo tuliipiga faini ya shilingi milioni sabini na saba, kama to compound now, milioni sabini na saba, wakasema tumewaonea. Wameenda Mahakamani wamepigwa faini ya bilioni moja au kifungo cha miaka ishirini, hivi sasa tunavyozungumza, Meli tuliyoikamata ya Buhanaga One, ipo Tanzania, samaki waliyokuwemo mle tani thelathini na mbili, wako ndani ya meli wanashikiliwa, wako Tanzania na yale mapezi ya papa na yenyewe yapo na Mmiliki wa meli amefungwa, Wakala amefungwa na Nahodha amefungwa miaka ishirini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanatakiwa either walipe bilioni moja au wafungwe miaka ishirini, kulipa bilioni moja au kufungwa miaka ishirini, kwa nini isiwe suala la kujivunia hili? Jambo kubwa namna hii, kwa nini Taifa mnalisoma kwenye kitabu hiki Waheshimiwa Wabunge mnaliona la kawaida, ni rekodi ambayo haijawahi kufanyika toka nchi hii ipate uhuru na hata Mungu aumbe dunia na akaiumba Tanzania, haijawahi kuitokea. Kwa nini mnalisoma na hamsemi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania sasa hivi imeheshimika Kimataifa kwamba tunasimamia rasilimali zetu na tunapongezwa. Juzi hapa nchi mbalimbali zilikuwa zinachukua vijana kwenda kusoma mafunzo nje ya nchi, tulikuwa tunachukua vijana wanne, watatu, wawili, sasa hivi nimepeleka zaidi ya kumi na wanaombwa wengine watafika zaidi ya ishirini kwa sababu ya hatua Tanzania inazozichukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ukija hata kwenye hili suala la 0.4, Waheshimiwa Wabunge walitendee haki Bunge. 0.4 kwa samaki wanaovuliwa Ukanda wa Uchumi wa Bahari Kuu, kulipia mrabaha wa dola 0.4, hili jambo halijaanzwa na Serikali, hili jambo limeanzia kwa Wabunge wenyewe na tukaweka maazimio humu ndani ya Bunge. Tukasema kwamba ni lazima Taifa linufaike, watu walikuja na meli zenye ukubwa wa mpaka tani 300. Wanalipa leseni ya dola 65,000 peke yake ni kama shilingi milioni 150 tu, anaingia na meli yenye uwezo wa kuchakata mpaka wa kubeba mzigo wa tani 300 za tuna.

Mheshimiwa Spika, mbona hawajajiuliza tuna akivuliwa hapa anauzwa kwa bei gani, kabla hawajaishauri Serikali kuondoa 0.4 mbona hawajajiuliza hilo swali,? Leo mbona hawajajiuliza swali, watu wanavua dagaa, dagaa ambao wanauzwa kilo moja Sh.10,000 au Sh.15,000, tunatoza ushuru wa 0.3 na wanalipa, leo kwa nini lizungumziwe Kampuni la Kigeni linalokuja kuvua hapa matani kwa matani ya rasilimali za Watanzania na kwenda nazo, halafu tuachwe watupu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema Bunge ndiyo liliiambia Serikali kwamba tumechoka kudhulumiwa, tumechoka kuonewa na hizi meli za uvuvi zinazotoka nje ya nchi. Serikali ya Awamu ya Tano ilipokuja ikatekeleza mara moja, ikaweka kile Kifungu kile cha 0.4 kwa mabadiliko ya Kanuni za mwaka ule wa 2009 zikabadilishwa mwaka 2016, tukaweka tozo ya 0.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge hapa ni mashahidi, Waziri aliyekuwepo, Mheshimiwa Tizeba, alitoa holiday ya miezi sita ya kutokulipa hii 0.4. Alipotoa ile holiday ya 0.4, Kamati iliyoundwa na Mheshimiwa Spika ikabaini kuna dosari na Tanzania imepoteza bilioni tano kwa holiday ile na Serikali tukalaumiwa kwa nini tumetoa holiday, tukapoteza rasilimali hizo. Sasa Bunge linalalamika, kwa kutoa holiday tu ya miezi sita, Bunge hili hili na Wajumbe hao hao na wengine walichangia jana, ambao wameilalamikia Serikali kwa holiday ya miezi sita, leo wanageukaje ghafla kwamba 0.4 ni makosa, Serikali ilifanya njama za kuhujumu uvuvi wa Bahari Kuu. Waitendee haki Serikali yao. Hii Serikali ni ya kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakiwa mnazungumza Mheshimiwa Waziri mwenzangu Tizeba ndiye aliyeiweka na hakuiondoa, Mheshimiwa aliiweka tozo ya shilingi 0.4 na jana ananilaumu mimi tena kwamba sijaiondoa hii 0.4.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, facts are facts, naomba mtulie msikilize majibu, Watanzania hatupendagi facts, sijui tukoje. Ninyi msikilizeni Waziri aseme, angekuwa anasemwa mtu ambaye yuko nje ya Bunge hilo ni sawa kwa sababu hana nafasi ya kurekebisha. Kama Selasini umefanya jambo nakwambia Selasini umefanya hivi, usiseme usinitaje, hapana, wewe si uko hapa, (Makofi)

Endelea Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mbona hata mimi nimetajwa tu vizuri tu, mpaka wengine wakaenda mbali wakasema Waziri hasalimii watu, mbona nimetajwa tu, mbona hakuna Mbunge aliyekataa.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Ongea bwana.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema, Waziri aliyekuwepo aliweka hii Kanuni na yeye jana amegeuka kuwa mlalamikaji ya kwamba mimi nime-frustrate uwekezaji kwa kuweka 0.4. Kwa hiyo ninachotaka kusema Waheshimiwa Wabunge waitendee haki Serikali yao, 0.4 wameiweka wenyewe kwa nia njema ili kuweza kulifanya Taifa letu linufaike, ndiyo maana akaunda na Kamati ya kutushauri juu ya jambo hili tufanyaje ili uvuvi wa Bahari Kuu tuweze kunufaika zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wanapozungumza kuhusu kutoza shilingi 0.4 Waheshimiwa Wabunge lazima tutafakari vizuri, 0.4 tunaiondoa, lakini mbadala wake ni nini, Taifa litanufaika na nini, twende kwa utaratibu gani, kama kuna issue yoyote ile ya kuhusu 0.4 kwa wavuvi wetu ndiyo wameshindwa kuja kuvua kwenye maji yetu, tutaitafutia majawabu, lakini nataka niwakumbushe, tulipoanza kufanya Operation MAT, Ukanda wa Uchumi wa Bahari Kuu, meli ishirini na nne zote zilizokuwa zinavua, ndani ya EZ yetu tulizikamata kwa kujihusisha na uvuvi haramu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo lazima watu wajue, Tanzania, siyo Tanzania ile ya zamani, hatuwezi kuendelea kukubali kuruhusu watu wanakuja, eti kwa sababu tu lazima waje kwenye maji yetu kuvua, watufanyie wafanye uvuvi haramu, wahujumu raslimali zetu, halafu sisi tuendelee kuwaacha, tutaendelea kuwadhibiti. Hata hivyo, niseme, wako watu sasa hivi wanashindwa kuja kuvua, kwa sababu yawezekana bado wana hiyo kesi ya kutoroka kutokana na jinsi tulivyowatuhumu juu ya uvuvi wa Bahari Kuu, walivyotoroka kwa sababu ya uvuvi haramu au kwa sababu zingine. Sasa hili, hatuwezi kuliamua hapa, watupe muda Serikali, tufanye uchambuzi wa kina, tulinganishe wapi na wapi kwa sababu hiyo 0.4 iliwekwa kwa mazungumzo mapana ya Serikali ili nchi yetu kuiwezesha iweze kukusanya mapato makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niongelee suala la mapato na lenyewe limezungumzwa na Waheshimiwa Wabunge wengine wakaenda mbali sana, wakasema hii Wizara yenyewe inajivunia leo mapato haya, kwa sababu ya faini, Waheshimiwa Wabunge watendeeni haki basi hawa vijana wanaofanya hizi kazi. Hizi fedha wanazokusanya hawaweki mifukoni mwao, hizi fedha zote zinazokusanywa zinaingia kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali na sisi hao hao, ndiyo ambao tuna oiomba maji Serikali tunaomba Zahanati, barabara, umeme na huduma mbalimbali za Serikali. Fedha hizi, hakuna Afisa hata mmoja ambaye anachukua yeye anaweka mfukoni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa wamesema, suala la faini, Wizara kwa mfano, katika Sekta ya Mifugo katika para ya 23, mapato ya mwaka 2018/2019 ni bilioni 33.9, lakini mapato hayo faini kati ya fedha hizo ni bilioni tatu, ambayo ni sawa na asilimia tisa. Kwa hiyo siyo kweli kwamba mapato haya ni ya faini tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, katika upande wa Sekta ya Uvuvi, para ya 124 katika mapato ya mwaka 2018/ 2019 ni bilioni 30.3 na hii ni kuishia tarehe 15 Mei, mwaka haujaisha. Faini ni bilioni 6.5 ambayo ni sawa na asilimia 21.3.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kwamba, jitihada hizi zilizofanywa na Wizara ni suala la kudhibiti, tumefanya usimamizi vizuri, wa kuhakikisha kwamba kila eneo linalotakiwa kutoza, linatozwa, wale watu waliokuwa wanatorosha mapato, waliokuwa wanatorosha mifugo yetu tumewadhibiti, waliokuwa wanatorosha rasilimali za uvuvi watu kama nilivyosema, walipakia samaki zetu hapa wakaenda bila kulipa chochote, tumehakikisha wanalipa. Wale watu waliokuwa wanakwepa kodi, tumewasimamia wanalipa kodi, lakini vilevile hata wahalifu lazima waendelee kulipa faini na hizi faini zitaendelea hadi pale wahalifu watakapoisha. Kwa sababu hakuna namna nyingine, sheria zimesema ukifanya hivi utapigwa faini hii.

Mheshimiwa Spika, pia kutoza faini sio dhambi kama kuna mhalifu, kwa hiyo wahalifu wakimalizika na faini hazitakuwepo zitaendelea kushuka kadri watu watakavyokuwa wana-comply. Sasa Waheshimiwa Wabunge, leo nikizungumza trend ya mapato ya uvuvi, mwaka 2009/2010 yalikuwa bilioni 6.6 tu, mwaka 2010/2011 ilikuwa bilioni 8.2, mwaka 2011/2012 ilikuwa bilioni 8.9, mwaka 2012/2013 ilikuwa bilioni 8.3; mwaka 2013/2014 ilikuwa bilioni 10.8; mwaka 2014/2015 ilikuwa bilioni 15.5; mwaka 2015/2016 bilioni 17.87; mwaka 2016/2017 ilikuwa bilioni 18.58; mwaka 2017/2018 ilikuwa bilioni 26.9; na mwaka huu kuishia Mei tarehe 15 ilikuwa bilioni 30.3. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye mifugo mwaka 2009/2010 ilikuwa bilioni 2.7; mwaka 2011/2012 ilikuwa bilioni 8.7; mwaka 2012/2013 ilikuwa bilioni 5.6; mwaka 2013/2014 ilikuwa bilioni 6.8; mwaka 2014/2015 ilikuwa bilioni 6.4; mwaka 2015/2016 ilikuwa bilioni 14.1; mwaka 2016/2017 ilikuwa bilioni 12.5; mwaka 2017/2018 ilikuwa 21.7; na leo tarehe ya leo 23 Mei, 2019 ni bilioni 33.85 na ni kuishia tarehe 15 Mei. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ukija na mtiririko huo, ukija na mtiririko huo mwaka wa 2000 kwa jumla yake, mwaka 2017/2018 ilikuwa bilioni 17.3 na leo 2018/2019 tuna makusanyo mpaka sasa hivi ya bilioni 64.15 na tutafika bilioni 70 ifikapo tarehe 30 Juni, kwa malengo tuliyopewa ya bilioni 40. Makusanyo zaidi ya bilioni 30 na haya makusanyo ya bilioni 30 ambayo yamekusanywa na Wizara hii, yote yako kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali, yanaendelea kutekeleza Mipango mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa mmempongeza Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, amejenga Zahanati ndiyo hizo fedha, mmempongeza Waziri wa Maji, ndiyo hizo fedha. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Rudia, MBUNGE FULANI: Rudia tu. MBUNGE FULANI: Arudie.

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, sisi tunatafuta hizi hela, lakini wanawapongeza, wamempongeza sana Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa amepata pongeza nyingi sana, amejenga zahanati nchi nzima, ni fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wamepongeza miradi ya maji imejengwa, tunaishukuru Serikali na wakawa wanaomba hata tozo ziongezeka, sisi tumetoa mchango wa ziada siyo ile tuliyopewa na Serikali, wa ziada ya bilioni 30. Nataka niwaulize bilioni 30 kama hawa watumishi wangu na mimi Waziri ni mla rushwa, kama sisi ni wala rushwa hizi fedha tungezifikishaje Hazina,? Wapongezeni Vijana hawa, kwa sababu kama wangekula rushwa hizi fedha zisingepatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nawaomba, tuwe wakweli tukiwa hapa, hata Ilani ya Uchaguzi ya CCM inatueleza kutekeleza Ilani hii, hata hiyo ya CHADEMA au ya Chama kingine, sijaona Ilani ambayo itatekelezwa bila pesa, hakuna Ilani ya Chama chochote duniani ambayo inaweza kutekelezwa bila fedha. Kwa hiyo kama kuna njia zozote za kupinga ukusanyaji wa mapato ni kuzipinga hata Ilani za vyama vyenu, kwa sababu hakuna Ilani duniani ambayo unaweza kuitekeleza bila kukusanya kodi, lakini tutaendelea kukusanya kodi hizo na hatutawaonea wananchi kama inavyozungumzwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yamezungumzwa mambo mengi, migogoro ya wafugaji; utatuzi wa migogoro, Wizara yetu imefanya mambo makubwa katika historia ya utatuzi wa migogoro na hata dada yangu yule aliyeanza kusema, Mheshimiwa Gimbi, aliyesema kwamba Mpina ameonea wafugaji, Mpina amewasaliti Wasukuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza moja, nikubali kabisa kwamba mimi siyo Waziri wa Wasukuma, mimi ni Waziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. La pili, hatutawa- favor watu kwa ukabila wao, wakivunja sheria watashughulikiwa. Niliwahi kusema hapa, kwenye uvuvi haramu hata Mzee Mpina mwenyewe tukimkuta ameshiriki uvuvi haramu tutamkamata. Leo nazungumza Mzee Mpina yuko pale, kama atashiriki uvuvi haramu, tutamkamata, kwa sababu hakuna, hatuwezi kutengeneza mazingira ya ukabila ukienda huku unafanya hivi, lakini nataka nimhakikishie hakuna kipindi kingine ambacho migogoro ya wafugaji imetatuliwa kama kipindi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Timu zimeenda maeneo mbalimbali, Wabunge wengine wamezungumza vizuri, kuna watu wengine walikamatwa, ng’ombe 540, Naibu Waziri wangu akaenda tukawaomba watu wa Maliasili na Utalii, ni kweli ng’ombe walikuwa ndani ya hifadhi, tukawaomba wawasamehe, wakasamehewa, ng’ombe 500 wakatoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Katibu Mkuu nikamtuma siku ya Pasaka, kwenda Simiyu ambako ng’ombe zilikuwa zimekamatwa zaidi ya 200, siku ya Pasaka, akaenda kuomba na kwenyewe tukawaomba wenzetu wa Maliasili na Utalii watusaidie kutokana na mazingira yaliyokuwepo, mifugo ile ikatoka. Vilevile tumehangaika nchi nzima, kutafuta malisho ya wafugaji ambako leo, Wizara yetu imetenga hekta 373,000 za kuwapangisha wafugaji katika hatua hii wakati tunawatafutia maeneo mbalimbali kwa ajili ya malisho. Maeneo ya Serikali. haijawahi kutolewa offer hiyo katika kipindi kingine chochote kile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo, Halmashauri tumezifuata moja baada ya nyingine kwenye migogoro mikubwa ya mifugo, tumepata mpaka sasa hivi hekta 199,000 ambazo na zenyewe tutaweka mifugo. Mambo haya hayajawahi kufanyika migogoro ya wafugaji kupigana mapanga na kufanya nini, leo imepungua, ilikuwa dhahama kubwa nchi hii, mbona haipongezwi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, migogoro ya mifugo tuliyoibua mikoa hiyo michache (mitano) tuliyokwenda ni migogoro 43. Katika migogoro hiyo 43 tuka-solve migogoro 27, sawa n a asilimia 63 ya migogoro. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye na mimi naungana sana na Watanzania wengine wote wanaoendelea kumpongeza aliamua kuunda timu ya Mawaziri wanane kwenda kushughulika na migogoro ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi. Tumetembea nchi nzima na tumetoa mapendekezo mengi juu ya kutatua migogoro hii. Ninaamini baada ya hatua hizi kufikiwa tatizo la migogoro la wananchi kukosa malisho litakuwa limepungua.

Mheshimiwa Spika, nawakumbuka wapiga kura wa Kongwa. Tayari tumetenga hekta 13,500 kwa ajili ya wananchi katika Ranch ya Kongwa ili kuweza kuwanufaisha wananchi wa kongwa ambao wamekaa na Ranch hii kubwa sana na kwa muda mrefu lakini hawana mahali pa kuchungia. Kwa hiyo tumekwenda maeneo mbalimbali kutatua changamoto hizi. Mmeona hata juzi hapa Mawaziri tunazunguka nchi nzima kutatua migogoro tukiwa pamoja kama timu moja ya Serikali, kutatua migogoro ya wafugaji. Kwa hiyo mambo haya Waheshimiwa Wabunge Serikali hii tuko kazini na tunaendelea kuyapigania kwa nguvu zetu zote.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, suala la magonjwa ya wanyama. Tumefanya kazi kubwa sana kwenye suala la magonjwa ya mifugo ambapo kwa mara ya kwanza Serikali imeweza kuogesha ng’ombe nchi nzima baada ya kutoa dawa 8,823, tumeogesha nchi nzima. Katika bajeti hii mnayoipitisha tumetenga zaidi ya milioni 500 ambazo tutaogesha tena mwaka unaofuata; kwa hiyo tumejipanga vizuri. Kituo chetu kile cha TVI kinaendelea kuongeza uzalishaji wa chanjo. Tulikuwa tunazalisha chanjo nne tu hapa nchini, sasahivi tumeendelea kuzalisha chanjo, hata hii ya homa ya mapafu ya ng’ombe tayari tumeshaanza na tunaendelea, na tunategemea kwamba baada ya muda mfupi tutafikia chanjo zote 11 ambazo leo tunatumia mabilioni ya fedha za Watanzania kuagiza chanjo kutoka nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, naomba muendelee kutuunga mkono. Mama mmoja akanipigia simu akaniambia Mpina Waziri wa Mifugo hivi Nyerere amefufuka? Nikamuuliza kwanini mama? Mama mtu mzima mwenye umri wa karibia miaka 100 na kitu; Nyerere amefufuka? Nikamuuliza kwanini? Yaani Serikali imeanza kuogesha mifugo! Tunaona kila sehemu Serikali inaogesha mifugo! Nikamwambia mama Nyerere hajafufuka ila kuna kijana wake anait wa Magufuli, kijana wa Nyerere ndiye anayeyafanya haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, operesheni Nzagamba. Operesheni Nzagamba imefanyika kwa nia njema sana. Waheshimiwa Wabunge tukumbuke, lazima tujiulize hili swali; kwa nini viwanda vyetu vimekufa? Watanzania wengi wamejiuliza swali hili lakini ukweli ni kwamba viwanda hivi havikupata ulinzi wa kutosha ndiyo maana vilikufa. Tumeendesha operesheni hapa na matokeo ya operesheni Waheshimiwa Wabunge mmeyaona. Tumeendesha Operesheni Nzagamba, tumekamata watu mbalimbali kwenye maeneo mbalimbali wakijaribu kufanya utoroshaji mkubwa wa rasilimali zetu.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, hakuna mtu atakayekwenda kuwekeza kwenye nchi ambayo hailindi wawekezaji wa ndani. Yaani leo hii unamwambia mtu ajenge kiwanda, kesho watu wanaingiza maziwa hapa nchini, hayana vibali, hayajalipa chochote hayajapimwa hata ubora yanaingia hapa nchini yanauzwa kwa bei ya chini kiasi kwamba huyu hawezi kushindana. Unamwambia mtu ajenge kiwanda cha nyama wakati hoteli zote zinakula nyama kutoka nje, Watanzania wote wanakula nyama kutoka nje na zinauzwa kwa bei ndogo kumbe zingine zimeingizwa hapa zingine zikiwa zime-expire, Watanzania wamekula. Usipowalinda namna hiyo watakula chakula ambacho hakina ubora na hakina viwango. Tufanye nini?

Ukiwakamata tayari una-frustrate wawekezaji. Nani anaye-frustrate wawekezaji? Viwanda vyote nchi hii ilishindikana kuendelea. Wawekezaji wakawa wanapiga danadana wanakimbia. Leo tumeleta hapa mpango, viwanda vipya vinajengwa, uwekezaji wa takriban bilioni 200 kwa muda mfupi wa hatua ambazo Seri kali sisi tumezichukua katika kupambana na watu waliokuwa wanaharibu soko la Watanzania ili kuwepo na ushindani ulio sawa.

Mheshimiwa Spika, huwezi kuupata ushindani ulio sawa kama haya mambo utayaendeleza. Leo tunajenga kiwanda cha chanjo chenye uwezo wa ku-supply chanjo 27, Tanzania, haitaagiza chanjo tena. Mnataka Serikali hii ifanye nini? Viwanda vikubwa vya nyama vinavyojengwa havijawahi kuwepo. Watu wengine walisema wingi wa viwanda si tija, tija ni ufanisi. Sasa hata hivyo viwanda vingi vya aina hiyo hatukuwa navyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima wawekezaji wetu wa ndani tuwalinde na ndiyo maana operesheni hizi zimekuwa zikifanyika. Wafugaji wetu hakuna namna yoyote ile ambayo tunaweza tukawaona kwa namna yoyote ile. Tozo tunazoziweka ni tozo ambazo zinalifanya walau Taifa nalo linufaike. Huwezi ukawa na mifugo nchi hii halafu hupati chochote. Mifugo hii, Tanzania kuwa ya pili Afrika kuwa na mifugo; na ninataka nisahihishe hizo takwimu, watu wamesema kwamba Tanzania ni nchi ya tatu, hapana Tanzania ni nchi ya pili baada ya Ethiopia kuwa na mifugo mingi. Sisi tunashikilia asilimia 1.4 ya mifugo yote iiyoko duniani; tunashikilia asilimia 11 ya mifugo yote iliyoko Bara la Afrika, halafu unakusanya mapato ya bilioni 12, hatuwezi kuruhusu hilo.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, mtuamini, nia ni njema ya kujenga uchumi wa nchi yetu. Tuzalishe mifugo yetu, tupate malighafi ya viwanda, tuzalishe nyama, tuuze nje ya nchi, tuuze maziwa nje ya nchi, tutosheleze soko la ndani. Hivyo hivyo na kwenye samaki. Leo samaki tulikuwa tunaagiza kwa mabilioni ya fedha, uagizaji wa samaki sasahivi umeshuka kwa asilimia 67 tangu tuanze kuchukua hatua hii na mambo yanaenda vizuri. Leo kiwanda chetu cha Chobo kila wiki kinabeba tani 45 kutoka mwanza kuja Dar es Salaam kwa kutumia ndege zetu wenyewe za ATCL. Leo mageuzi haya yanafanyika, sasa tutapata kiwanda cha kuchinja ng’ombe 1,000 cha Chobo kule Mwanza. Tuna minofu ya samaki inayotakiwa kusafiri kila leo. Uvunaji wetu wa samaki sasahivi uko tani 180 mpaka 200 kwa siku; kwa hiyo tuna mzigo mkubwa wa kusafirisha kwenda nje ya nchi. Viwanda hivi vyote vya nyama tunavyovijenga vitatuwezesha kuzisafirisha nyama kwenda nje ya nchi, tutapata fedha za kigeni. Tumetengeneza ajira nyingi za Watanzania, tumetengeneza soko la Watanzania, tumetengeneza bei ya Watanzania katika rasilimali za mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo niwaombe endeleeni kuunga mkono jitihada za Serikali ambazo zina nia njema kabisa ya dhati katika kuhakikisha kwamba mageuzi ya kweli yanapatikana na taifa linanufaika na rasilimali zake na kuhakikisha kwamba mtu yeyote yule hatachezea soko la nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, tumetengeneza dawati la sekta Binafsi, dawati hili limeleta mageuzi makubwa sana hapa nchini. Sekta ya mifugo na uvuvi ilikuwa hata haikopesheki. Mpaka leo hii tunavyozungumza kupitia dawati hili tayari mikopo ya bilioni 17 imetolewa kwa wawekezaji wa sekta ya uvuvi na kwa wawekezaji wa sekta ya mifugo. Hivi tunavyozungumza mikopo ambayo inategemewa kutolewa hivi sasahivi kupitia dawati hili ni bilioni 55 ambayo nayo itatolewa muda wowote kupitia hili dawati ambalo limekuwa kiungo kikubwa sana kati ya Wizara na Serikali na kati ya wadau na wawekezaji wote na wafugaji wote, na wavuvi wote nchini. Leo tunavyozungumza mambo yanaendelea, wanaenda mbali zaidi hata kusaidia mpaka kuandika business plans ili kuwezesha tu mambo haya yaweze kufanyika.

Mheshimiwa Spika, wengine mmezungumzia kuhusu Kiwanda cha Azam. Nataka nizungumzie Kiwanda cha Azam, kiwanda cha Azam kiko Zanzibar, ni cha maziwa, ambapo wana-import maziwa ya unga kutoka nje na baadaye wanayachakata wanazalisha maziwa hapa nchini. Kiwanda hiki cha Azam cha Zanzibar baada ya Kanuni mpya ambazo ziliwataka kila wanapo-supply maziwa kutoka Zanzibar kuingia nchini wanatakiwa walipe shilingi 2,000 kiwanda kilifungwa, wakashindwa kufanya hivyo. Kilipofungwa kiwanda, kukawa hakuna tena ajira zilizopo pale za Watanzania, zikawa zimesimama hakuna kitu kinaendelea. Tukaamua kwa dhati kabisa kwamba tuwape unafuu.

Mheshimiwa Spika, ukweli ni kwamba hatukuwapa punguzo lolote ila tuliwapa unafuu wa tozo. Kwa maana ya kwamba maziwa ya unga yanapoingizwa hapa nchini tunatoza 2,000, yanapoingizwa ya maji tunatoza 2,000. Sasa huyu anayeingiza ya unga akichakata anapata lita 8, anapoingiza Tanzania Bara anatakiwa alipe shilingi 16,000 kwa lita moja aliyoichakata.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tulichoona kwamba hapa Zanzibar wameajiriwa Watanzania wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania na hoja ilitoka kwa Wabunge hawahawa humu humu ndani, mkituomba kwamba hiki kianda tukiwezeshe kifanye kazi. Tulichokifanya sisi tunamtoza yule kwa equivalent. Tunamtoza kwa uwiano; kwa maana ya kwamba tunamtoza kwa equivalent ya kilo ya unga ambayo ni shilingi 2,000. Kwa hiyo unachukua shilingi 2,000 ukigawa kwa nane unakuta shilingi 250. Ndicho tulichokifanya ili kiwanda kile kiweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, lingine tulilofanya, sheria inasema maziwa yakitoka Zanzibar yakiingia huku yametoka nje ya nchi yanatakiwa kulipa import levy na maziwa yakitoka hapa low milk inayozalishwa hapa ikitaka kupelekwa Zanzibar kwa ajili ya kuchakatwa na yenyewe inatakiwa ilipe export levy. Tukasema sasa hii kwa sababu maziwa haya yamezalishwa na Watanzania, maziwa ya Watanzania hapa bara hayana soko, maziwa ya Watanzania yanayozalishwa Zanzibar hayana soko, tukasema hii tuiondoe kabisa, wakitaka kuingiza maziwa yaliyochakatwa kutoka Zanzibar ya Wanzanzibari wenyewe waliyoyazalisha, yakiingizwa hapa Bara wasilipe chochote.

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile maziwa yatakayochukuliwa hapa kwenda kiwanda cha Azam yaliyozalishwa na Watanzania hapa yakienda kule wasilipe chochote, ndiyo concept ya Serikali. Hakuna favour yoyote tuliyompa, na ndiyo maana tunaendelea kumtoza kwa sababu tu ya yale maziwa anayoyaagia kutoka nje ya nchi. Baada ya hapo, akiacha kuagiza kabisa ya nje ya nchi atatozwa asilimia sifuri.

Mheshimiwa Spika, baada ya haya niliyoyazungumza ninataka sasa nimalizie na baadhi ya hoja chache ambazo Waheshimiwa Wabunge wengine mbalimbali waliweza kuziuliza hapa. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri alivyojibu baadhi ya hoja mbalimbali hapa ile asubuhi alipopata fursa ya kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge; na akajaribu kutoa clarification nyingi sana juu ya hoja mbalimbali zilizotolewa za baadhi ya Waheshimiwa Wabunge, akiwemo Mheshimiwa Zitto Kabwe.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, mlizungumzia sana suala hili kwamba Serikali ya Awamu ya Tano hakuna jambo lolote ambalo imelifanya; Ilani yote haijatekelezwa; kama Mheshimiwa Naibu Waziri ambavyo aliweza kuzungumza ile asubuhi. Lakini hoja hii ameizungumza kwa nguvu sana Mheshimiwa Zitto Kabwe, akasema na Wizara inajivunia tu faini n.k. hakuna kinachofanyika, Serikali ya Awamu ya Tano hakuna jambo lolote iliyofanya katika Ilani ya Uchaguzi. Nilikuwa nataka Mheshimiwa Zitto Kabwe angekuwepo hapa; kwa sababu kwa muda mrefu sana amekuwa hata akitoa takwimu za uongo juu ya ukweli na uhalisia wa utekelezaji wa shughuliza Serikali ya Awamu ya Tano, lakini wakati mwingine na kuonekana chuki dhahiri juu ya Serikali hii ya Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Spika, anawadanganya watu kwamba mapato yalipanda mwaka ule wa 2014 na leo yameshuka, yamekuwaje, Serikali hii hakuna hatua yoyote nyingine ambayo imeichukua juu ya mambo haya.

Mheshimiwa Spika, sisi tunakwenda vizuri. Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi juu ya ujenzi wa bandari tumejipanga vizuri. Sasa hivi upembuzi yakinifu unafanyika na mkandarasi wetu yuko kazini anafanya kazi hiyo na Serikali imeshatenga na imeshaanza kumlipa na hivi karibuni atatoa ripoti ambayo itatuonesha tukajenge wapi bandari. Tayari mazungumzo tumeshayafanya na Serikali ya Korea na tuko vizuri katika kutafuta fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mradi huu unatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, TAFICO imeanzishwa na tayari tumepata billion 4.2 kutoka Japan kwa ajili ya kuboresha baadhi ya miundombinu iliyoko pale. TAFICO Business plan imeshaandaliwa kwa kulitekeleza jambo hili. Sasa unaposimama hata kama una chuki namna gani, hata kama una chuki namna gani na Serikali hii ya Awamu ya Tano ni bora hata ukawa mvumilivu tu; kwa sababu hakuna namna yoyote ambayo Serikali ya Awamu ya Tano inaweza ikashindwa kutekeleza majukumu yake eti kwa sababu ya watu wawili watatu ambao wana chuki nayo.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kuhakikisha kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inatekeleza majukumu yake, Ilani ya Uchaguzi inatekelezwa kwa kiwnago kikubwa. Ni vizuri sana Mheshimiwa Zitto Kabwe asiiharibu ile rekodi tuliyoiweka naye enzi hizo. Tuliweka rekodi nzuri ya michango mizuri hapa Bungeni ambayo imelisaidia taifa hili lakini ameanza na kuku- attack mpaka wewe Mheshimiwa Spika ambaye ndiye muasisi wa mageuzi, sio uchonganishi!

Mheshimiwa Spika, ninachosema, siku ya ESCROW, Mheshimiwa Spika, akiwa Naibu Spika wa wakati huo ndiye aliyeamua Mpina aingie kwenye Kamati ya ESCROW, Kangi Lugola, Hamis Kigwangalla aingie kwenye Kamati ya ESCROW na maombi hayo yaliombwa na Filikunjombe pamoja na Zitto Kabwe. leo hii Zitto Kabwe anasimama katika Bunge hili, na maeneo mbalimbali kuzungumza hata maneno ya uongo dhidi ya Mheshimiwa Spika ambaye mimi nasema kati ya watu ambao wametengeneza viongozi humu Bungeni kwa watu ambao hamuijui historia ni Mheshimiwa Job Ndugai Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Na watu waliomtengeneza hata Mpina Mheshimiwa Job Ndugai yumo, sio mtu mwepesi wa kusimama na kumnyooshea kidole, sio mtu mwepesi kihivyo unless ni kwa watu ambao wasioijua historia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Job Ndugai amefanya mambo makubwa ya nchi hii. Sasa ukiendesha kwa chuki zako, Rais John Pombe Magufuli ni kwa sababu watu tu hawamjui, laiti wangekuwa wanaijua siri ya Mheshimiwa John Pombe Magufuli hata wale ambao wanaongea haya na yale kule wasingepoteza huo muda. Hakuna mtu atakayemkwamisha Mheshimiwa John Pombe Magufuli kutekeleza majukumu yake, kwa chuki, kwa hila, kwa namna yoyote na wala wanaotegemea kwamba anaweza akayumba wala kuyumbishwa kwa maneno ya hapa na pale wasitegemee hilo.

Mheshimiwa Spika, Rais huyu ni Rais ambaye ameshavuka mipaka mingi ya viongozi, na historia ya Tanzania itaandika, sisemi haya mimi Mpina kwa sababu ni Waziri hapa, niwe mwananchi wa kawaida kabisa kwetu nyumbani Meatu Mwamuge nitasema haya, kwamba Rais Magufuli ni wa mfano na wa kuigwa mfano katika taifa hili. Niwe Mbunge wa kawaida nitayasema haya, niwe Waziri hivi nitayasema haya. Ni mara chache kupata viongozi wako committed namna hii, anatakiwa aungwe mkono na Watanzania wote katika mageuzi anayoyafanya ya ukombozi wa nchi yetu. Ni mara chache sana kumpata Rais ambaye akiamua kupasua hapa anapasua, na mnalijua tatizo la kupasua bila kuangalia. (Makofi/Kigelegele)

Mheshimiwa Spika, ukipasua bila kuangalia, utapasua mjomba wako, unapasua shangazi yako, utapasua mali za watu ambao hawakamatiki, utapasua mali za watu ambao huwezi kuwagusa nchi hii. Kwa hiyo ni mara chache sana ndiyo maana viongozi wengi wanayumba kwa sababu ya kukosa misimamo hiyo. Mimi nataka kama taifa tumuunge mkono Rais huyu tutafika mbali katika ukombozi wa nchi yetu, tuijenge nchi yetu, tuache hizi siasa nyepesi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, someni! Ooh! Nimejisahau.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana, lakini nimalizie kwa kusema kwamba, safari ya mageuzi ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi imeanza, tena iko hatua nzuri. Nami na wasaidizi wangu kama tulivyoahidi na tunaendelea kuwaahidi Wabunge, tutatumika sisi kwa nguvu zote, watendaji wangu hawa, waoneni hawa, wana mateso makubwa, kuwa mtumishi halafu chini ya Wizara ya Mpina, wana mateso makubwa. Pale Wizarani tumeshakubaliana kwamba muda ni namba tu, kwa hiyo hatujali muda gani, hatujali sasa hivi ni usiku katika kufanya majukumu yetu na tunaendelea kuwahakikishia, sisi tutakuwa vibarua hivyo, mpaka tutakapomaliza hili jukumu na tumejitoa hivyo mimi na wasaidizi wangu kuhakikisha kwamba mageuzi haya yanapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi na Naibu Waziri wangu hapa, tunafanya hivyo, hakuna gain yoyote, hakuna any personal gain tunayoipata zadi ya maslahi ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa kusema kwamba, sasa baada ya kuwa nimemaliza kutoa maelezo yangu hayo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wasitucheleweshe, waipitishe hii bajeti tu mara moja, tusifike hata hiyo saa kumi na mbili ili tuwahi kwenda kutekeleza, kwa sababu, majukumu ya wafugaji na wavuvi yanatusubiri sana na wengine wadau wako hapahapa wanamhitaji Waziri, kwa hiyo, kuendelea kuchelewesha kupitisha bajeti itachelewesha utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, naafiki.