Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kunipa nafasi hii. Mimi natoka kwa wafugaji, baba yangu alikuwa daktari wa mifugo kwa hiyo, ninaelewa mambo mengi sana ya mifugo.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kujiweka kabisa kwamba anapenda wafugaji na anapenda mifugo. Nina hakika kuwepo kwake kutasaidia sana kwa wafugaji kuweza kunufaika na kutoa mchango mkubwa kwenye mapato ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, mifugo imeongezeka na mazao ya mifugo yameongezeka. Pamoja na hivyo mifugo mazao yake ni protein kwa binadamu. Mazao ya chakula na mazao ni malighafi, mazao ya mifugo ni malighafi ya viwanda vyetu. Wakati huohuo nataka niwaambie, kwamba mifugo inaweza ikatoa mapato makubwa kuliko sekta nyingine yoyote kama tutaiangalia vizuri. Hata sasahivi mchango wa mifugo, mazao yake na bidhaa ni kubwa sana kwa Serikali hii. Vilevile nilipokua nikifanya kazi NDC kiwanda cha viatu bora cha kilikuwa namba mbili ya kutoa mapato Serikalini; kwa hivyo hii inaonesha kwamba kama tutaisimamia hii sekta vizuri kwa kweli wafugaji watanufaika na taifa nalo na Serikali itanufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na michango hii mikubwa, na sitaki kurudia takwimu kwa sababu Waziri ameweka takwimu vizuri na waliotangulia wameongea juu ya takwimu vizuri. Nikirudia haitasaidia lakini ni wazi kwamba mchango wa mifugo na mazao yake ni mkubwa sana kwa taifa letu. Hata hivyo, pamoja na mchango wa mifugo katika maeneo mbalimbali sekta hii inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo kama tutaziondoa wafugaji watanufaika, Taifa hili litanufaika.

Mheshimiwa Spika, ya kwanza, ni kutokutekeleza matumizi ya ardhi na wanajua kabisa kwamba hakuna mfugaji mmoja mmoja mwenye eneo isipokuwa Serikali yenye ranchi. Wafugaji wanakuwa na ardhi ambayo ni ya pamoja (communal) na haiwezekani kuwa ya mmoja mmoja jamani. Kwa hivyo Serikali yetu ikiweza ku-protect au kulinda maeneo hayo ambayo ni communal ya wafugaji wa jadi na wafugaji wa kisasa, nina hakika wafugaji hawatapata migogoro wanayoipata sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, migogoro hii iko kati ya hifadhi na wafugaji, kati ya wafugaji na wakulima na wengine. Kama maeneo ya wafugaji kwanza yatajulikana na yatalindwa, migogoro hii itapotea bila ya nguvu kubwa jamani na naomba hili lifanyike na tutaondoa migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ya pili ni rushwa; kama kuna watu wanaumizwa na rushwa nchi hii ni wafugaji na hasa kwenye hifadhi. Nina mfano mzuri kule kwa Mheshimiwa Millya aliyemaliza kuongea, ng’ombe wa mfugaji wamekwenda kuchukuliwa nyumbani kwa sababu hawapati watu wanaopeleka mifugo kwenye hifadhi. Wamewapeleka kwa kuwadanganya kwamba wanawapeleka mahali pazuri, lakini kumbe wanawapeleka kwenye hifadhi na siyo rahisi kwa mfugaji wa kawaida kujua kwamba mipaka ya hifadhi ni wapi, naomba na hili lionyeshwe. Walipofika kule, wameambiwa mpo kwenye hifadhi, lipeni milioni 10 na wale wakakataa na sasa wapo mahakamani na inawezekana wakashindwa na hii ni laana kwa kila mmoja; kwa yule aliyehusika na hata Serikali yetu itahusika kwa namna fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, suala hili la rushwa liangaliwe na sekta hii iwalinde wafugaji wasiungane kwa sababu nakubali kwamba kuna wachache ambao wanaingiza mifugo kwenye hifadhi, lakini wengi wanaonewa kwa sababu uelewa wao kule porini si mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu, nataka niwaambie kwamba bila kuangalia mifugo, wafugaji watapotea na nchi hii itapata hasara kwa sababu nimewaambia kwamba bila kuwatetea hawa wafugaji, hakuna namna. Nataka niwaambie kwamba jamani kuna suala la dawa feki na kuna watu ambao wanataka washikilie wafugaji wawaone kwamba ni wazuri kumbe wanawashikilia wafugaji kwa sababu wanataka kupeleka dawa feki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Serikali na Wizara hii, Waziri naomba wasimdanganye, ataniuliza kwa nini nasema hivyo, wanakuwa karibu na yeye halafu wafugaji wanapelekewa dawa feki na ng’ombe na wafugaji wanaumia. Namwomba sana Waziri namwamini lakini si rahisi kuwajua watu ambao wanataka kunufaika kwa kuonekana ni wazuri lakini kumbe ni ubinafsi wao wenyewe. Naomba dawa hizi feki ziangaliwe, chanjo za ng’ombe ziwe na uhakika na dawa za tiba ziwe na uhakika, nina hakika Sekta hii itakuwa na mchango mkubwa sana kwenye uchumi wa nchi hii, itawanufaisha wafugaji, umaskini utapungua; tuwasaidie wafugaji na Mungu atawabariki nyie wote. Ahsanteni. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Mary Nagu.

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Kila siku nasahau kutoa hoja, lakini naunga masuala yote ya Serikali. Naunga kwa mikono yote miwili bajeti hii na mimi nipo pamoja na wao. (Makofi)