Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ya siku ya leo kwa uhai na baraka tele katika maisha yetu. Nina mambo machache ya kuchangia; la kwanza, niipongeze Wizara kwa kazi nzuri ambayo tumesoma kwenye bajeti yao na kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri na nimshukuru kwamba sasa hivi wamekubali kukata vitalu kwa ajili ya wafugaji ambao wanazunguka maeneo ya ranch.

Mheshimiwa Spika, kwetu Dodoma tuna ranch ya Kongwa na wananchi wanakwenda pale kwenye vitalu vile kwa ajili ya ufugaji, lakini kitu ambacho naona ni kigumu kwa wananchi wangu ni kulipishwa ng’ombe mmoja Sh.10,000 kwa mwezi. Naona gharama hii ni kubwa sana, kwa sababu ranch wanapoingia hakuna majani ambayo yamepandwa na watumishi wa ranch, hakuna dawa ambayo wanapewa mifugo wanaoingia katika vitalu vile. Kwa hiyo ukisema kwamba mfugaji mmoja ana ng’ombe 50 tu na ng’ombe 50 kwa Dodoma ni ng’ombe wachache sana, ng’ombe 50 kwa mwezi akiingiza kwenye kitalu cha ranch ni Sh.500,000 kwa mwezi mmoja.

Mheshimiwa Spika, niiombe Wizara ione namna ya kupunguza bei hii ambayo ni kubwa katika vitalu vyetu ili kuwasaidia wafugaji. Hawana maeneo ya kuchunga ng’ombe, hawana maeneo kabisa na wanapomtoza mfugaji shilingi 10,000 kwa ng’ombe mmoja, akitoka pale hana pa kuuza maziwa, Dodoma hatuna kiwanda cha maziwa mpaka uende Arusha au mpaka mfugaji apeleke maziwa Iringa, kitu ambacho ni kigumu na ni gharama sana kwa mfugaji.

Mheshimiwa Spika, mbali ya hivyo wangetoa elimu wa wale ambao wanafuga katika vitalu vyao, hakuna elimu yoyote inayotolewa kwa wale wafugaji ambao wanafuga kwenye vitalu vya ranch na wanashindwa kununua mitamba ile, bora wangeruhusu mitamba ya ranch ikapanda ng’ombe za shilingi 1,600,000. Sasa mfugaji achunge ng’ombe kwenye kitalu Sh.10,000 kwa mwezi kwa kila ng’ombe, lakini akitaka mtamba anunue kwa Sh.1,600,000, sio haki. Naomba sasa Wizara iangalie namna ya kusaidia wafugaji wanaoingia kwenye ranch ambao wamekodi vitalu kwa bei ndogo, lakini wapate elimu na zaidi ya elimu wakubaliwe mitamba ya ranch iwapande ng’ombe wa wale ambao wako kwenye kitalu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, ni suala la chuo chetu cha TARILI cha Mpwapwa chuo hiki ni cha siku nyingi, ni chuo cha zamani, kinazalisha wataalam wazuri na kimepewa eneo kubwa sana na Serikali ya Wilaya ya Mpwapwa, lakini hawana vifaa, watumishi vibarua wa pale hawalipwi, waliokuwa wanashuhgulika mashambani kulima na kupanda majani kwa ajili ya ng’ombe walikwishaacha kazi, wala haki zao hawajalipwa. Hata hivyo, vibarua waliopo kuna vibarua 70 pale, nadhani wapo zaidi ya 70 hawajawahi kulipwa. Niombe kama kweli chuo kile ni cha thamani kwa Serikali yetu, kama chuo kile kina manufaa kwa nchi yetu, Serikali ione namna sasa ya kukisaidia kile chuo hata vifaa hawana, wanatakiwa kulima na kupanda mazao kwa ajili ya ng’ombe wale wanaowafuga pale na ng’ombe wa Mpwapwa ni wazuri mno ni wazuri sana hata kwa wafugaji wa mmoja mmoja, lakini hawana vifaa. Naomba Serikali sasa iwahudumie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme tena juu ya Kiwanda cha SAAFI kilichopo Rukwa, na-declare interest kwamba mimi ni Mjumbe wa PAC na tumekagua fedha ambazo zilitolewa na Serikali kwa ajili ya kiwanda hiki, ni zaidi ya miaka mitano Serikali haijafaidi kitu chochote na hiki kiwanda na Serikali ilisema inaingia ubia na yule mwekezaji na wakaingiza zaidi ya bilioni 10 kwa ajili ya kiwanda hiki, lakini hakuna manufaa yoyote ambayo Serikali inapata kupitia Kiwanda cha SAAFI. Naomba Serikali sasa leo watakapohitimisha watuambie ni nini ambacho kinaendelea juu ya kiwanda hiki maana fedha zile ambazo ziko pale zilizowekezwa ni mali ya umma, ni mali ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongelee pia machinjio ya Ruvu, Serikali imeweka fedha nyingi sana pale Ruvu fedha nyingi, tulijenga machinjio ya Ruvu kusaidia machinjio ya Dodoma, kusaidia machinjio ya Vingunguti lakini majengo yale yamekaa bure tu hayana kazi. Fedha za Serikali zimeingia mle lakini hakuna kinachoendelea. Tuliambiwa mashine zilishaletwa pale kwa ajili ya machinjio ya kisasa, hakuna kinachoendelea, je, tunaanzisha miradi ili tuache njiani kweli? Je, tunatumia fedha za umma ili zikae ziharibike bila matumizi, sidhani kama ndio lengo la Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali ni kuanzisha mradi na kuona kwamba mradi ule unawafaidisha Watanzania na wako wanaotafuta na wanachinja nyama hapa Dodoma ng’ombe, mbuzi, kondoo kusafirisha nchi za nje, machinjio ya Ruvu yangesaidia hata machinjio ya Dodoma, lakini majengo yale yamekaa pale hayana kazi. Naamini na vifaa vilishakuja lakini hakuna kinachoendelea na sijui kama vile vifaa viko Wizara ya Mifugo au vile vifaa vilishauzwa au bado viko bandarini mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Wizara kwamba wameamua sasa kupitia Ranch ya Ruvu kwamba wameingia ubia na RIDP kwa ajili ya kujenga kiwanda kikubwa kwa ajili ya kuchinja, kwa ajili ya kupaki nyama na kwa ajili ya mambo kama haya yanayohusu mifugo. Ni jambo jema kabisa, lakini kwa nini tusitumie ranch zetu, ranch ya Kongwa ina mifugo mingi, nadhani kwamba ni vizuri ranch zetu zikasadia kuwa mfano na tukajenga viwanda vya maziwa, vya nyama katika ranch zetu kuliko kujenga maeneo ambayo hayana mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)