Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi naomba nichukue nafasi hii kama walivyofanya wenzangu nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri na uwasilishaji wake mzuri. Mimi nilikuwa na tatizo moja ambalo niliomba Serikali iangalie kwa jicho la huruma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vyuo vilivyofungwa ni pamoja na chuo changu cha St. Joseph, Songea ambacho kilikuwa na maeneo mawili; eneo la kwanza ni eneo la campus ya kilimo na eneo la pili ni campus ya teknolojia. Hiki chuo kimefungwa, lakini sina tatizo na sababu za msingi ila nilichokuwa nakiona ni kwamba uamuzi huu umechukuliwa mkubwa mno, haulingani na mazingira halisi, sisi sote tunataka vijana wetu wapate elimu na kwa sisi Songea kile chuo cha St. Joseph ndio chuo kikuu pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo zipo sababu za msingi zilizosemwa na kubaliana nazo lakini vilevile ningeomba nishauri, kwa mfano suala la udahili wa wanafunzi ambao hawajafikia viwango, Mheshimiwa Waziri ametuambia hapa kwamba vijana 424 wamefutiwa udahili wao. Lakini hawa vijana 424 ni kati ya vijana 3,585. Ukiangalia takwimu hizi maana yake waliokiuka taratibu ni asilimia 11.8; kwa hiyo vijana asilimia 88.2 hawana tatizo lolote. Kwa hiyo, haiwezi kufika mahali hiyo ikawa moja ya sababu ya kufunga vyuo au kuvifuta vyuo. Ukiangalia sababu hizi sio sababu zinazotokana na vijana ni sababu zinazotokana na utawala wa chuo, utawala wa uongozi wa TCU na viongozi wengine wa Wizara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo huwezi ukafika mahali makosa ya kiwizara yakaenda kutoa adhabu kwa chuo ambacho chenyewe kilikuwa haina kosa. Lakini yako matatizo ambayo yamesemwa kutokana na vyuo hivi na hasa chuo changu; matatizo ya uongozi, matatizo ya utawala na matatizo ya kitaaluma. Sitaki kubishana na Mheshimiwa Waziri ni kweli makosa hayo yanajitokeza lakini ufumbuzi wa makosa hayo sio kufuta chuo, ufumbuzi wa makosa hayo ni pale ambapo una kitaka chuo au taratibu zilizokosewa ziweze kurekebishwa. Na kama kurekebishwa hakuwezekani zipo taratibu za kudhibiti uongozi uliopo; lakini sasa ukiangalia uamuzi wetu wa kufuta hivi vyuo umekuja kuwahukumu moja kwa moja wahusika kwenye vyuo ambao ni wanafunzi wetu na utawala kwa ujumla wa chuo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie kwamba siku zote wanasema ukiwa na mtoto umemuogesha kwenye dishi (beseni), maji yakichafuka unachofanya ni kuyatupa maji, huwezi kuondoa dishi na mtoto ukaenda kuwamwaga kwa sababu maji yamechafuka, huo sio utaratibu.
Kwa hiyo, kama makosa yalifanywa na uongozi na kama makosa yalifanywa na Wizara yenyewe kwa kutumia vyombo vyake kule kilichotakiwa ni kuona namna gani tunaadhibu wale waliohusika na wala sio vijana waliokuwa wanasoma au utawala wa chuo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi taratibu zilizotumika kukifuta kile chuo maana kimefutwa, sio kimefungwa, kimefutwa usajili wake, hati yake ya kuongoza kile chuo imefutwa rasmi. Kwa hiyo, uaratibu uliotumika katika kukifuta chuo hiko haukuwa sahihi na kuna sababu kadhaa. Kwanza uamuzi wenyewe wa kukifuta chuo ni wa ghafla mno haukuwa na taarifa yoyote, notice yoyote ya kuwajulisha kwamba baada ya hapa tunafuta chuo, ni uamuzi ambao umetokana na taarifa walizozipokea, wakaamua hata uongozi umepata taarifa za kufutwa chuo kutokana na vyombo vya habari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, tumewaadhibu watu wengine ambao hawana hatia, kulikuwa na wanachuo kutoka makundi mbalimbali, tumeamua kuwahamishia vyuo vingine, lakini kuna watu walikuwa wanasoma kama part time pale anatoka kazini anakwenda kufanya masomo, kwa hiyo maana yake kumuhamishia maeneo mengine kwanza unamuingiza kwenye migogoro ya kulipa ada, vilevile unamuingiza kwenye migogoro ya kiutumishi kati yake yeye na ofisi yake.
Kwa hiyo, nilikuwa nafikiri maeneo hayo yote yangeangaliwa kabla ya kutoa uamuzi huo. Athari yake ni nini? Kwanza sisi wenyewe kama Kanda ya Kusini tumeathirika sana, tumeathirika sisi kama Mkoa wa Kusini lakini vilevile na wanafunzi hawa wameathirika sana kisaikolojia, kiuchumi na kijamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, matokeo yake huwezi ukategemea vijana hawa wanakohamishiwa wakaenda kufanya vizuri katika taratibu zao za kimasomo kwa sababu athari hiyo imekuwa kubwa sana na imewaumiza sana vijana wale. Lakini vilevile kimkoa sisi tumekosa mambo mengi sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, chuo hiki pamoja na shughuli nyingine walizokuwa wanafanya, lakini vijana hawa ndio walikuwa wakiwa kwenye field wanakwenda kwenye taasisi zetu mbalimbali za kielimu; walikuwa wanajitolea kwenye vyuo, wanajitolea kwenye shule, wanafanya tafiti mbalimbali ambazo zilisaidia kuwezesha mkoa kuinua kiuchumi.
Lakini sio hilo tu, hata hali ya kiuchumi ya wananchi katika maeneo yale ilikua kutokana na kuwepo kwa chuo hiki, wananchi wengi walifanya shughuli zao, wananchi wengi walijenga nyumba mbalimbali ambazo kuwepo kwa wanachuo hawa kulisaidia sana kuinua uchumi wa wananchi na kusababisha mzunguko wa fedha kwa jamii ya Songea Mjini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, athari hizi zimetukuta wote, kwa hiyo tunaomba Serikali kwa sababu mmeshatoa adhabu kwa TCU, nilikuwa naiomba Serikali ione uwezekano wa kuamua kukirudisha chuo hiki cha Songea pamoja na masharti ambayo mnaona yatafaa ili waweze kuyarekebisha. Lakini kukifuta moja kwa moja naona sio sahihi na haitakuwa kuwatendea haki wanafunzi na ndugu zetu wa Songea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, na tuna maswali ambayo tunajiuliza, je, kwa nini TCU iliamua kutokutoa notice kwa chuo? Lakini la pili kwa nini TCU haikutoa muda na nafasi ya chuo kufanya marekebisho yale ambayo waliyapata?
Vilevile tunajiuliza je, kwani Serikali haina namna bora nyingine ya ufungaji wa chuo lazima kukifunga chuo kwa ambush maana kimefungwa kile chuo utafikiri tupo jeshini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri tuangalie. Lakini vilevile tunajiuliza sana sisi Songea kwamba kile chuo kilichokuwa na matatizo kwa mujibu wa maelezo ya Wizara na TCU, ni kile chuo cha campus ya kilimo lakini chuo cha TEHAMA hakikukuwa na tatizo, kwa nini katika kufuta vimefutwa vyuo vyote viwili wakati campus ya TEHAMA haikuwa na matatizo.
Kwa hiyo, nilitaka niiombe Serikali yangu tukufu ione utaratibu wa kufanya ukaguzi, kutoa ushauri, kutoa maelekezo ili ifike mahali yale ya msingi yaweze kuondolewa na wakati huo huo kutoa haki kwa kile chuo kiweze kuanza tena usaili ili kuwarudisha wanafunzi katika chuo kile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya uongozi wa chuo kile na kwa niaba ya uongozi wa Songea kwa ujumla tupo tayari kupokea.