Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa fursa. Naomba nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Manaibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya katika sekta hii. Nami naunga mkono hoja moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako naomba nitumie nafasi hii vilevile kutoa pole kwa Watanzania wote wakiwemo wananchi wa Kyela, kwa matatizo makubwa waliyoyapata hasa baada ya mvua hizi kubwa kunyesha, kupata mafuriko, wamepoteza mazao, wamepoteza watu, wamepoteza maisha na vilevile miundombinu kuharibika. Leo hii ninavyoongea wasaidizi wangu wako Jimboni Kyela wakigawa chakula kwa walioathirika sana. Kwa hiyo, hata Waheshimiwa Wabunge ambao wanaweza wakapata huruma kidogo basi tunapokea michango tutaifikisha hapo kwa waathirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pengine niongelee kitu kifupi sana maana dakika tano siyo nyingi, kuhusu suala la ushirika ambalo aliongelea Msemaji Mkuu wa Kambi ya Upinzani, kwamba ushirika ni tabu tu kwa wakulima, lakini pengine kwa mazao mengine, lakini naomba niongelee zao la kokoa kwamba, ushirika ndiyo mkombozi kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu sana sisi Kyela tunazalisha sehemu kubwa ya kokoa nchini. Kokoa haijawahi kupanda bei zaidi ya Sh.3,000 kwa kilo, hiyo ni bei kubwa sana, lakini kuanzia Novemba, tulipoanzisha huu mfumo, tumeweza, kupitia hii minada, kupata bei nzuri ya kuanzia Sh.4,500, haijashuka imeendelea kuwa Sh.5,000, ikaenda Sh.5,600, tunaelekea kwenye Sh.6,000 sasa hivi kwa kilo. Vilevile mfumo huu umetufanya tuweze kuelewa pia unyonyaji mkubwa unaoendelea, hasa kutokana na wenzetu hawa wa katikati hawa, kwingine wanaitwa kangomba, sisi tunaita njemke.

Mheshimiwa Spika, kule kwetu kilo moja, lakini wala siyo kilo, ni kitini kimoja kinaitwa sado, ni Sh.800 analipwa mkulima, lakini hicho hicho kitini kimoja kinaitwa sado, kina kilo tatu ndani yake. Kwa hiyo, mkulima analipwa Sh.800, yeye akienda kwenye soko, anapata zaidi ya shilingi elfu 16, ni unyonyaji mkubwa sana! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nafurahi kwamba Serikali imeshatunga Sheria ile ya Microfinace Act ya 2018 ambayo inatupa msingi sasa wa sisi kuweza ku-regulate hii, hatuwafukuzi hawa watu, lakini kuwa-regulate sasa, kwa sababu chini yah ii sheria tunaweza kabisa tukatunga kanuni ambayo inaendana na zao kwa zao. Kwa mfano, mimi mwenyewe, nitakuwa wa kwanza katika kukimbilia kwa hii fursa kwamba tuwe na kanuni kwa zao la kokoa kwa kuwaelewesha ili hao wenzetu njemke wasipate faida kupitiliza, angalau nusu ibakie kwa mkulima na yeye nusu ifidie gharama zake za kwenda huko na kule. Kwa kweli ni kazi ambayo inawezekana kabisa ikafanyika na ikaleta tija katika soko.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, ni suala ambalo tuliliongelea juzi, aliliongelea Mheshimiwa Mwambe hapa la Ministerial responsibility. Alisema lazima Waziri anapofanya kosa sisi tuliseme hapa, ni kweli kabisa hakuna tatizo kabisa kuhusu Ministerial responsibility. Nilichokuwa nalalamikia mimi ni kwamba kuna suala ambalo, haliihusu hiyo Wizara yenyewe, lakini linahusu Mawaziri watatu, wanne, si sahihi ukam-single out Waziri mmoja huyo huyo kwa kumrushia mawe. Sasa inakuwa kama una kitu fulani kwake, ndiyo maana nikasema, chini ya Ibara ya 53, sisi ndani ya Bunge, chini ya Waziri Mkuu, tunawajibika kwa Bunge kwa pamoja, (collectively), kwa hiyo, ndiyo hicho nilitaka kufafanua tu waelewe kwamba sasa kama kuna Mawaziri wawili, watatu wanahusika, mmoja tu ukiendelea kumtupia mawe siyo sahihi hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili ni suala letu, hata mimi mwenyewe ukinilaumu, mimi mwenyewe nitaitetea Serikali hapa kwa sababu ni suala la kiserikali na hakuna ambaye amelikimbia na bado ulivyomsikia Waziri wa Viwanda na Biashara, ameeleza vizuri sana, hoja nyingi sana hapa zinaweza kuyeyuka kama mshumaa.

Mheshimiwa Spika, nimalizie tu kwa kusema, naunga mkono hoja. (Makofi)