Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia hoja hii kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kushika kalamu na kutoa mchango wangu kwa njia ya maandishi. Kwanza nianze kwa kuwapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote watatu pamoja na Makatibu wote kwenye Wizara hii bila kuwasahau Wakuu wa Taasisi zote zilizopo kwenye Wizara hii kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya kwa kipindi kifupi walichopewa kufanya kazi kwenye Wizara hii. Kwa kweli sasa tumeanza kuona matunda ya kazi zenu kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Liwale ni miongoni mwa Wilaya zinazolima zao la korosho na mazao mengine ya chakula na biashara kama vile ufuta, mbaazi, mtama na muhogo. Tatizo kubwa la wakulima wa Liwale ni upatikanaji wa masoko ya mazao hayo, Wilaya ya Liwale haina soko la uhakika la mazao ya biashara. Shida nyingine kubwa sana katika kilimo ni uhaba wa maghala ya kuhifadhia mazao hasa inapokuja kwenye msimu wa korosho. Mwaka huu korosho kwa mfano zimekaa muda mrefu sana kwenye maghala madogo ya vyama vya msingi, maghala ambayo hayana ubora hivyo kuharibu ubora wa mazao husika. Hivyo naiomba Serikali kuipatia ujenzi wa maghala kwenye halmashauri yetu.

Mheshimiwa Spika, malipo ya korosho kwa Wilaya ya Liwale bado si wa kuridhisha kwani wakulima wote wakubwa bado hawajapata malipo yao japokuwa uhakiki ulishakamilika. Naiomba Serikali kuangalia malipo haya japo msimu wa maandalizi wa mashamba umeshapita na wakulima hao hawajui hatma ya mashamba yao. Pamoja na kauli ya Mheshimiwa Rais alipokuwa ziarani Mtwara kuamuru wakulima wote walipwe, jambo hili kwa halmashauri ya Liwale halijatekelezwa kabisa.

Mheshimiwa Spika, Skumu ya Umwagiliaji ya Kata ya Ngongowele Wilayani Liwale ni ya muda mrefu sana. Hatma ya mradi huu hadi leo hatujui hatma yake licha ya kutengewa fedha kila mwaka; fedha za awali zaidi ya milioni 700 zimeliwa bila mafanikio. Naiomba Serikali kuja na timu maalum ili kufanya ukaguzi ili kuona namna mrdai huu ulivyohujumiwa.

Mheshimiwa Spika, idara ya kilimo katika halmashauri ya Liwale pamoja na changamoto nyingi lakini uhaba wa watumishi wa kada hii ni mkubwa; sambamba na uhaba wa vitendea kazi kama vile magari na pikipiki kwa ajili ya maafisa ugani. Kulikuwa na mradi wa upandaji wa miche ya mikorosho, vikundi mbalimbali vilihamasishwa kuanzisha vitalu vya miche ya mikorosho lakini hadi leo vikundi hivi bado havijalipwa malipo ya upandaji wa miche hii. Watu hawa walichukua mikopo kutoka kwenye taasisi za kifedha hivyo sasa watu hawa wako kwenye hatari. Naiomba Serikali kuwalipa watu hawa madai yao.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Liwale inapakana na Pori la Akiba la Selous hivyo kuna changamoto kubwa sana ya wanyama waharibifu kuharibu mazao ya wakulima. Wanyama hawa ni kama vile nyani, nguruwe, viboko na tembo. Hivyo naiomba Wizara ikisaidiwa na askari wa wanyamapori kuja na mkakati maalum wa kuwasaidia wakulima hawa namna ya kuanzisha vikosi vya misako ya mara kwa mara, misako ambayo inahitaji msaada wa vifaa kama bunduki ndogo, nyavu za kusakia na zana nyingine za kusaidia kupunguza athari za uharibifu huo.