Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Kilimo ambayo kimsingi ni uti wa mgongo wa taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Wakulima wa Miwa. Kumekuwa na kilio cha muda mrefu sana cha wakulima wa miwa wa bonde la Ruhembe Jimboni Mikumi ambao ni wakulima wa miwa wa nje (out growers) katika ukanda wa Bonde la Ruhembe ambapo malalamiko yao ya muda mrefu ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, idadi ya miwa inayoingizwa kiwandani kutoka kwa outgrowers bado imekuwa ndogo sana hivyo tunaomba sana Wizara iliangalie suala hili kwa kuwa tumewashauri sana wakulima na watu wengine walime miwa kwa wingi, lakini miwa inayochukuliwa na kiwanda ni kidogo. Hali hii inasababisha miwa mingi ya wakulima wa nje kutochukuliwa na kiwanda, hasa ukizingatia pia kuwa kiwanda nacho kina mashamba yake.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Mzani. wakulima wa miwa wamekuwa wakilalamikia sana mzani unaotumika na kiwanda cha Illovo kwa kuwa mzani ni wa Illovo na wanaopimia ni watu wa Ilovo hivyo wakulima wanakosa wawakilishi wa kuwawakilisha ili kuhakikisha kuwa kiwango cha miwa na utamu kweli vinaendana na uhalisia. Hivyo wakulima wanaomba sana wapate mzani wao au wawe na uwakilishi wa kutosha katika mzani unaotumiwa na kiwanda cha sukari cha Ilovo.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Utamu wa Muwa (sucrose). Kumekuwa na malalamiko makubwa kutoka kwa wakulima wa miwa kwamba kwa kuwa hawana wawakilishi wakati wa upimaji wa utamu wa sukari, basi wamekuwa wanapewa takwimu ambazo si sahihi, hivyo kuwafanya walipwe pesa kidogo sana kutokana na vipimo vya sukari vinavyoonesha kuwa miwa yao ina utamu kidogo tofauti na uhalisia. Kwa kuwa kuna wakati wanaambiwa miwa yao ina sucrose mpaka nne (4), kitu ambacho wataalamu wanasema hakuna kiwango hicho kwa miwa ya bonde la Ruhembe, bali inakuwa kwenye 10 -11 na si hizo takwimu ambazo wanaambiwa na watu wa kiwandani.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Mabaki (Maganda ya Miwa – Bagasse). Wakulima wameendelea kulalamika kuwa wanalipwa utamu tu wa miwa na hawalipwi mazao mengine yanayotokana na miwa kama mashudu (bagasse) ambazo zinatengenezewa umeme na nyingine zinatumika kama mbolea. Pia wamekuwa hawalipwi molasses ambazo zinatumika kwa ajili ya kutengeneza sprit, hivyo kilio kikubwa cha wakulima kwa Serikali ni kuhakikisha wakulima hawa wa miwa wanalipwa na vitu vingine vinavyotokana na miwa kama bagasse na molasses sambamba na sucrose (utamu) ili kuuinua uchumi wa wakulima wetu wa nje.

Mheshimiwa Spika, Kuhusu Pembejeo. Kama Kambi Rasmi ya Upinzani ilivyoshauri, kilio kikubwa cha wakulima ni ukosefu wa pembejeo kwa wakati. Ili tupate kilimo bora ni vema sana Serikali ikahakikisha kuwa upatikanaji wa pembejeo unapatikana kwa wingi na kwa haraka
iwezekanavyo. Kwa mfano kwenye Wilaya yetu ya Kilosa pia tumekuwa na ucheleweshaji mkubwa sana wa pembejeo. Pia zimekuwa na tatizo la kupatikana kwa bei ya juu sana na inapanda kila mwaka na kufanya wakulima wetu wa Wilaya ya Kilosa kushindwa kulima kwa tija ilhali wilaya yetu imebarikiwa sana kwa kuwa na ardhi nzuri ya kilimo na ni moja ya wilaya bora kabisa hapa nchini kwetu kwenye sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, tunaiomba sana Serikali ili wakulima wetu waweze kulima kilimo bora na cha kisasa, ihakikishe upatikanaji wa pembejeo, usambazaji wa pembejeo na matumizi yake. Pembejeo zinazohitajika sana kwa wakulima wetu wa Wilaya ya Kilosa ni mbegu bora, mbolea na madawa, ahsante sana.