Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba hii muhimu katika maendeleo ya uchumi wa taifa letu. Ninaipongeza Wizara iliyoongozwa na Mheshimiwa Waziri Japhet Hasunga, Naibu Waziri Mheshimiwa Omary Mgumba, Naibu Waziri Mheshimiwa Innocent Bashungwa na Katibu Mkuu wa Wizara na watendaji wa Wizara kwa hotuba nzuri ya kimkakati ambayo itaenda kutatua changamoto nyingi zilizoko katika Wizara hii. Ni matumaini yangu kuwa, timu hii itaibadilisha kabisa tija ya sekta hii nchini.

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa mazao ya kimkakati, yaani kahawa, pareto, pamba, tumbaku, alizeti, parachichi, mbaazi, kunde, choroko, dengu, soya, kwenye mazao mchanganyiko Mkoa wa Songwe unazalisha kwa wingi kahawa tena ya arabika, pareto, cocoa, mpunga, parachichi, soya, mahindi, maharage, viungo na mboga. Fursa za kuendeleza mazao haya, hususan pareto, kahawa, cocoa, viungo na alizeti ni kubwa sana. Wakulima wamehamasishwa sana na wameitikia wito na wanazalisha kwa wingi hasa katika Wilaya ya Ileje.

Mheshimiwa Spika, iko haja ya Serikali kuwa na mkakati wa kuzingatia hatua zote za mnyororo mzima wa thamani katika kila zao muhimu na la mkakati, liwe la chakula au la biashara. Hii ni pamoja na uzalishaji, usafirishaji na uhifadhi. Soko linahitaji aina ya bidhaa, kiasi na ubora na kwa hivyo iko haja ya kuwekeza katika kukuza uzalishaji mkubwa. Uzalishaji mkubwa unahitaji teknolojia na matumizi bora ya pembejeo, mbegu bora, miche, mbolea, dawa, pamoja na kuimarisha shughuli za ugani, ili kulinda ubora na wingi wa uzalishaji mazao husika.

Mheshimiwa Spika, katika suala zima la ugani kuna changamoto kubwa ya upotevu mkubwa wa mazao wakati wa kuvuna na wakati wa kuhifadhi. Upotevu huu wa mavuno unatokana na changamoto ya uhifadhi, maghala, kwamba hayatoshelezi na kwa hivyo hata ile dhana ya kutumia mfumo wa stakabadhi ghalani unashindikana, na kwa hivyo, kumfanya mkulima kukosa bei nzuri na huduma muhimu za kumlinda dhidi ya hasara na umasikini wa kipato.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya yangu ya Ileje mazao yanayozalishwa ni pamoja na kahawa ya arabika, pareto, alizeti na kwa kiasi kidogo cocoa na korosho ambayo imeanza kulimwa. Eneo linalolimwa kahawa limeongezeka kutoka hekta 5,859 hadi hekta 6,229 ambapo jumla ya kata 10 zinajihusisha na kilimo cha kahawa. Uzalishaji kwa Ileje upo kati ya tani 550 hadi tani 800 kwa mwaka. Mwaka 2017/2018 tulipata tani 707.9, mwaka 2018/2019 tumeweza kupata tani 549.9. Kushuka huku kumesababishwa na hali ya hewa iliyoathiri kipindi cha kuchuma maua. Ileje na Mbozi ni wilaya mbili zinazozalisha kahawa ya arabika, kahawa hii inafanya vizuri kwa sababu, ya hali nzuri ya hewa, rutuba na mvua ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, masoko ya kahawa bado ni changamoto japo bado mahitaji ya kahawa ni makubwa katika masoko ya nje kama Japan wanaonunua gourmet coffee kwa bei kubwa sana kwa sababu ni kahawa inayozalishwa bila kutumia kemikali (organic), Ulaya, Canada, India, China na kadhalika. Masoko haya yanatupa fursa ya kuona umuhimu wa zao hili, ili kuwekeza zaidi kuhakikisha tunaingiza fedha nyingi ya nje kujenga ajira za wananchi wengi zaidi.

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali katika kurekebisha mfumo wa vyama vya ushirika; hii imesaidia sana, lakini bado elimu ya kutosha inahitajika kwa wananchi kuielewa hii dhana, hasa baada ya historia mbaya iliyojengeka huko nyuma.

Mheshimiwa Spika, tunaishauri Serikali iendelee kufanyia kazi suala la masoko. Kilimo hai kiendelezwe kwenye kahawa, hii itasaidia wakulima kupata bei nzuri. Serikali itueleze itaweka mkakati gani wa kuendeleza hili. Ugani kwenye kilimo cha kahawa unahitajika sana ili kuwawezesha wakulima kuongeza tija.

Mheshimiwa Spika, zao la pareto ni miongoni mwa mazao ya kipaumbele kwa Wilaya ya Ileje na ndani ya Mkoa wa Songwe. Zao linalimwa katika hekta nne vijiji 12 wakulima 3,500. Wakulima wanahitaji elimu zaidi, miche bora na utaalamu kuzingatia ubora wa zao wakipeleka sokoni, ili wapate bei nzuri. Serikali isaidie katika kuwasaidia wakulima kutengeneza makaushio bora na yanayozingatia utunzaji wa mazingira. Jumla ya tani 397 za mauwa ya pareto zilikusanywa mwaka hadi Aprili, 2019.

Mheshimiwa Spika, tunashauri Serikali ifanyie kazi changamoto zinazolikabili zao hili. Suala la masoko liendelee kufanyiwa kazi ili kupata masoko ya bei nzuri kwa wakulima. Kuboresha miundombinu ya hifadhi ya mazao (maghala).

Vyama vya ushirika kuwezeshwa kiuchumi/mitaji, ili kuwawezesha wanachama wao kuendesha shughuli za maandalizi ya zao hili.

Mheshimiwa Spika, parachichi ni zao linaloongezeka kwa umuhimu katika Wilaya yetu. Hili pamoja na pareto na hata kahawa bado vinaingiliwa sana na walanguzi, hasa kutoka Kenya. Je, Serikali inafanya nini kuzuia hili jambo ambalo linawanyonya wakulima na kuwanufaisha wakenya?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.