Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. JUSTIN J MONKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami ya kuchangia katika hotuba ya Bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. Natambua kabisa kilimo kwa nchi yetu ya Tanzania ni sehemu muhimu sana kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge wengine waliotangulia ndiyo inayoajiri zaidi ya wananchi asilimia 65 na kuhakikisha kwamba inaleta chakula kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukijaribu kupitia katika Bajeti hii ya Kilimo ni ukweli usiopingika kwamba fedha zilizotengwa kwenye Bajeti ya kilimo ni ndogo sana, ni chache sana. Tunajua liko tatizo la Kibajeti na maeneo mengi ni ya kipaumbele, lakini tuiombe Serikali sana ifanye maamuzi ya makusudi kuongeza fedha katika Bajeti hii ya Kilimo. Kwa utaratibu huu tunaokwenda, hizi bilioni mbili, bilioni mia mbili na hamsini na tatu, kwenye Sekta hii yote ya Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika hazitoshi kututoa hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunazungumzia wananchi zaidi ya asilimia 65 na ukiangalia kwenye fedha za maendeleo, huko tena ndiyo kumekuwa hakufai zaidi, kwa sababu fedha nyingi ambazo zimetengwa kwenye upande wa maendeleo zinatoka kwa wafadhili, tunategemea wafadhili kwa zaidi ya asilimia 38, ukienda kwenye umwagiliaji zaidi ya asilimia 91 ya fedha zilizopangwa kwenye umwagiliaji zinatoka kwa wafadhili wa nje, siyo mapato yetu ya ndani, wakati sisi, kwenye Sekta yenyewe ya Kilimo inazalisha kwa zaidi ya asilimia 28 ya pato la Taifa. Kwa hiyo, naiomba sana, Serikali kwa utaratibu huu tunaokwenda nao kwa kutumia fedha za nje, tunaweza tukapata fedha kwa wakati ambao siyo muafaka na matokeo yake kilimo chetu kikaendelea kudidimia na Wizara hii isifanye vizuri.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kwenye upande wa umwagiliaji, kwa kweli Sekta ya Umwagiliaji imetengewa fedha kidogo sana shilingi bilioni thelathini na saba. Ni fedha kidogo sana ukiangalia na bilioni ishirini na tisa ndiyo zinapelekwa kwenye upande wa maendeleo. Nimejaribu kuangalia hakuna mradi wowote katika Mkoa wa Singida, ambao upo kwenye umwagiliaji, iko miradi michache sana ambayo itatekelezwa kwa fedha hizi kidogo ambazo zipo. Sasa, sisi tunataka kuongeza uzalishaji, wakati huo huo, tunahangaika sana na kujaribu kuona namna ambavyo tunaweza tukahifadhi mazao mengine. Nadhani tungewekeza kwenye Kilimo cha Umwagiliaji na tukawa tunalima mwaka mzima, hata tusingetumia nguvu kubwa sana katika kuhifadhi mazao ambayo tutayahitaji wakati ambao wananchi wanatafuta chakula wakati ambao kimehifadhiwa kwenye maghala, ambao wakati mwingine yako mbali sana na maeneo waliyoko wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka niombe, Serikali ifanye juhudi ya makusudi, wamesema Waheshimiwa Wabunge wenzangu, kwenye upande wa umwagiliaji zipatikane fedha angalau zaidi ya bilioni mia tano ambazo zinaweza zikaenda kwenye maeneo mengi ya kuhuisha pamoja na kujenga miundombinu. Kule katika Jimbo langu, yako mabwawa mengi, liko Bwawa la Suke, liko Bwawa la Mgori, liko Masoghweda, liko Kisisi, liko Ntambuko, yako ni maeneo mengi ambayo yanafaa kwa kilimo cha umwagiliaji hata na miradi ya maji. Hata hivyo, hatujaona kwamba tumechukua hatua za makusudi za kutumia maji haya ambayo tayari Mungu ameshatupa bure ili kuweza ku- develop kilimo cha umwagiliaji na kuongeza uzalishaji wetu kupitia huku.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni upande wa masoko; naipongeza na kuishukuru sana Wizara kwa kuweka Kitengo cha Masoko katika Wizara hii ya Kilimo. Kwa sababu tumekuwa tukitegemea sana Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, ambao wakati mwingine hawajui hata ubora wa bidhaa ambazo Wizara ya Kilimo...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JUSTIN J MONKO: Mheshimiwa Spika, nakushuru sana na naunga mkono hoja, lakini waangalie sana suala la umwagiliaji. Ahsante sana. (Makofi)