Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika wangu katika mambo ambayo utakumbukwa kuyafanya kwenye Bunge hili ni pamoja nakutengeneza Kamati ya iliyochunguza fujo zilizotokana na gesi kule kusini. Kamati iliyochunguza madini ya Tanzanite na kamati iliyochunguza madini ya Almasi.

Mheshimiwa Spika, nimetazama picha Mheshimiwa Rais akiwa ameshika paji la uso anaonyesha kutafakari sana. Picha ile inaonesha amezeeka kuliko alivyoapishwa. Inaonekana Mheshimiwa Rais ana mawazo mengi. Sasa kutokana na hiyo hilo nililosema kwanza na hili la Mheshimiwa Rais naomba niseme yafuatayo.

Mheshimiwa Spika, kazi ya Bunge hili kuishauri Serikali, kazi ya Bunge hili ni kuisimamia Serikali. Tunafanya makosa makubwa sana kufanya siasa ndani ya Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, naomba pia niseme nimekuwa msafirishaji wa korosho kwa miaka mingi. Maana Wabunge hapa hawajaambiwa waeleze vitu wanvyofanya. Wapo watu wanasimama hapa wanatetea mambo mabaya yanayofanyika kwa sababu tu wanalima korosho. Mimi nimesafirisha korosho, na kutokana na hilo nataka niwambie, karosho inaoza kama vitungu. Korosho iliyooza maji maji yake yakigusa korosho nyingine inaoza.

Mheshimiwa Spika, nimetangulia kukusifu kwa kutengeneza hizi kamati kwa sababu nataka nikuombe; kama kuna ubishi ndani ya Bunge hili kwamba korosho zimeoza au hazijaoza tengeneza kamati ya watu wachache waeendee wakakague kwenye maghala. Nataka nikwambie korosho imeoza kwa asilimia 30, na hakuna ubishi. Narudia; kama kuna ubishi, Mheshimiwa Spika wetu, Mheshimiwa Spika wangu, sisi ndio tunaosimamia Serikali tengeneza watu waende wakaone wakuletee taarifa. Kwa sababu tukizubaa zikiendelea kuoza hata hizo zilizopo tutapata hasara kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Gazeti la Nation la Kenya la tarehe 12 Mei lilikuwa na kichwa cha habari kinachosema President Magufuli aingizwa chaka na lilikuwa tunazingumza juu ya hii kampuni ya Indo Power kwamba hii kampuni ni ya kitapeli sasa tunazungumza kampuni ambayo ilisimama kama middlemen ikaja ikaidanganya nchi, ikaidanganya Serikali yote kwamba ina uwezo; na Serikali yetu, ya nchi yetu ikaingia mikataba na kampuni ambayo kumbe haina uwezo ilikuwa inaenda kutafuta kampuni nyingine.

Mheshimiwa Spika, ulikuwepo wakati wa sakata la Richmond na Mheshimiwa Mwakyembe ndiye alikuwa Mwenyekiti katika kuchunguza sakata lile. Kampuni ya Richmond haikuzalisha umeme; ilionekana kwamba haina uwezo, viongozi waliwajibika hapa. Kampuni ya Indo Power imekuja kutudanganya hapa, tumeingia hasara, hapo ndipo inaingia hoja ya Mheshimiwa Mnyika. Hakuna sababu ya taarifa, hakuna sababu ya miongozo; sisi kama Wabunge tuna wajibu wa kuangalia ni wapi tulipokosea.

Mheshimiwa Spika, sakata la korosho litadumu kizazi hata kizazi kwa sababu maghala sasa yamejaa, msimu unakuja, hakuna maghala ya kuweka korosho, wakulima wanadai, kwa hiyo kutakuwa na hasara mfululizo katika jambo hili, na hii inaenda kuwa kashfa kama za EPA, ESCROW na Richmond. Ndiyo maana sisi tunasema, kwa unyenyekevu wote, suala hili la korosho kama tulijikwaa, kama tuliteleza tusiendee kuvutana bila sababu ya msingi taifa likaendelea kupata hasara na wananchi wakaendelea kupata hasara; kwa sababu ukweli wa tatizo upo. Ndiyo maana naungana na wanaosema Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali kama Mheshimiwa Spika utaona haifai uchague watu wachache wakaangalie basi Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali aende akachunguze ili aje aliambie Bunge fedha zilizopelekwa kwenye utaratibu huo ni kiasi fulani zimetumika hivi watu fulani hawakutumia vizuri fedha zilitoka wapi na tumepata hasara kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninasikitika sana kuwa suala ambalo linahusu maslahi ya taifa kulifanyia siasa. Bunge linapotoka kabisa, na Spika una uwezo, na umeshafanya mambo mazuri nayakaleta matokeo mazuri. Hili lipo mikononi mwako tusiache wananchi wetu wakateseka tu na majibu kwa sababu watu tunataka kufanya siasa.

Mheshimiwa Spika, baada yakusema haya ninakuomba sana nizungumze pia habari ya kahawa. Zao la kahawa limefanya mambo mengi mazuri katika nchi hii. Wale mliosoma Sekondari ya Lyamungo ilijengwa na KNCU kwa sababu ya kahawa; wale ambao wanaosoma sasa Chuo cha Ushirikia Moshi na waliosoma Chuo cha Ushirika Moshi kilijengwa na wakulima wa kahawa; kilijengwa kutokana na mapato ya kahawa. Hoteli ya KNCU pale Moshi, Moshi Curing yote kahawa ilifanya kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini zao la kahawa Mkoa wa Kilamanjaro linakufa na linauawa kwa sababu ya ushirika. Ushirika wa KNCU uliingia kwenye kashfa ya namna mbalimbali. Mali za ushirika zilifujwa, mashamba ushirika yalifujwa, wananchi walidhurumiwa na kadhalika na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, lakini yapo matatizo mengine yanayotokana na kwanini zao la korosho linakufa. Bei ni ndogo kwa sababu hatuna masoko ya nje hatuna ya ndani mazuri, na kwa sababu hiyo wakulima wanakata tamaa. Katika Wilaya ya Rombo katika Jimbo langu la Rombo baadhi ya wakulima wamekataa tama. Wanang’oa ile mibuni wanapanda makabichii, nyanya na kadhalika; jambo ambalo si zuri kabisa kwa sababu hata mimi nimesoma kwa kahawa na jua thamani ya kahawa.

Mheshimiwa Spika, mimi ninaiomba Serikali, jinsi ilivyopeleka nguvu kwenye zao la korosho, jinsi inavyopeleka nguvu kwenye zao la pamba iwakumbuke wakulima wa kahawa wa Rombo na wa Mkoa wa Kilimanjaro na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, tuna shida ya Maafisa Ugani; ni wachache na ajira zao zinatoka kwa kusua sua. Wapo wazee wetu ambao wamestaafu wapo kule vijiji ambao wanaweza wakaletwa sasa kwenye mfumo. Wapo vijana ambao wamemaliza shule ambao kwa bahati mbaya hawajaajiriwa bado pia wanaweza wakaletwa kwenye mfumo kwa kujitolea. Wakati mwingine wakulima wale wakiwalipa wao wenyewe; Serikali iangalie namna ya kutengeza progamu ili wawalete hawa watu ili waweze kulisaidi lile zao.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna hoja ya pembejeo kuwa ghali, madawa yako juu na kadhalika na kadhalika. Liangaliwe hilo ili Serikali isaidie pembejeo ziwe naafuu wananchi waweze kununua pembejeo vizuri waweze kuamsha lile zao la kahawa.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya mwisho ni kuhusu umwagiliaji. Tunapoteza maji mengi sana katika nchi hii. Mvua inayonyesha maji…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Malizia Mheshimiwa.

MHE. JOSEPH R. SELASINI: …maji yanapotea. Kwa hiyo nilikuwa naomba Serikali na Wizara ingalie uwezekano wa ku-tap haya maji ya mvua ili yaweze kuwasidia wananchi katika kilimo na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, ninakushuru, ahsante sana, na ninawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kunisikiliza.