Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Napongeza, hotuba ni nzuri ya kimkakati na naamini itaenda kujibu hoja nyingi ambazo zilikuwa zimeleta wasiwasi mkubwa sana katika sekta hii. Bado nasikitika tu kuwa Wizara hii bado inapewa bajeti ndogo ukilinganisha na mahitaji, na hasa ukichukulia kuwa ni sekta ambayo kwa kweli ingetutoa katika umaskini kabisa katika nchi yetu. Mimi ninaamini hivyo na nafikiri hata data zinaonesha kuwa kweli hii Wizara hata ingepata trioni moja tu ingefanya mambo makubwa sana kwa sababu ndio inayoajiri asilimia kubwa sana ya watanzania wakiwemo akina mama na vijana. Vilevile ndiyo inayolisha taifa zima na ingeleta fedha nyingi sana za kigeni ambazo zingetuwezesha sasa kufanya mambo mengine makubwa zaidi ya miundo mbinu na kadhalika, hayo ndio maoni.

Mheshimiwa Spika, lakini sasa hivi nataka kuzungaumzia sana suala zima la kilimo chetu, kwamba kimejikita sana kwenye mvua; na kama tunavyojua mvua huwezi kuitegemea kiasi hicho. Tumekuwa na scheme nyingi sana za umwagiliaji lakini kwa bahati mbaya scheme hizi zote zilikuwa zinasimamiwa kwa kiasi kubwa na fedha za nje, na hata hao wahisani wenyewe kuwa ndio waliokuwa wanaweka wakandarasi kuja kuendesha hizo scheme na nyingi hazikufanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, ningependa kuomba sana Serikali ihakikishe kuwa inaweka fedha ya kutosha katika scheme za umwagiliaji; lakini vilevile waangalie ni kwa jinsi gani wanaweza kuwasaidia wanananchi wakulima wadogo wadogo katika kuanza utaratibu wa kuvuna maji ya mvua. Mvua huwa inanyesha nyingi sana kwa vipindi tofauti nchi kwetu lakini inaishia chini. Kama wananchi wangekuwa wanafundishwa jinsi kuvuna maji ya mvua kwa sehemu zao wenyewe walizopo ingesaidia hata kwa kiasi kikubwa sana kukidhi mahitaji ya maji katika maeneo yao na wengeweza kumwagilia, kufuga na kufanya shughuli zile zingewaletea kipato.

Mheshimiwa Spika, nataka nije kwenye suala zima la mazao ya kimkakati. Kuna mazao makubwa ya kimkakati ambayo yametajwa na katika mkoa wangu wa Songwe na hasa Wilaya ya Ileje; kuna mazao matatu ya kimkakati katika Tanzania lakini Wilaya yangu inayalima kwa wingi ikiwa ni pareto, kahawa, alizeti na bado kuna fursa ya kuzalisha mazao mengi kwa sababu ya hali hewa, udogo uliopo kule na watu wenyewe wanajituma sana katika kufanya kazi. Tatizo letu kubwa ni huduma za ugani. Huduma za ugani ni ndogo, tunahitaji wataalamu wengi sana wa kutuongoza katika kila kijiji.

Mheshimiwa Spika, vilevile suala lingine ni masoko; bado masuala ya masoko hayajakaa vizuri. tunajua Serikali imefanya makubwa sana na kwa kweli wametusaidia kwa kiasi kikubwa sana katika kuonyosha ule mfumo mzima wa soko lakini bado haujakamilika, bado kuna changamoto nyingi, kuna tozo nyingi na bado kuna tatizo la miundombinu ya kuyafikia masoko yale.

Mheshimiwa Spika, tungependa kuona sana Serikali ikihakikisha kuwa katika hata maeneo ambayo yana fursa nzuri za uzalishaji kama Ileje, Mbozi na Mkoa mzima wa songwe basi inaturahisishia miundo mbinu ambayo itawawezesha wananchi kufikisha mazao sokoni.

Mheshimiwa Spika, Vilevile Kuhusu Elimu Pamoja na Pembejeo Bora. Tuna matatizo makubwa ya pembejeo za kuwezesha mazao yetu kuwa na ubora na uzalishaji mwingi. Bado tuna fursa kubwa sana katika soko la dunia kwa kahawa na pareto. Pareto kwa Afrika tunaongoza sisi Tanzania, hiyo ingekuwa fursa kubwa sana kwetu kuhakisha kuwa tunawekeza nguvu zaidi katika zao hili kwa sababu tayari sisi tuna hiyo fursa kitaifa. Kwenye kahawa vilevile kuna masoko maalum ambayo tungeweza kuyalenga kwa mfano masoko ya organic, masoko ambayo yangeweza kuwa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Malizia Mheshimiwa dakika moja.

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Spika, kwa hali hiyo ningependa sana kuona Wizara hii ikijikita kimikakati katika yale maeneo ambayo yana mazao ambayo tayari yana- advatage ya kuzalishwa kwa wingi.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.