Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye mapendekezo haya ya Bajeti ya Kilimo. Bahati mbaya sana ni dakika tano na mambo ni mengi kidogo, lakini niwapongeze Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya, Waziri na Manaibu wake, wanafanya kazi nzuri. Ninaamini kwamba mazonge yaliyopo kwenye Wizara ya Kilimo mengi wameyakuta kwa hiyo pengine hayawahusu sana isipokuwa wanao wajibu sasa wa kurekebisha tunapotokea hapa kwenda mbele pengine wafanye kazi ile ambayo inakusudiwa. Mengi kwa kweli siyo ya kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ambalo ninataka kushauri Sekta hii ya Kilimo inachukua watu wengi sana lakini bahati mbaya sana ukiangalia mtiririko wa utengaji wa fedha ukilinganisha na Makubaliano kwa mfano ya Malabo ya asilimia kumi, sisi bado tuko kwenye average ya asilimia 1.2. Nadhani kama lengo letu ni kupambana na umaskini wa watu wengi kwa wakati mmoja, basi lazima tuongeze bajeti kwenye Wizara ya Kilimo, vinginevyo kasi ya kupambana na umaskini itakuwa shida. Kama tunataka kushughulika na umaskini wa watu wetu lazima tuongeze bajeti maana mtiririko wake kwa kweli ni mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, mwaka jana hapa tulifanya mabadiliko madogo kwenye Sheria ya Korosho. Matokeo ya tulichokifanya watu wote tunajua, haihitaji kwenda shule kujua kwamba hali ya tasnia ya korosho sasa hivi ni mbaya sana, ni almost iko ICU, matatizo ni mengi, mambo ni mengi. Kulikuwa na nia njema ya Serikali, Rais akaweka nia njema, waliokwenda kuitekeleza nia njema ya Rais wamekwenda kugoroga na kuua Sekta ya Korosho.

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyoongea,bahati mbaya zoezi lilikumbwa na dhuluma, lilikumbwa na rushwa, lilikumbwa na ubabaishaji mwingi sana na uongo mwingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyoongea Jimbo la Mtama peke yake kwenye vyama vya msingi 11 wakulima ambao wana korosho chini ya tani 1,500 ambao wamehakikiwa mashamba yao zaidi ya 1,281 kwa miezi nane toka korosho yao ichukuliwe hawajapata senti tano, 1,281, lakini korosho yao imechukuliwa. Msimu umeanza hawana fedha za kutengeneza mashamba yao, hali ni mbaya.

Mheshimiwa Spika, sasa mapendekezo yangu; la kwanza; napendekeza tuilete Sheria ya Korosho hapa Bungeni, yote tuipitie upya ili tuokoe zao la korosho. Kile kipengele tulichokinyofoa kimesumbua sheria nzima, sasa ileteni sheria yote tupitie.

Mheshimiwa Spika, la pili, zoezi hili kwa kuwa lilikumbwa na maneno mengi, mengine ni ya uongo, ninapendekeza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali aende kukagua atuletee ripoti hapa ndani ya namna zoezi lilivyokwenda ili tuchukue hatua ya kuziba mashimo kwenye yale maeneo ambayo yana shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pendekezo la tatu, kama nilivyosema watekelezaji wa nia njema ya Mheshimiwa Rais wengi wamekwenda kukoroga mambo. Sasa ni vizuri waliokoroga wawajibike kwa matendo ya kuvuruga tasnia ya korosho. Na hapo ni vizuri tukawa specific, si sahihi kuingiza Serikali yote kwenye mambo yaliyofanyika hovyo, watu waliofanya hovyo wanajulikana na kama wasipochukua hatua wenyewe… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Nape Nnauye, dakina moja ya kumalizia.

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nasema hivi; waliokoroga kwenye jambo la korosho wachukue hatua wenyewe, wasipofanya tutaleta kusudio la kusema jinsi walivyoshiriki mmojammoja na jinsi ambavyo wanapaswa kuchukua hatua kwa sababu waliyoyafanya ni kuhujumu korosho, wananchi, lakini pia wamehujumu uchumi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tukiulizana korosho yetu iko wapi, korosho haiwezi kukaa zaidi ya miezi sita hapa nchini ikabaki salama. Mkituambia bado mna korosho sahihi, korosho inayoweza kutumika, huu ni uongo, tukiendelea kusema uongo huu na bado hatuoni aibu tunaendelea kubaki, sio sawa. Ndiyo maana wito wangu, leteni sheria tuipitie upya, CAG aende akakague lakini waliotukoroga wawajibike na msipowajibika tutaleta hoja hapa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)