Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba Kigosi Kuwa Hifadhi ya Taifa Kigosi pamoja na Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji wa Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba la Igalla Kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki (Minamata Convention on Mercury)

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba Kigosi Kuwa Hifadhi ya Taifa Kigosi pamoja na Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji wa Hadhi Sehemu ya Eneo la Pori la Akiba la Igalla Kuwa Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla pamoja na Azimio la Bunge la Kuridhia Mkataba wa Minamata kuhusu Zebaki (Minamata Convention on Mercury)

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa fursa hii ya kufafanua maeneo machache ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu na pili niwashukuru wachangiaji wote na kimsingi niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa kiasi kikubwa wameunga mkono hoja ambayo imewekwa mezani kwako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia zaidi niwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wa Kamati kwa ushirikiano mkubwa waliotupa wakati tulipokuwa tukifanyia kazi azimio hili, lakini pia niwapongeze sana na niwashukuru Kambi ya Upinzani Bungeni pia kwa kuunga mkono hoja hii kwa kiasi kikubwa na niwahakikishie tu kwamba mashaka yaliyopo, wasiwasi mdogo uliopo tutaushughulikia kwa uungwana na ustaarabu wa hali ya juu tukizingatia mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge wenzetu ambao wamechangia hapa Bungeni, tunafahamu Mheshimiwa Magdalena Sakaya amezungumzia uwezekano wa uwepo wa watu katika maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie tu kwamba Mheshimiwa Rais anawapenda sana Watanzania, anajali maslahi yao na anayahudumia kwa karibu sana mahitaji ya Watanzania wote ikiwemo hawa Watanzania ambao kipindi ambapo ulinzi ulilega kwenye maeneo haya ya hifadhi walivamia na ndio maana mwezi Januari 15 Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli alitupa maelekezo mimi pamoja na Mawaziri wengine saba tukafanya kazi kubwa sana ya uchambuzi wa maeneo yenye migogoro na maeneo yote haya tuna mapendekezo mahususi ambayo tumeyafikisha kwake na wakati atakapotupa mwongozo namna ya kuyamaliza basi tutarudi kwa Waheshimiwa Wabunge na kwa wananchi kuwapa mrejesho, lakini pia kufanyia kazi maelekezo ambayo tutakuwa tumepewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwamba tuko makini na nia ni njema na migogoro yote iliyopo katika maeneo yanayohifahiwa kwa kweli tutaishughulikia kiuungwana sana na sote ni mashahidi maeneo ya hifadhi kwa sasa yametulia kwa kiasi kikubwa, wananchi wanaishi vizuri na maeneo ya hifadhi na askari wetu, hakuna tena ile pigapiga, kamata kamata haipo tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu pia kufafanua kwamba changamoto ambazo zimetolewa katika eneo la mzigo ambao anabebeshwa TANAPA tunazifahamu na Serikali imekwishaanza kuzifanyia kazi, mwaka huu tulifanya kazi kidogo bahati mbaya haikukamilika kama ambavyo tunatarajia, kwa hiyo tutaendelea kufanya kazi kwa ukaribu na Wizara ya Fedha ili tuweze kuona walau kuna namna ambayo tunaisaidia TANAPA na uhifadhi kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mwisho kabisa nisema tu kwamba baada ya mchakato wa kupandisha/kubadilisha hadhi maeneo haya matatu kwa maana ya Hifadhi ya Taifa ya Nyerere, Hifadhi ya Taifa Mto Ugalla na Hifadhi ya Taifa ya Kigosi Tanzania itafikisha Hifadhi za Taifa 22. Pia tukichanganya na marine parks mbili ile ya Mafia Ruvuma Estoary Marine Park pamoja na ile ya Mafia kule tukichanganya na hii ya Mnazibay tutakuwa nazo jumla parks zipatazo 24 na hivyo Tanzania itakuwa ndio nchi yenye hifadhi nyingi zaidi hapa Barani Afrika. Kwa sasa kuna nchi ya Kenya ambayo ina hifadhi 23 ukichanganya hifadhi za nchi kavu na hifadhi za kwenye maji, lakini Tanzania tulikuwa nazo hizo 16, baada ya kupandisha na kubadilisha hadhi maeneo yote haya sasa Tanzania tutakuwa tuna hifadhi 24. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwambe anauliza hizi zina maana gani? Maana yake kubwa ni kwamba hii itakuwa ni selling point ya muhimu sana kwamba sisi ni nchi yenye hifadhi nyingi, kwa hiyo, kiuhifadhi itatupa credit, lakini pia kibiashara itatupa credit kwa sababu ni selling point kwenye marketing kuna punch line. Kwa hiyo, tukisema kwamba sisi tuna nyingi zaidi kuliko wengine tunaonekana sisi ni vinara na hivyo ni bora zaidi kuliko wengine na hivyo itatusaidia kuuza kirahisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nukta yangu ya mwisho nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa mwongozo ambao amekuwa akiutoa kutuwezezesha kufikia hatua hii. Kwetu sisi wahifadhi hii ni hatua kubwa na nyeti na hizi Hifadhi za Taifa sio tu zitasaidia kupata mapato lakini zinaweka mustabali wa maisha ya watu wetu. Nchi yetu imekuwa degraded kwa kiasi kikubwa, eneo la malisho ya mifugo limeharibika kwa zaidi ya asilimia 31, kiasi cha mvua kimepungua sana na sababu ni hii encroachment ya wananchi kwenye maeneo yaliyohifadhiwa na hii ilikuwa inatishia kuleta njaa miongoni mwa watu wetu ambao sisi Waheshimiwa Wabunge tunawatetea hapa kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hatua hizi anazochukua Mheshimiwa Rais za kumaliza migogoro, lakini pia kubadilisha hadhi baadhi ya maeneo ili kuyahifadhi vizuri zaidi ili kuyapa ulinzi mkubwa zaidi, ili kuweza kuyatumia kibiashara zaidi kwa kweli ni hatua ambazo zitaandika jina la Mheshimiwa Rais Magufuli kwa wino wa dhahabu kwa vizazi na vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na kwa maazimio yote mawili naomba kutoa hoja. (Makofi)