Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Grace Sindato Kiwelu

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. GRACE S. KIWELU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia Wizara hii muhimu sana katika Taifa letu. Nichukue nafasi hii kuwashukuru walimu wangu wote walionisaidia kufika mahali hapa leo, ninawashukuru sana, lakini niwapongeze walimu wote nchini kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na mazingira magumu waliyonayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, urithi pekee tunaoweza kuutoa kwa watoto wetu ni elimu, na kwa maana hiyo ni lazima elimu hiyo iwe bora na isiwe bora elimu. Na ili elimu hiyo iwe bora ni lazima tuhakikishe tunatatua matatizo ya walimu, wamesema Waheshimiwa Wabunge hapa, matatizo waliyonayo walimu wetu, liko tatizo la upandishwaji wa madaraja, tatizo hili limekuwa ni tatizo sugu, walimu wetu kila mwaka Wabunge wakija hapa wanalisemea hilo lakini bado tatizo hili linaendelea kuwepo.
Nikuombe dada yangu Mheshimiwa Waziri wa Elimu, ninamba tuangalie walimu hao, lakini wanadai kwamba pamoja na hao wanaobahatika kupandishwa hawaangalii umri wa mtu kuuingia kazini, anaweza akaingia wa mwaka huu akampita daraja aliyefanyakazi zaidi ya miaka kumi, sasa yapo malalamiko hayo ninaomba myatazame.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwingine ni tatizo la ucheleweshwaji wa mishahara. Walimu hawa kwanza nimesema wanakaa kwenye mazingira magumu, mazingira hayo yanawasababishia kushindwa hata kuzihudumia famila zao. Mshahara mnawacheleweshea, walimu wanaokaa mbali na miji wanafunga safari kufuata mishahara, wanatumia muda mirefu kufuatilia mishahara yao na watoto wetu wanakosa vipindi. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, akikisheni mishahara ya walimu hawa inafika kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine Mheshimiwa Waziri ni unyanyaswaji wa walimu. Wamesema wenzangu hapa, walimu wanapigwa makofi na Maafisa Elimu, wananyanyasika sana walimu hawa. Lakini lingine wako walimu wanaoonekana kuwa upande wa pili wakionekana na upinzani wanaandikiwa barua za onyo, lakini wale wanokuwa upande wa wapinzani wetu wao wanaonekana wanafanya sahihi. (Makofi)
Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri, angalieni masuala haya tusiwagawe watanzania kwa itikadi za kisiasa, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ni suala la nyumba. Suala la nyumba maeneo mengi bado ni tatizo hasa wale wanaokwenda maeneo yenye mazingira magumu amesema mchangiaji aliyemaliza hakuna hata nyumba za kupangisha. Na hili ni tatizo kubwa sana hasa kwa watoto wetu wa kike, unajikuta wanapewa nyumba na Wenyeviti wa Vijiji mwisho wanakuwa wake zao. (Makofi)
Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri hakikisheni suala la nyumba kwa walimu wetu mnalifanyia kazi haraka ili waweze kupata hizo nyumba za kuishi na hao wanaokaa mbali tuwape basi transport allowance, wanakaa mbali sana na maeneo ya vituo vyao vya kazi. Lakini na posho ya pango, watumishi wa Wizara nyingine wanapata, kwa nini walimu? Walimu wametufikisha hapa ndugu zangu tuwekeze kwa walimu kama kweli tunataka kuboresha elimu ya Taifa letu. Tutafanya mengine yote lakini tusipowekeza kwa walimu wetu kuhakikisha wanapata maisha mazuri, fedha zao wanapata kwa wakati itakuwa ni kazi bure.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala la elimu bure. Waraka Namba 6 ulieleza yake mambo mliyoyaeleza pale, lakini niseme kwa kifupi, wamesema pia wenzangu, wakuu wa shule mnawapa wakati mgumu sana, ile fedha ya OC mnayotuma kwanza ni fedha kidogo, haitoshelezi, leo shule nyingi zina madeni ya umeme, maji, walinzi wanadai, leo tumechongesha madawati tumesaidiwa na TANAPA, tuna vifaa ambavyo vinahitaji vilindwe na walinzi. Leo walinzi hawajalipwa mishahara wanaondoka kwenye mashule yetu, viti vikiibiwa tutakuwa wageni wa nani.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia shule nyinge wamekatiwa maji, Mheshimiwa Waziri wewe ni Mwanamke wamesema Wabunge wenzangu mtoto wa kike bila maji hawezi kusoma. Leo shule zimekatiwa maji, watoto hawa wa kike tunawasaidiaje, watakimbia shule mwisho mnakwenda kuwakamata wazazi wao kuwaweka ndani, lakini Serikali ya Chama cha Mapinduzi mmeshindwa kutimiza wajibu wenu kwenye hizi shule. Hakikisheni mnapeleka fedha za kutosha, leo chakula kipatikane mashuleni hasa yale maeneo yenye mazingira magumu. Watoto hawaendi shule kwa sababu hakuna chakula na hata wanakwenda wanasinzia madarasani, walimu wanashindwa kufundisha kwa sababu watoto wetu wana njaa. Wazazi wameshindwa kuchangia kwa sababu hawana kipato cha kuchangia.
Mheshimiwa Naibu Spika, wengi walipelekwa shule kwa sababu walijua chakula kinapatikana hasa yale maeneo ya wafugaji, leo chakula hakuna watoto wemeondoka mashuleni, lakini hata wale wanao-supply chakula kwenye mashule yetu hawajalipwa mpaka leo wanadai na wengi wao wamechukua mikopo kwenye mabenki, leo tunataka kuwatafutia vifo watu hawa kwa sababu mabenki yatakwenda kutaifisha mali zao. Niombe sana Mheshimiwa Waziri hakikisheni suala hili mnalifanyia kazi, walipeni wazabuni ili waweze kutimiza wajibu wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nisemehe shule zenye mahitaji maalum. Kwa hapa nimshukuru sana Waziri wa TAMISEMI nililisema hili kwenye Wizara yake na tuliwasiliana, niwaombeni sana shule hizi zina mahitaji mengi muhimu. Tunawahitaji watoto wetu hawa wenye ulemavu, tunajua wanao uwezo lakini miundombinu ya shule hizo bado ni tatizo, ukiingia kwenye vyoo ni tatizo, vifaa vya kujisomea bado ni tatizo. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri fuatilieni watoto hawa wenye ulemavu, wanaouwezo wa kuwa viongozi katika Taifa hili. Ni jana tu nimetoka kutuma dawa katika ile shule ya watoto wenye ulemavu Njia Panda, hawana hata fedha za dawa, kwa hiyo niombe sana akikisheni shule hizi mnaziangalia kwa jicho la kipekee.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ni suala la Ujenzi wa maabara. Tatizo la Serikali hii badala ya kuanza jambo la kwanza tunaanza la mwisho kwenda la kwanza. Maabara hizi zilijengwa, wananchi walipata wakati mgumu sana, walinyang‟anywa mbuzi, walinyang‟anywa kuku, maabara hizi zimekamilika leo, hakuna walimu, hakuna vifaa, tuwaeleweje Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Ninaomba sana na kwenye hotuba yako umesema vifaa vitaanza kununuliwa 2018 kama sikosei, sasa ni kwa nini tusingeanza kuandaa walimu, tukaviandaa vifaa alafu tukajenga hizo maabara. Leo watoto wetu wanakosa walimu, wanasayansi tutawapata wapi, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri ulifanyie kazi suala hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ni ombi kutoka kwa mdogo wangu hapa ameniomba, wana Chuo cha Maendeleo ya Jamii kule Tarime, anaomba sana chuo kile mkibadilishe kiwe chuo cha VETA. Kwa sababu kama tumeshindwa kuvijenga bora tukatumia vyuo hivi au majengo haya yaliyopo kufungua vyuo vya VETA ili watoto wetu hawa wakaendelee kupata elimu hii ya ufundi kupitia vyuo hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ni suala la polisi Wilaya ya Siha walisimamia mtihani wa kidato cha nne mwaka jana. Lakini mpaka leo hawajalipwa fedha zao. Nikuuombe sana Mheshimiwa Waziri na ni Wizara yako ilitakiwa iwalipe, tunaomba mkawalipe polisi wale fedha zao na ukizingatia nao bado wako kwenye mazingira magumu fedha zao hawazipatai kwa wakati, kazi hii walishaifanya, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri mkalifanyie kazi suala hili ili polisi hao waweze kupata fedha zao.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunao upungufu mkubwa sana wa walimu wa Sayansi katika Wilaya yetu ya Siha. Ninaomba sana tuhakikishe tunawekeza kwa walimu hawa, kuna hiyo taarifa tuliyoipata ya mgomo wa UDOM. Walimu hawa hawafundishwi, zaidi ya wiki mbili sasa, walimu hawa wangetusaidia kuziba hilo pengo la walimu wa sayansi. Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri fanyia kazi suala hili watoto wetu warudi darasani wakafundishwe ili wakafundishe watoto wetu. Nakushukuru sana.