Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere

Hon. Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. awali ya yote nianze kwa kukupongeza wewe na mfumo mzima wa taasisi yetu ya Mhilimi wa Bunge kwa kukubali hoja hii iingie hapa Bungeni siku ya leo lakini pia zaidi kwa kutoa ushauri, mchango na mapendekezo mbalimbali ambayo yanalenga katika kuboresha utekelezaji wa majukumu ya usimamizi ambayo Serikali imepewa na Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, pili; nimpongeze Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa uamuzi wake wa kuamua kubadili matumizi ya sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selou kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere. Na niwashukuru Waheshimiwa Mawaziri wenzangu wote pamoja na Serikali kwa ujumla, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ushauri na mwongozo katika kutekeleza agizo la Mheshimiwa Rais la kuleta hoja hii hapa Bungeni siku ya leo.

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo naomba pia niwashukuru watendaji wote wa Wizara yetu wakiongozwa na Katibu Mkuu Prof. Adolf Mkenda kwa kuendelea kutupa ushauri wa kiufundi ambao umetuwezesha kufikia hatua hii.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nitoe ufafanuzi kwenye maeneo machache ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa wabunge lakini pia niwaahidi kwamba kwa yale ambayo sintoweza kuyagusa, hususan yaliyoletwa kwa maandishi na hata mengine ambayo yamechangiwa kwa kusema hapa Bungeni, basi tutayazingatia katika kutekeleza maagizo haya baada ya azimio hili kufanikiwa kupitishwa na Bunge.

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo naona kubwa na limejitokeza sana ni suala la kwa nini eneo lote la square kilometer 50,000 za Pori la Akiba la Selous lisigeuzwe kuwa eneo la uhifadhi maalum la Nyerere. Niliona alitoa taarifa hapa Mheshimiwa mchangiaji mmoja kwamba pengine huu mfumo ulivyo kwa sisi kupandisha hadhi sehemu tu ya ikolojia nzima una maana yake. Japokuwa pia hata kama tungetaka kuutazama mfumo huo wa conservation area tukaunganisha na maeneo mengine pia ingeweza kufaa tu. Lakini kwa sasa tunaona mapendekezo haya ambayo yanatokana na maelekezo ya Mheshimiwa Rais inafaa zaidi kwa hivyo ambavyo tumeyaleta na tunaomba Waheshimiwa Wabunge wapitishe mapendekezo haya kama yalivyo kwa sababu zifuatazo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza; ni ukweli kwamba Hifadhi za Taifa kwa mfumo wa ikolojia ambao upo katika nchi yetu, huwa zinakuwa zimefichwa na maeneo yenye hadhi nyingine za uhifadhi katika mzingo wake. Kwa maana ya kwamba kama kuna Hifadhi ya Taifa katikati kwenye kiini ambayo inatengeneza kiini cha ikolojia hiyo basi pembezoni mwake kunakuwa aidha na mapori ya akiba, mapori tengefu, misitu ya hifadhi ama maeneo ya jumuiya za uhifadhi za wananchi. Na haya maeneo mengine yanafanya kama vile buffer ya hiki kiini ambacho kinakuwa ni Hifadhi ya Taifa. Na huu ndio muundo ambao utaupata katika ikolojia zote.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, hata ikolojia maarufu zaidi hapa nchini na duniani kote kwa ujumla wake ikolojia ya Serengeti kuna mapori ya akiba kama ya Ikolongo, Gurumeti, Pori la Akiba la Maswa, Poli Tengefu la Loliondo, kuna eneo la Hifadhi ya Ngorongoro; yote haya yanaizunguka ikolojia pia Lake Natroni kwa kule juu yote haya yanaizunguka Hifadhi ya Taifa ya Serengeti. Kwa hivyo, kunakuwa kuna maeneo mengi ambayo yapo katika hadhi tofauti tofauti za uhifadhi ambapo katikati yake ndio kunakuwa kuna Hifadhi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, na muundo huu haupo kwa bahati mbaya, muundo huu unatuwezesha kuwa na uhakika wa kuwa na hifadhi ya Taifa katika kiini lakini pia unasaidia matumizi mengine kufanyika katika maeneo ambayo yana hadhi nyingine tofauti, kwa mfano kama ni kwenye mapori ya akiba na mapori tengefu na kama kuna wanyamapori basi inaruhusiwa kuwinda wale wanyama lakini pia kama ni maeneo ya misitu basi hapo itaruhusiwa kuvuna ile misitu ili iweze kutumika.

Mheshimiwa Spika, hii ni kwa sababu malengo ya nchi yetu sio kuwa na maeneo ya hifadhi na kuwa nayo tu, malengo ya nchi yetu ni kuwa na maeneo ya hifadhi lakini pia kuyafanya maeneo haya yatusaidie katika kupambana na umasikini. Yatupe kipato ambacho kitatusaidia kutekeleza miradi mingine. Kwa hivyo, tunaangalia siku zote tunafanya trade off kwamba eneo hili tutafaidika zaidi tukifanya nini, tukifanya utalii wa picha ama tukifanya utalii wa picha na uwindaji ama tukivuna miti. Kwa hivyo hivyo ni vigezo katika vigezo ambavyo vinatufanya tuamue eneo gani liwe nini kama Taifa na ni muundo ambao umedumu kwa muda mrefu na haujawahi kutuangusha.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, tunaomba kwa kweli muundo huu tuendelee kuulinda na hata kwenye hii Hifadhi ya Taifa ya Nyerere kuna jumuiya za uhifadhi wa wanyamapori ambazo zipo zinazunguka hifadhi hii; kuna misitu kama alisema Mheshimiwa Mchengerwa na Mheshimiwa Bobali ambapo wanavuna miti wale hawavuni miti Selous, wanavuna miti kwenye misitu ya hifadhi ambayo ipo pembezoni mwa Selous. Kwa hivyo, ni vitu kama hivyo kwamba hii maliasili tunaitumia kwa kuvuna, tunapovuna tunauza tunapata faida kama nchi inatusaidia kuhifadhi maeneo yenyewe lakini pia inatusaidia kutekeleza miradi mbalimbali ya kijamii ikiwemo barabara, shule, afya na vitu vinginevyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, hata pale Selous inapozunguka watu wengi hudhani kwamba miti inavyovunwa pale ama mikaa inayochomwa pale basi imetoka Selous kwa sababu wananchi katika nadharia yao wanadhani eneo lote lile tu kwa sababu tu ni msitu basi lote ni Selous, hapana pembezoni mwa Selous kuna hifadhi za misitu hususan katika eneo hilo la Wilaya ya Liwale lakini pia ukipanda kwa juu zaidi kuna jumuiya ya hifadhi ya wanyamapori, jumuiya ya Gonabis ipo pale kutoka kule Wilaya za Kibiti mpaka kule eneo la Kisarawe. Lakini pia kwa upande wa huku utakuta kuna Hifadhi ya Misitu ya Udzungwa, kuna Kilombero Pori Tengefu la Kilombero ambalo alikuwa analizungumzia Mheshimiwa Suzan Kiwanga.

Mheshimiwa Spika, na hapa labda niseme kidogo kwa sababu amelizungumza kwa kirefu kwamba wale Sheshe wanapaswa kuwa katika Pori Tengefu la Kilombero na kwa sasa katika ramani mpya ya kutengeneza hii ikolojia ya huku kusini upya, tumeamua kupandisha hadhi Pori Tengefu la Kilombero ili sasa liende likawe Pori la Akiba la Kilombero yaani iwe Kilombero Game Reserve. Na sababu kubwa ni pamoja na kuhifadhi hao Sheshe. Walikuwa zaidi ya 40,000 mwaka 1990 leo hii wamebaki 4,000 tu na hao Kampuni ya Kilombero North Safaris wanasaidia sana katika kutoa ulinzi kwa hao Sheshe ambao wamesalia.

Mheshimiwa Spika, pia Kilombero ilikuwa mashuhuri kwa makundi makubwa ya Nyati na Tembo ambayo sasa hivi huyaoni tena. Kwa hivyo, tumekusudia kwa kweli kwa dhati kuimarisha ulinzi katika eneo hili. Pia naomba ifahamike kwamba Milima ya Udzungwa, Milima ya Mahenge na Milima ya Mbalika kwa ujumla wake ndiyo inatusaidia kupata Bonde la Kilombero ambalo linafanya kazi kama chujio la kupeleka maji katika Mito hiyo ya Luwegu pamoja na Mto Kilombero kutengeneza Mto Ulanga ambao unaenda kutengeneza hilo Bonde la Stiegler ambalo tunakusudia kuzalisha umeme takribani megawati 2115.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, uhifadhi wa eneo hili upstream huku Kilombero ni muhimu sana na kwa maana hiyo tumeamua kupandisha hadhi eneo hili lakini pia Milima ya Mahenge na misitu yake, Milima ya Mbalika na misitu yake na maeneo ya jirani ambayo bado hayana watu tunayapandisha hadhi kuwa Pori la Akiba la Kilombero. Pia tunatoa sehemu kubwa kutoka 6,500 square kilometer mpaka kubakisha 2,500 za kiini cha bonde kurudisha kwa wananchi kwa ajili ya kupunguza presha ili waweze kuishi kihalali na waweze kufanya shughuli zao za kilimo na ufugaji katika eneo ambalo sasa litakuwa halali kuliko ilivyo hivi sasa ambapo wanahesabika kama wavamizi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, tumeangalia sana suala hilo kwa ujumla wake na haswa kwa faida hizo kubwa za kiuhifadhi lakini pia faida pana zaidi za kitaifa za kuzalisha umeme katika Bonde la Mto Rufiji.

Mheshimiwa Spika, pia ilijitokeza kwa kina sana hoja ya TANAPA kubebeshwa mzigo. Na sisi tunaona lakini tofauti ya maeneo yanayohifadhiwa na kusimamiwa na TANAPA na yale yanayohifadhiwa na kusimamiwa na TAWA kwa kweli ni matumizi tu, umuhimu wa maeneo haya ni uleule bioanuai iliyopo kwenye maeneo haya ni ileile na pengine wakati mwingine mapori ya akiba yanaweza yakawa yana bioanuwai nzuri na nyeti zaidi kuliko hata Hifadhi za Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, hii lugha ya kwamba tunapandisha hadhi ni lugha tu rahisi lakini kimsingi hatupandishi hadhi, tunachokifanya tunabadilisha matumizi ya eneo kwamba eneo hili matumizi yanaruhusiwa, eneo hili matumizi ya resource iliyopo pale hayaruhusiwi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, maeneo haya ni muhimu sana na kwa takwimu za haraka haraka TAWA ambayo kwanza ni taasisi changa sana inasimamia takribani maeneo yenye ukubwa wa kilomita za mraba 250,000 wakati TANAPA inasimamia eneo lenye ukubwa wa kilomita za mraba 60,000 baada ya kuongeza na hizi hifadhi mpya tatu.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, ukiangalia pia bajeti ya TANAPA per square meter ni kubwa sana, ni zaidi ya asilimia 157 katika standard ambazo zimewekwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhifadhi wa Bioanuai (ICUN) wakati TAWA wapo kwenye asilimia 83, kwa hivyo bado hawajafikia hata ile asilimia 100 ya per square meter ya eneo ambalo wanapaswa kusimamia. Ngorongoro wameshafika zaidi ya per square meter kwa asilimia 600 zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, ukipiga hesabu hizo unaona kabisa kwamba kwa kweli mgawanyo wa resources ambazo zinapatikana per square meter ya eneo ambalo linahifadhiwa bado unaipa disadvantage kubwa sana taasisi hii ambayo bado ni changa pia ya TAWA.

Mheshimiwa Spika, hivyo, katika uelekeo wetu wa mbele, tunaona kwamba ili kuondoa hii fragmentation ya mgawanyo mbovu wa rasilimali katika taasisi ambazo zinafanya kazi ileile ambayo ina umuhimu uleule, tunakusudia ndani ya Serikali bado tunaendelea na mchakato wa ndani kufanya kidogo amalgamation ambayo tutamtenga TANAPA atabaki peke yake na tutamchukua TAWA tutamuunganisha na Ngorongoro kutengeneza taasisi moja yenye nguvu lakini pia itakuwa ina nguvu ya rasilimali ili iweze kusaidia ku-balance kidogo uwiano per square meter wa uhifadhi kwa maana ya kipimo cha rasilimali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, tunafikiria kufanya hivyo, hatukusudii kuunganisha zote kwa pamoja, tunaona pia itatuletea changamoto lakini kwa sasa tunakusudia walau kuunganisha TAWA na Ngorongoro ili tuweze kugawanya resources ziende zikasaidie zaidi kuimarisha uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, kwamba nani ana mzigo mkubwa zaidi, na kwamba tunamuongeze mzigo TANAPA, mwenye mzigo mkubwa zaidi ni TAWA. Na hata hivyo, kwamba TAWA maeneo yake yanachukuliwa, ni kweli yanachukuliwa lakini pia maeneo ya mapori ya akiba pia yanaongezeka; kwa mfano hapa nimetaja Pori la Akiba la Kilombero linaongezeka na linaongezeka ukubwa pia kwa zaidi ya square kilometer 5,000, sasa hivi lina square kilometer 2,500, hicho kiini ambacho bado kipo hai.

Mheshimiwa Spika, lakini tunapoongeza na hii milima na misitu ambayo ipo hapa jirani katika Pori la Akiba la Kilombero litakuwa na zaidi ya square kilometer 7,500. Kwa hivyo, litakuwa eneo kubwa sana na eneo lote hili linaweza likatumika kwa shughuli za uwindaji na shughuli nyingine za matumizi ya rasilimali.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, tunaongeza pia mapori ya akiba mengine ambayo yapo katika pipeline katika hatua mbalimbali ndani ya Serikali ikiwemo eneo la Wamimbiki, Lake Natron na Wembele tumesema hapa asubuhi kwenye swali. Maeneo yote haya pia tunaongeza kule magharibi eneo la Luganzo Tongwe, tunatengeneza pori la akiba, haya maeneo ni makubwa sana na yataenda kuimarisha shughuli za uwindaji wa kitalii ambao unasimamiwa na Taasisi ya TAWA na kama tutafanikiwa kupitisha mapendekezo yetu kama yatakuja hapa Bungeni basi tutakuwa na hiyo taasisi moja mpya ambayo itasimamia maeneo yote ya hifadhi za wanyamapori nje ya maeneo ya Hifadhi za Taifa.

Mheshimiwa Spika, swali lingine ambalo limejitokeza sana ni eneo la Mradi wa REGROW, Mheshimiwa Naibu Waziri amefafanua hapa kiasi fulani. Nilipenda tu kuongeza kwamba Mradi wa REGROW ambao unalenga kukuza utalii kanda ya kusini, ni mradi wa kuhifadhi lakini pia kukuza shughuli za utalii. Kwa hivyo, tunachokifanya katika Pori la Akiba la Selous kubadilisha matumizi ya sehemu ya eneo hilo kuwa Hifadhi ya Taifa ni katika jitihada hizohizo za kuimarisha uhifadhi lakini pia kukuza utalii. Kwa hivyo, Benki ya Dunia hawajasema neno lolote lile kwamba watasitisha utekelezaji wa mradi huu katika eneo hilo na wanaunga mkono kwa sababu malengo yapo palepale.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, kuna suala la UNESCO kwamba hatujawaarifu UNESCO kwamba pengine tutapoteza hadhi ya kuwa eneo la Urithi wa Dunia, hapana. Eneo hili bado ni mali ya Serikali na kwa kuwa lipo chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii, linasimamiwa na msimamizi mmoja kwa maana ya administration yake na msimamizi huyu ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, hizi taasisi zote zinafanya kazi kusimamia mali ambazo zipo chini ya Wizara ambazo ziko chini ya custodian wake mkuu ambaye ni Katibu Mkuu wa Wizara. Kwa hivyo, iwe katika hadhi ya pori la akiba ama Hifadhi ya Taifa bado msimamizi/mmiliki ni yuleyule mmoja ambaye amepewa dhamana ya kusimamia naye ni Katibu Mkuu. Kwa hivyo, UNESCO hawatoweza kubadili kutunyang’anya hiyo hadhi kwa sababu tumepandisha tu hadhi ya kiuhifadhi zaidi tumebadilisha matumizi sasa inakuwa Hifadhi ya Taifa kwa sababu eneo ni lilelile na simamizi ni yuleyule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni kwa mujibu wa kanuni za UNESCO ile kanuni ya 172 ambayo inaeleza namna kama nchi itaamua kubadilisha mipaka ya usimamizi katika eneo lake ama itaamua kumbadilisha msimamizi. Taratibu ambazo zitapaswa kufuatwa na nchi yetu ni kupeleka taarifa ya mabadiliko hayo ya matumizi ambayo tumeifanya na wala hakuna shida yoyote kwa sababu hatubadilishi mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo napenda kulizungumzia ni eneo la mifugo, kwanza hakuna makazi wala mifugo ndani ya Pori la Akiba la Selous. Mifugo ambayo inaonekana ipo katika ukanda huo wote, ipo katika maeneo mengine nje ya Pori la Akiba la Selous na haya ni maeneo ambayo pia yanahifadhiwa katika hadhi nyingine mbalimbali tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kuna mifugo mingi sana katika eneo la Kisarawe na pale ilipo inavamia kwenye Hifadhi ya Jumuiya ya Gonabis ambayo ni WMA ya wananchi. Na tumeona sasa ili kupunguza presha katika ikolojia hiyo yote basi tutamega sehemu ya hifadhi hii ya Jumuiya ya Wanyapori ya Gonabis na kuwapa wananchi ambao ni wafugaji lakini tuta-restrict matumizi badala ya kuruhusu wajenge makazi na waishi humo ndani ya WMA tutawaruhusu katika kipindi fulani fulani cha mwaka waweze kuingiza Mifugo yao katika eneo ambalo tutaliwekea mipaka ili waweze kuchunga. Lengo ni kupunguza pressure katika ikolojia hiyo nzima ili wananchi pia waweze kupumua, wafugaji nao kupata mahitaji yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu miundombinu, hii ni habari njema kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi wenzangu wote wanaotokea mikoa ile, kwa sababu tunavyoenda kuweka mkakati wa kutengeneza Hifadhi ya Taifa pale, miundombinu ni jambo la lazima. Ilivyokuwa zamani ili ufike Selou njia rahisi zaidi ilikuwa ni kuruka kwa ndege hizi ndogo ambazo ni gharama kubwa sana lakini utalii wa picha kwa kiasi kikubwa unahitaji miundombinu mbalimbali ikiwemo usafiri wa reli, Mheshimiwa Rais tayari yuko katika mkakati wa kufanya mazungumzo lakini pia kutekeleza mradi wa kuboresha reli ya TAZARA, kwa hivyo, itakuwa ni njia mojawapo ya kufika katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, pia kuna barabara tayari Mheshimiwa Rais alishaagiza ijengwe kwa kiwango cha lami. Katika mradi huu, Serikali sasa itajipanga kuhakikisha Selou na Nyerere National Park panafikika kirahisi zaidi kuliko ilivyo sasa kwa sababu watalii wa picha wakiwemo wa ndani ni rahisi zaidi kufika kwa njia ya barabara kuliko hizi ndege ndogo ambazo ni gharama kubwa.

Mheshimiwa Spika, pia kupitia mradi REGROW tutajenga viwanja vya ndege vidogo vidogo visivyopungua vitano. Vilevile kwa sasa tunafanya utafiti ili tuweze kujenga kiwanja kimoja cha ndege kikubwa eneo la Kisaki, nje kidogo ya hifadhi ya Taifa ya Nyerere ili iwe ni rahisi kufika katika eneo hili. Kwa hivyo, Waheshimiwa Wabunge wenzangu hizo ni fursa ambazo zitakuja kwa kupata hifadhi mpya ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu kwamba utalii utaporomoka, hapana. Utalii hauwezi kuporomoka ndiyo utakua sasa kwa kasi zaidi kwa sababu tunaenda kuwekeza kwa nguvu zaidi.

Mheshimiwa Spika, mapato ya TAWA, nimeshajibu hayatashuka. Labda moja ambalo napenda kulifafanua tena, naona na muda umenitupa mkono ni kuhusu wafanyakazi, Mheshimiwa Mlinga ameliongea kwa uchungu sana naomba nilifafanue.

Mheshimiwa Spika, wafanyakazi hawa ni wa Serikali kwa ujumla wake, kwa mujibu wa Kanuni za Utumishi wa Umma, kwamba yuko kwenye taasisi gani ni jambo moja lakini jambo lingine ambalo ni la ukweli sana ni kwamba kwa kuwa ni watumishi wa Serikali stahiki zao zote za msingi kwa mujibu wa taratibu za Serikali ziko pale pale. Kwa hiyo, kama yupo kwenye parastatal ambayo inatoa zaidi ya kile ambacho kinatolewa na Serikali, hiyo ni bahati yake lakini kwamba wabaki palepale ni jambo ambalo linaweza likafikiriwa, naomba nilichukue tuone kama kwa mujibu wa sheria linaweza likatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata kama likishindikana pia siyo jambo baya kwa sababu kuna maeneo mapya mengi ambayo yanaanzishwa na yanapandishwa hadhi kuwa Mapori ya Akiba na yako chini ya TAWA na watumishi watakaotoka katika eneo hili wanaweza kwenda kuanzisha hayo maeneo mapya. Pia sisi kama Serikali tunaona tunavyozidi kufanya maboresho ya taasisi hii mpya ya TAWA ndivyo ambavyo mapato yake yanakua na pengine katika hatua fulani na wao wataweza kufikia hatua hiyo ya kulipwa vizuri zaidi kama ambavyo leo wafanyakazi wa TANAPA wanalipwa.

Mheshimiwa Spika, wewe mwenyewe ni shahidi wakati mnaanza kazi kwenye maeneo haya ya uhifadhi mlikuwa mnavaa ‘chachacha’, vijana wadogo wadogo kama Mlinga pengine hawakuwahi kuziona, lakini enzi hizo kulikuwa hata viatu hakuna, sare za kuvaa kulikuwa hakuna na hata waliokuwa TANAPA walikuwa hawapati hayo mahitaji. Hata TAWA wakati inaanza hata sare pia walikuwa hawana lakini leo hii watumishi wote wa TAWA wana sare nzuri, wanavaa viatu vizuri, wanalipwa vizuri, wanapata stahiki zao vizuri, japokuwa katika kiwango cha chini. Kwa hivyo, kadri TAWA inavyoendelea kuimarika ndivyo ambavyo na wao watazidi kuboreshewa maslahi yao.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii na naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, naafiki.