Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Kuridhia Mapendekezo ya Ubadilishaji Hadhi Sehemu ya eneo la Pori la Akiba la Selous kuwa Hifadhi ya Taifa ya Nyerere

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja hii ya hili Azimio lililoko mezani. Kwanza ni- declare interest kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati na moja ya mambo ambayo tumeyachekecha katika kupitia na kutolea maoni Azimio hili ni uhalisia wa eneo ambalo limependekezwa limeguliwe na sehemu fulani ibakie kuwa Hifadhi ya Taifa na sehemu nyingine ibakie kama Pori la Akiba.

Mheshimiwa Spika, katika uchambuzi wetu kwenye Kamati ambayo maoni yetu nayaunga mkono asilimia 100 pamoja na wazo la Mheshimiwa Rais la kupanua wigo wa maeneo yaliyohifadhiwa nchini na kuweka sehemu ya Selous kuwa mojawapo, tumeona kwamba kuna faida mara mbili endapo eneo hili litachukuliwa katika ujumla wake na kuhifadhiwa kama mamlaka sawa na ile ya Ngorongoro. Kwa maana hiyo sasa tutakuwa na mamlaka mbili ya maeneo yaliyohifadhiwa yenye matumizi ya aina mbalimbali badala ya kuwa matumizi ya aina moja tu kwa maana ya tofauti ya National Park na Conservation Area ni kwamba kwenye National Park ni exclusive use ya matumizi ya kupiga picha tu utalii wa picha, lakini kwenye conservation area kuna matumizi mseto ndiyo maana kwa sababu eneo hili lilikuwa ni eneo la akiba la uwindaji, tutakapokuwa tumekubaliana kwamba sasa na yenyewe liwe mamlaka kama Ngorongoro, tutakuwa na hiyo fursa ya kuwekeza kwenye utalii wa picha katika yale maeneo ambayo utalii wa picha unawezekana hasa eneo la Kaskazini maana nimeangalia katika kumbukumbu zilizopo hili pori linaweza likatengwa katika maeneo manne.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la Kaskazini ambalo limepakana na Hifadhi ya Mikumi ni eneo safi kabisa kwa utalii wa picha na eneo la Mashariki na eneo la Kusini na eneo la Magharibi haya ni mapori ambayo hata leo tukisema yote iwe National Parks itatuchukua miaka mingi sana kuyaendeleza, kuwekea miundombinu, kuna milima kuna misitu kuna maeneo oevu na ningefikiri kwamba tunapochukua kama ni eneo la hifadhi kama la Ngorongoro tunakuwa tumepata faida ya kuwa na maeneo ya utalii wa picha na yale matumizi mengine ya uwindaji wa kitalii ambayo yatafanya yale mapato yawe maradufu.

Mheshimiwa Spika, tutapata mapato kutokana na utalii wa picha katika eneo ambalo lina hadhi ya kama National Park na tunapata matumizi ya ule uwindaji wa kitalii ambao pia utatuletea manufaa makubwa.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo katika Kamati tuliona kwamba mapendekezo ya Mheshimiwa Rais ambayo tunayaunga mkono asilimia 100, yalitamka Nyerere National Park, tukasema tusipoteze jina la Mwalimu wetu kwa sababu Mwalimu ni cheo ambacho mtu hata ukipandishwa hadhi ukawa Rais bado utaendelea kuitwa Mwalimu na ndiyo maana Mwalimu anaitwa Mwalimu milele.

Kwa hiyo, ibakie kwamba Mwalimu Nyerere Conservation Area kama ndiyo moja ya majina ambayo tunapendekeza kama Kamati nami naunga mkono, pia lisimamiwe na TAWA.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu unaweza ukajiuliza hapo ulipo kwamba Ngorongoro ndiyo waje wasimamie? Jibu ni hapana TAWA tayari walikuwa wanalisimamia kama pori la akiba nasi katika maoni yetu na maoni yangu binafsi naona kwamba TAWA nao wapewe fursa ya kusimamia eneo la hifadhi inayofanana na Ngorongoro, wakachukue somo kule Ngorongoro wamefanikiwaje na wawekewe kabisa bajeti ya kutosha kwa sababu lile pori ni kubwa waweze kuli-manage likiwa na sehemu mbili. Sehemu ambayo ina utalii wa picha, linalofanana kabisa na Mbuga yoyote ya Taifa na eneo lingine lililobaki ambalo litaendelea na yale matumizi ambayo yalikuwa yameshabainishwa.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nilikuwa najiuliza na naomba hili nitoe kama maoni binafsi kwamba huku sasa tunaelekea kuwa na taasisi mbalimbali za uhifadhi hapa nchini, tunayo TAWA, tunayo Misitu, tuna TANAPA, na sasa pia tuna Ngorongoro, kwanini tusifikirie tuunganishe hivi vyombo vyote tukawa na chombo kimoja? Kwa mfano Kenya, wao wanayo ‘Kenya Wildlife Service’, Uganda wanayo ‘Uganda Wildlife Service’ nasi labda tuje na pendekezo nilikuwa najisemesha mwenyewe hapa kwa kufikiria nikasema kwanini tusiwe na Tanzania Wildlife and Nature Conservation Authority ikachukua hizi Taasisi zote pamoja zikaunganishwa tukawa na mamlaka moja inayosimamia uhifadhi wa wanyamapori na mazingira yake katika Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, tukija na huo model basi tutakuwa tunaya-manage maeneo yote bila kuwa na utengano na kuwa na moja ambayo inajiona kwamba ni dhaifu, nyingine ni bora kuliko nyingine na kwa njia hiyo tutakuwa tumehifadhi rasilimali yetu ya Tanzania katika upeo na mtizamo mpana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema kwamba maono ya Mheshimiwa Rais na hekima yake tumepokea kwa furaha kabisa na tunampongeza kwa kuwa na maono ya kuhifadhi Selous kama National Park na tunamuongezea maoni yetu kwamba iwe ni mamlaka ambayo inasimamiwa kwa ujumla wake bila kugawanywa na isimamiwe na taasisi moja ambayo ni TAWA.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana naomba kuwasilisha na naunga Azimio mkono asilimia 100. (Makofi)