Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa na mimi fursa nianze kwa kuunga mkono hoja na vilevile kuwapongeza sana viongozi wa Kamati yangu na Wajumbe kwa kazi kubwa wanayofanya ya kutushauri Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli tumeanza vizuri mwaka huu na kama alivyosema Mheshimiwa Mtulia nyota wetu wa soka ambaye vilevile nahodha wa timu ya Taifa akatufungulia milango, akawafungulia milango vijana wetu Watanzania kuingia kwenye ligi ya heshima duniani, kubwa ya EPL ila tu niombe Watanzania najua mmehamasika sana tujiebushe na kauli zisizo na staha kwenye mitandao ya michezo inayotumiwa na wengi, badala ya kumsaidia Samatta hatumsaidi bali tunamjengea uwasama kijana wetu na wenzake huko ughaibuni nawaomba sana hasa katika kutumia mitandao na bahati mbaya sana wanaowatafsiria wenzetu huko Aston Villa siyo Watanzania, ni wenzetu ambao hawatutakii nia njema ni Kiswahili watapotosha tu, kwa hiyo, hebu tujihadhari sana na mihemuko iliyopitiliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwaeleza tu Watanzania na Waheshimiwa Wabunge sasa hivi tuna wachezaji 22 wanaocheza nje nchi ambao tukiwahitaji wakati wowote wapo tayari kuisaidia timu ya Taifa bila kumsahau kinda wetu Kelvin John ambaye sasa hivi yupo kwenye football academy ya Uingereza na timu nyingi kwa kweli zinamtolea macho sasa hivi. Leo tumempokea hapa Bungeni Salim Mtango wa Tanga kwa kubeba mkanda wa UBO wa dunia na mwenzake vilevile Mchanje Yohana wa Tanga huko huko naye amebeba mkanda wa UBO nawapa pongezi sana tena sana. Sasa hivi Tanzania tuna jumla ya mikanda 12 ya Kimataifa. Kwa hiyo, tunafanya vizuri sana kwa ndondi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rashid Shangazi namshukuru Mbunge wa Mlalo amelalamikia usikivu hafifu wa TBC maeneo kadhaa ya nchi yetu. Nitumie nafasi hii kuelezea tu kwamba mara baada ya Uhuru Baba wa Taifa alihakikisha nchi hii inajenga minara minane ya masafa ya kati dhidi ya (medium wave) na hiyo minara kwa kweli, ni kama iliweza kujitosheleza nchi nzima ilikuwepo Dar es Salaam, Arusha, Mwanza, Kigoma, Dodoma vilevile Mbeya, Songea na Nachingwea, lakini teknolojia ya mawasiliano inakwenda kwa kasi sana, mitambo ya medium wave ilianza kupoteza/kuondoka kabisa katika teknolojia ikaingia mipya kabisa ambayo kwa kweli kusikia inafurahia lakini ina matatizo pia kwa upande hasa sehemu ambayo kuna vizuizi kama milima, tukaingia huu teknolojia ya frequency modulation (fm) na mitambo ile kwa sababu imekosa watengenezaji waliacha kabisa ikakosa kwakweli vipuli kwahiyo nchi ikaingia kwenye mtikisiko mkubwa sana wa jinsi gani tutatoka huko ndiyo tukaanza kutumia kuweka sehemu mbalimbali za nchi mitambo ya fm.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeweza kwa mfano katika muda mfupi uliopita Serikali ya Awamu ya Tano ilipoingia usikivu wa TBC ulikuwa asilimia 54 tu sasa tunaelekea kwenye asilimia sabini na kitu, tumekwenda Wilaya za mpakani Rombo, Longido, Tarime, Kibondo na Nyasa, lakini huwezi tu ukaweka ukaacha inabidi urudie tena kuangalia kwa sababu mawimbi haya yana tabia ya kuhama kutokana na topography.

Kwa hiyo, tumepita hivi karibuni tumeenda Tanga kuangalia mitambo yetu tukakuta kweli bado tuna matatizo baadhi ya sehemu kutokana na mitambo yetu kukosa nguvu, sasa iliyoko sehemu ya Mnyuzi sehemu kama Mkinga na Kilindi inabidi turudie na ninawahakikishia Wabunge kutoka Mkoa wa Tanga kwamba eneo hilo tumeliona Mkinga na Kilindi kuna matatizo. Vile vile tulikwenda Lushoto tumeona kuna mitambo pale lakini hata tukiikarabati na tutaikarabati ndani ya miezi mitatu ijayo bado Bumbuli na Mlalo wanatatizo ambalo wanahitaji kwa kweli kulifanyia kazi na tunawahakikishia ndani ya mwaka huu tutatatua tatizo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekwenda kilimo cha Mabungo ambacho kipo Moshi vilevile mtambo wetu vimeshika sana nguvu yake inahitaji ukarabati, vipuri vyote vimeshafika, lakini hata tukisha karabati bado Rombo itaendelea kupata matatizo kutokana na milima milima sehemu ile, Rombo inahitaji kwa kweli tuifanyie kazi zaidi pamoja na kwamba Rombo hapo hapo tuna mitambo mipya inabidi tuongeze mitambo mingine ni kama ambavyo tutakavyofanya Longido ambako tuna mitambo tayari Namanga, tuna mipambo Longido DC lakini mitambo Longido DC lakini bado lazima tuongeze mitambo mingine kutokana na topography ta eneo hilo, tumeenda Manyara, tumeenda Singida hali iko hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu mwaka huu wa fedha tunaweka mitambo Unguja na Pemba kwa bajeti mliopitisha hapa, tunaweka mitambo Simiyu na vilevile tunaboresha usikivu Songwe na Ludewa kwa Mheshimiwa Ngalawa. Vilevile, kwa ushirikiano kwa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote tutaweka mitambo Kilwa, tutaweka Itigi, Ruangwa, Kilombero na bila kusahau Kyela.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Amina Mollel kwa kuona juhudi za Wizara katika kuboresha matangazo ya TBC.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Maendeleo ya Huduma za Jamii imelalamikia ubovu wa miundombinu ya michezo; napenda kusisitiza kwamba ndugu zangu kwa kweli ni jukumu letu sote si jukumu la Serikali peke yake Wizara, Taasisi, Mashirika ya Umma, sekta binafsi na hata sisi Waheshimiwa Wabunge unaweza ukajenga hata kiwanja cha volleyball kwa kutumia pesa ya Mfuko wa Jimbo au kiwanja cha netball.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli ni wajibu wetu wote tusisubiri tu Serikali peke yake na wito huu tumeshautoa na umepokewa kweli na mikoa mingi, tunashukuru sana Mkoa wa Arusha ambao umetoa agizo, umeazimia kwamba kila Halmashauri itajenga viwanja vya michezo na wao Jiji la Arusha wameamua wameanza nimeenda kuangalia kiwanja cha Ngarenaro, ni kiwanja changamani kuna netball, kuna basketball, kuna mchezo wa soka pale kiwanja kizuri kimemalizika kwa asilimia 80 wanajenga kwa jumla ya shilingi milioni 360. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeenda sehemu inaitwa Sinoni, kuna Mtanzania pale anaishi Marekani amekumbuka nyumbani, amejenga kiwanja kizuri sana kina taa mpaka za usiku kwa ajili ya watoto kwa shilingi milioni 126; hawa vijana wa kutolewa mfano kuliko vijana wenzetu wengi wanaokaa nje muda mwingi wako kwenye mitandao ya kijamii. Unafuatiwa Mkoa wa Dar es Salaam, nilishasema naipongeza Simba Sports Club wanajenga viwanja viwili, kimoja cha nyasi na kingine kiwanja cha nyasi bandia huko Bunju. Vilevile Manispaa ya Kinondoni inajenga uwanja wa kisasa Mwenge kwa shilingi bilioni 2.7 na ukamilika mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijawatendea haki Manispaa ya Songea Mjini kwa Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro, wametenga eneo la ekari 50 katikati ya Kata ya Lirambo na Peramiho kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja cha kisasa cha gofu. Sasa hapa tutaona ndugu zetu wa Songea hiyo gofu watakapoanza kujifunza, lakini kwa kweli nina uhakika kutokana na uzuri wa eneo lenyewe na hakika nchi nyingi zitakimbia kuja kufanya mchezo kule wa gofu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii vilevile kuwatahadharisha wana Tanga wanaonisikiliza saa hizi wanaovamia eneo la TFF la Mianjani ambako kutajengwa training center yenye viwanja na vilevile hosteli. Naomba niwasisitizie kwamba hawatalipwa fidia, kuna mtu anawadanganya danganya sehemu za ardhi/ofisi zetu hizi kwamba hebu jengeni mtalipwa fidia, fidia haitalipwa, nataka niwahakikishie hilo na ujenzi utaanza muda si mrefu kutoka sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kubenea amelalamikia anauita ushabiki wa TBC, nilitaka nisisitize tu kwamba Mheshimiwa Kubenea kupitia kwako kwamba TBC ni chombo la Serikali, hilo haliwezi kubadilika na TBC inachokifanya siyo tofauti na vyombo vingine vya Serikali duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TBC iko pale kuelezea kwa kinagaubaga utekelekezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo za Serikali ambavyo hivi vitu haviwezi kupata nafasi kwenye vyombo vya habari binafsi ambavyo vinaangalia zaidi faidi at the end of the day. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pengine wengine hawana habari, BBC mnayoiona kila siku msije mkafikiri iko pale kwa msaada hapana. BBC leo iko pale kwa umri wa miaka 98 haijawahi kuzimwa hata siku moja, iko pale kwa maslahi ya Serikali ya Uingereza, sio inatusaidia na sisi tupate taarifa iko pale kwa maslahi. VOA huu mwaka wa 78 haijawahi kuzimika inatangazwa kwa lugha 47, BBC lugha 40, wafanyakazi zaidi ya 3500 kila chombo kwa ajili ya nini. Kama ingekuwa kuwatangazia Waingereza wenyewe si ingekuwa kiingereza peke yake hivi ni vitu vya kimkakati kila nchi inafanya, msiishambulie TBC bila sababu, kuna Serikali inafannya vitu, lazima vitangazwe. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, sijui nimesikia kengele? Ooooh!

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)