Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, awali ya yote nitoe shukrani za dhati kwa Kamati kwa taarifa yao nzuri ambayo wamewasilisha leo katika Bunge hili tukufu na ambayo kwa uwazi kabisa imesifia utendaji mzuri wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sifa hizo ambazo tumezipokea kwa mikono miwili toka kwenye Kamati zinatokana na kazi nzuri ambayo Wizara inaifanya katika kudumisha mahusiano ya kidiplomasia kati ya Tanzania na nchi mbalimbali duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipimo cha mahusiano ya kidiplomasia kipo cha aina tofauti. Kila mtu anaweza akajaribu kutaka kupima kwa vile anavyopenda yeye lakini kuna vipimo rasmi ambavyo wataalam wanavitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja, tunaangalia tuna balozi ngapi katika nchi mbalimbali na balozi ngapi zina uwakilishi hapa nchini. Kwa kipimo hicho tumefanya vizuri sana na tunakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tunaangalia tunashirikiana kiasi gani na nchi mbalimbali. Hivi juzi Waziri wa Ulinzi amepokea msaada wa magari ya jeshi kutoka Marekani. Hicho ndicho kipimo cha uhusiano wetu wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Marekani, uhusiano mzuri kiasi kwamba tunaweza kushirikiana hata katika masuala ya ulinzi na usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia mahusiano yetu na Jumuiya ya Ulaya ni mazuri sana. Jumuiya ya Ulaya imeleta Balozi wake, ameshawasili na anafanya kazi vizuri na sisi tumepeleka Balozi Brussels na kwa maana hiyo tayari Jumuiya ya Ulaya imeshaweza kuleta fedha, Euro milioni 62, kuthibitisha mahusiano hayo mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka kuelewa misingi ya diplomasia duniani, watu wengi sana wamechangia na niwaombe wote waliochangia kwanza wakasome Montevideo Convention ya mwaka 1933, lakini pili, wakasome Westphalia Treaty ya mwaka 1648, hizi nyaraka mbili ndiyo miongozo thabiti ya kidiplomasia duniani. Tusije tukachangia tukadandia gari wakati hatujui gari linaelekea mwelekeo upi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niruhusu nitoe ufafanuzi kwa faida ya Waheshimiwa Wabunge na kwa faida ya Watanzania wote ambao wanatuangalia. Mheshimiwa Salome Makamba wakati anachangia amesema kwamba Wizara ilitoa majibu mabaya dhidi ya Serikali ya Marekani. Naomba niliambie Bunge lako tukufu kwamba Wizara haijatoa kauli yoyote kuijibu Serikali ya Marekani na kwa misingi hiyo, nimuombe Mheshimiwa Salome Makamba alithibitishie Bunge hili ni taarifa ipi ambayo Wizara imetoa dhidi ya Serikali ya Marekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia limeongelewa suala la wanafunzi na Watanzania waliopo China na tishio la ugonjwa unaosababishwa na virus anaitwa corona. Kwa sababu suala hili ni muhimu, nalo naomba nilitolee ufafanuzi; mpaka tunavyoongea hivi sasa, katika Jimbo la Huan na Mji wa Hubei kuna wanafunzi wa Kitanzania 437 na kuna familia moja ya Kitanzania yenye watu wanne, hivyo kufanya Watanzania waliopo katika jimbo hilo kuwa 441.

Mheshimiwa Spika, kwa taarifa ambazo tunazipata mara tatu kwa siku, kama vile dozi ya panadol, hakuna Mtanzania ambaye ameathirika na ugonjwa huo. Hivyo niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwa ujumla kwamba Watanzania waliopo China katika Jimbo la Huan wako salama salimini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumeruhusu Watanzania wengine kutoka kwenye majimbo mengine waweze kurejea pale wanapopenda wao kurejea kwa sababu tunaheshimu uhuru wao wa kuweza kutembea na kuja huku kusalimia ndugu kwa sababu hawatoki katika jimbo hatarishi. (Makofi)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, ninaomba kuwasilisha. (Makofi)