Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama Kuhusu Shughuli za Kamati Kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa na mimi nimeomba nafasi hii kwa sababu ya mambo madogo mawili tu ambayo nilifikiri ni muhimu niyazungumze katika hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, asilimia 85 ya watu wa Rwanda ni wakristo, na kama mtakumbuka mauaji ya Kimbari yaliyotokea Rwanda wakristo hawa hususan Wakatoliki wenzangu walihusishwa sana na yale mauaji, na ni kweli kwa sababu kuna wahanga walikimbilia katika makanisa, lakini baadhi ya mapadre wakawatosa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ili baadaye nieleze ninachotaka kusema ninakumbusha miaka ya 1980 kulikuwa na mihadhara inaendelea nchini kwetu, na mihadhara hii iliwahusu sana Wakristo na Waislam. Wakristo tulilalamika sana Waislam walipokuwa wanalitaja jina la Bwana Yesu na walikuwa wanasema kwao ni Nabii Issa Aleyhi-Salam, lakini mapambano yalikuwa makubwa matokeo yake mihadhara iliachwa. Hakuna asiyekumbuka kipindi kile hali ilivyokuwa mbaya.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninalotaka kusema ili niweze kueleza vizuri hoja yangu, Mheshimiwa Rais, Dkt. John Joseph Pombe Magufuli anahimiza Watanzania tufanye kazi ili kila mtu aweze kupata ujira wake na kipato chake kutokana na kufanya kazi, na hata vitabu vya dini vinahimiza kazi. Mtume Paulo kwa Wakristo mnajua anasema asiyefanya kazi na asile chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nayasema haya kwa sababu ya hoja ya ulinzi na usalama tunayojadili na sasa hapa nataka ku-refer Wizara ya Mambo ya Ndani. Wizara ya Mambo ya Ndani ndiyo inayosajili vikundi vya dini katika nchi yetu na kwa maoni yangu ni kwamba sheria iko wazi na kanuni zipo na Wizara inajiridhisha kabla ya kufanya huo usajili. Na niseme wazi mimi sina tatizo na kikundi chochote cha dini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini yapo matendo ambayo yanafanywa na baadhi ya vikundi vya dini yasipoangaliwa na nchi na wenye mamlaka yanaweza yakalitumbukiza Taifa hili mahali pabaya kwa sababu ya hofu ya kuingilia uhuru wa dini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama anasimama Mchungaji au Askofu anawaambia watu fungueni mapochi yenu hela ziingie na anatoa hotuba labda kuanzia asubuhi mpaka jioni, ni wazi vijana wataacha kufanya kazi, watakwenda kufungua mapochi yao wakisubiri fedha ziingie kwa upepo wa kisulisuli. Sasa hii si sahihi. Na ndiyo maana nasema kama Wizara inavijua vigezo vya kusajili haya makanisa, mambo kama haya Wizara inapaswa iingilie kati kwa sababu jambo kama hili likiendelezwa linaharibu nchi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, wako wengine anasajili kanisa, baba ni askofu, mama ni mchungaji, kijana anaokota sadaka wanaweka maturubai barabarani ndiyo kanisa, wanawadanganya wananchi kwa kuwapa maji wanasema ni ya upako, wala maji hayo hatujui kama yamepitia TBS, wanawapa mafuta wanasema ni ya upako, hatujui kama yamepitia TBS, halafu matokeo yake watu wanachukua wanabugia tu wanaokota sadaka. Kwangu mimi anapomtaja Bwana Yesu au Roho Mtakatifu katika hoja kama hiyo mimi naona ni kashfa kwa sababu huyo sio Roho Mtakatifu ni roho mtaka vitu. Na lazima Wakristo wanajua tofauti ya Roho Mtakatifu na roho mtaka vitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yako mengi yanayoendelea, na wanaoumia ni akina mama. Sijui ni kwa sababu gani kwa sababu akina mama wengi ndio wanaoonekana kwenye makanisa hayo. Mtu anawaambia akina mama waondoe nguo za ndani wapunge hewani ili wapate ujauzito, tunaona tu na Serikali ina mkono mrefu nina imani hata kwenye haya makanisa Serikali ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa iko siku wanaoamini katika roho na kweli hao wakwelikweli wataamua kumtetea Yesu Kristo, bwana na mwokozi wa kweli baada ya kuchoka kashfa hizi na itakuwa mbaya. Sasa mimi naiomba Serikali isogope kupitia sheria inayosajili hivi vikundi vya dini. Kama kuna haja ya kuihuisha iihuishe ili iweze kuangalia ni vikundi gani kweli vya dini au ni vikundi gani vimekuja nchini kuja kufanya utapeli kwa ajili ya kuwaibia Watanzania. Serikali inao wajibu wa kulinda raia wake na kitu kidogo ambacho raia wanapata ili matapeli wasije wakaingia wakawapora.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninapenda kulizungumza ni kwamba tunakwenda kwenye uchaguzi na Mheshimiwa Rais wiki iliyopita amesema kwamba atahakikisha uchaguzi unakuwa huru na wa haki. Sasa uko ushauri amekuwa akipewa, wiki hii amepewa ushauri na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo, nina hakika atauzingatia na ninamuomba auzingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini na mimi nataka nimpe ushauri ambao tumekuwa tukiusema mara nyingi, wapo Watanzania wengi wanaoishi nchi za nje wakifanya biashara au wapo katika balozi zetu, sasa hivi tunahuisha daftari la kupiga kura bado hakuna kauli ya wazi ni namna gani Watanzania hawa watapata nafasi ya kujiandikisha kupiga kura au ni namna gani watakavyopiga kura. (Makofi)

Kwa hiyo ninaomba wakati ushauri mbalimbali ukitolewa na kuzingatiwa basi jambo hili ambalo tumelizungumza muda mrefu kwa miaka mingi lizingatiwe kwa sababu ni haki ya Kikatiba ya kila Mtanzania kuchagua uongozi wa nchi, kuchagua viongozi wanaowataka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, ni kwamba mtu akiwa mfungwa au akiwa mahabusu hapokwi haki zake. Hata jana au juzi tulimsikia Mwanasheria Mkuu wa Serikali akisema kuna haki ambazo wafungwa wamepewa na hazipaswi kuondolewa. Haki moja wapo ni hii ya kuchagua, wale wafungwa na wenyewe tunaomba wakati mazingatio yakifanyika ya namna tutakavyokwenda kwenye uchaguzi huru na wa haki, nao waweze kupewa nafasi ya namna ambavyo watajiandikisha na namna ya kupiga kura.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa, ninawaomba Watanzania wa vyama vyote, wa taasisi zote, kwa kawaida tunapokwenda kwenye uchaguzi lazima mihemko inapanda kwa kila mtu. Juzi Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi aliwakemea wale vijana ambao walikuwa wanawaalika wenzao kwa ajili ya kuwadhibiti vijana wa vyama vingine, hili ni jambo zuri alilofanya na kwa kweli nampongeza kwa jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini twende mbele zaidi, ile ni jinai, watu wanaofanya jinai namna hiyo wasikemewe tu kwa sababu watazoea kukemewa, watazoea kudekezwa. Imani yangu ni kwamba kama Serikali watu wa namna hiyo isipoanza kuwadhibiti tangu mapema zikaanza kutolewa kauli za kutishana namna hii, matokeo yake tunaweza tukafika kwenye uchaguzi tukiwa hatuko salama, tukafika kwenye uchaguzi nchi ikiwa vipande vipande. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naomba sana sisi Wabunge, viongozi wa vyama, wa taasisi za vyama na mabaraza ya vyama tujiepushe na kutoa kauli za kuwachochea Watanzania, za kuwachochea vijana wetu katika muda huu kwa sababu uchochezi huu unaweza ukaligawa hili Taifa na hatuna nchi nyingine zaidi ya Tanzania na tunao wajibu wa kuilinda Tanzania kwa nguvu zetu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ahsante sana. (Makofi)