Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Elias John Kwandikwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ushetu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kupata nafasi ya kuchangia hoja zilizo mbele yetu, lakini nitajikita kwenye eneo moja tu la miundombinu, hususan sekta ya ujenzi. Nimshukuru sana Mwenyekiti wa kamati na kamati nzima kwa kweli, kwa muda wote ushauri wao na maelekezo yao na kwa kiasi kikubwa tuliyazingatia na kwa kweli, yametupa ufanisi maeneo mengi. Na ndio maana Mheshimiwa Mwenyekiti hapa wakati wa kuwasilisha ametoa shukrani kuona Serikali inafanya kazi kubwa na kuweza kutekeleza pia, maoni ya kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipongeze tu Bunge kwa ujumla. Nasoma ripoti, nimezisoma ripoti tangu tulivyoanza kuzipokea katika Bunge lako, lakini utaona kuna maboresho makubwa sana. Na hata ukiiangalia ripoti ya wenzetu Kamati ya Miundombinu utaona kumekuwa na mabiresho makubwa. Hata maoni yake ambayo tumeyapokea ni maoni ambayo yanalenga kwenda kutuboreshea shughuli zetu, lakini pia ni maoni ambayo yanatekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya ujenzi ni muhimu kwa sababu ni sekta wezeshi, inatoa huduma kwenye ukuaji wa viwanda, kwenye kilimo na kwenye huduma mbalimbali kwa hiyo, tumepokea maoni ya kamati. Na maeneo ambayo yalikuwa yameguswa ni upande wa TANROADS, upande wa barabara, ujenzi wa viwanja vya ndege, upande wa Wakala wa Majengo Tanzania, pia tumepokea maoni kwenye Chuo cha Ujenzi Morogoro na Chuo cha Mafunzo ya Teknolojia Stahiki Nguvu Kazi kule Mbeya, lakini pia upande wa wakala wa ufundi na umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufundi kabisa tumeona changamoto ambazo kamati imezitaja. Nilihakikishie Bunge lako ushauri huu mzuri sana tutaendelea kuuzingatia, ili tuone kwamba tunakwenda kufanya maboresho makubwa, lakini kwa lengo hilohilo la kuona kwamba, tunaendeleza mkakati wetu wa kuwa wezeshi, ili kuweza kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo kadhaa Waheshimiwa Wabunge pia, wakati wakichangia hoja hii wameyazungumza, lakini niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba, changamoto za barabara, hususan kwenye kipindi hiki cha mvua nyingi na kamati imetushauri kwamba, tuangalie mtazamo kwamba, kipindi cha miaka hii ambapo mvua inakuwa nyingi pia, ile bajeti yetu upande wa dharura tunaweza kuiweka, lakini kimsingi ukiuangalia bajeti zetu tunavyoziunda tunakuwa tunapangilia hivyo kwamba, kuna maeneo korofi, kuna maeneo ujenzi wake ni wa muda. Tukitoa mwanya kwamba, wakati tukiwa tunazingatia kwamba, tumetenga fedha kwa ajili ya periodic maintenance kwa maana hiyohiyo kwamba, yako maeneo mengine ambayo kurejeshea miundombinu inategemea pia, kwamba, hali ya mvua iwe imepungua. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge kwa maeneo ambayo tunaona bado tuna changamoto na mvua imekuwa nyingi kwamba, tutakwenda kufanya marejesho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokuwa nikizungumza mara nyingi kwa utaratibu wa kibajeti kama Mheshimiwa Waziri wa Fedha alivyozungumza tunafanya mawasiliano. Kwa sababu, tulikuwa na bajeti ya bilioni 8.2 kwa ajili ya dharura, lakini hadi kufikia mwezi wa kwanza mwanzoni tulikuwa tuna mahitaji ya kwenda kwenye bilioni 15, lakini hivi ninavyozungumza kumekuwa na mvua nyingi zimenyesha kwenye Mikoa ya Mara kule, lakini mvua nyingi zimenyesha pia, kule Simiyu. Tunaendelea kupokea shida mbalimbali kwenye maeneo mengi, lakini niwahakikishie tu kwa sababu, Serikali inazingatia kuona watu wanapita katika maeneo yao kwenye changamoto za barabara niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tumejipanga kuwasiliana na wenzetu upande wa Wizara ya Fedha kwa utaratibu wa kibajeti, ili tuende kurejeshea mahitaji ya sehemu ambazo zimeharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimalize tu kwa kusema kwamba, Waheshimiwa Wabunge michango yao yote waliyoisema sisi tumeichukua kwa nia hiyo ya kwenda kufanya maboresho. Na nimalizie kwa kusema naishukuru sana Kamati na tutaendelea muda wote kusikiliza maoni ya kamati kwa nia hiyohiyo ya kufanya maboresho makubwa na ninaunga mkono hoja ambazo ziko mbele yetu, ahsante sana. (Makofi)