Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

Hon. Miraji Jumanne Mtaturu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2019

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja katika Kamati hizi mbili ambazo zimewasilisha taarifa zao, nami nipo kwenye Kamati ya Miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mungu ambaye ni mwingi wa rehema kutujalia uzima na kuweza kuendelea kufanya majukumu haya kwa ajili ya Watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru sana Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ambaye kwa hakika mwelekeo na dhamira yake imekuwa inarahisisha sana utendaji wa Serikali. Hii yote ni kwa sababu wananchi wa Tanzania wamekuwa na imani naye na ndiyo maana basi naye amekuwa akifanya kazi hii kama ambavyo wananchi wanatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapongeza kwa namna ambavyo tumeendelea kupata bajeti kwenye hii Wizara yetu ya Ujenzi kwa maana ya kutekeleza majukumu yaliyopo ndani ya Wizara hii. Kama alivyoeleza Mwenyekiti wetu pale asubuhi, ni kwamba tumepata fedha za kutosha kutekeleza miradi mbalimbali ambapo haya mashirika mbalimbali na taasisi yalileta taarifa zao kwenye Kamati yetu na kuona namna ambavyo Serikali iliendelea kuleta fedha. Najua bado kuna changamoto lakini ninaamini zitatatuliwa kulingana na muda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushahidi pekee ni pamoja na maeneo mbalimbali ikiwemo ununuzi wa ndege, ujenzi wa barabara za lami katika nchi yetu, mawasiliano mbalimbali, kwa maana minara inajengwa na hata juzi tumesaidi mkataba kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapeleka minara kwenye vijiji vipatavyo 555 nchi nzima. Yote hiyo ni dhamira ya dhati ya Serikali kuhakikisha kwamba inaboresha mawasiliano na huduma mbalimbali zinazotokana na Wizara yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nitumie nafasi hii kuendelea kumshukuru sana Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Selemani Kakoso pamoja na Makamu wake Mheshimiwa Hawa Mchafu ambao wamekuwa wakiongoza vizuri Kamati hii. Vile vile Wajumbe kwa pamoja tumekuwa tuna ushirikiano mkubwa katika kuhakikisha kwamba tunahoji mambo ya msingi kwa ajili ya maslahi ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu tulipata fursa ya kukutana na taasisi mbalimbali zilizopo chini ya Wizara hii ya Ujenzi, Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Mawaziri wake walituletea wataalam hao na tumeendelea kuhojiana kwenye Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitazungumzia sekta mbili ambazo nilidhani niweze kuzitolea maelezo ndani ya Bunge lako Tukufu. Nianze na wenzetu wa Wakala wa Huduma za Meli. Kama ambavyo tunajua kwamba sisi kijiografia katika ukanda huu tumekaa vizuri sana katika biashara kwa maana ya bandari na tumekuwa tukifanya hivyo kwa miaka mingi na tumekuwa tukipata faida kubwa ya fedha tunapotoa mizigo hapa kwenda kwenye nchi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri inayofanywa, changamoto moja kubwa sana ambayo tumeigundua; tumefanikiwa kukutana na wadau wa sekta hiyo ambao ni wasafirishaji mbalimbali wanaoleta mizigo kupitia bandari yetu, wamekuwa na malalamiko mbalimbali ikiwemo ucheleweshaji wa mizigo yao kutolewa kwenye bandari. Hii imesababisha baadhi ya wafanyabiashara kuhamisha mizigo yao na kushushia kwenye bandari nyingine ikiwemo Beira pamoja na pale Mombasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ukilisikiliza kwenye Kamati tumeenda kwa kina sana. Kwa kweli ni jambo ambalo tusipolifanyia kazi, wafanyabiashara wataondoka wengi wataenda kushushia mizigo eneo ambalo siyo hapa kwetu. Hii itakuwa ni athari kubwa kwenye uchumi wetu; na haya ambayo tunampongeza leo Mheshimiwa Rais na Serikali yake hawawezi kufanya bila kuwa na fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la storage limekuwa ni tatizo kubwa lakini pia kumekuwa na urasimu mkubwa sana katika utoaji wa mizigo. Kuna manung‟uniko makubwa kwa wadau. Tunaiomba Serikali ikakae na wadau iwasikilize na watoe ushauri wao namna ya kuenenda. Wao hawana tatizo na ulipaji, wana tatizo na urasimu mkubwa uliopo ndani ya mamlaka hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivi, tutakuwa tunaitendea haki nchi yetu na kwa hakika tutakuwa tuna uwezo wa kuongeza mapato ya kutosha kwa ajili ya kuwa na uhakika wa kutekeleza miradi ya kimaendeleo ambayo tunayo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wametueleza wenzetu pale kuhusu uchakavu wa bandari nchini. Ni ombi letu kupitia Bunge lako Serikali iende ikaboreshe miundombinu iliyopo kwenye bandari zetu. Najua juhudi zinaendelea, lakini kwa sasa wao wenyewe kama mamlaka walituambia kwamba changamoto kubwa ilikuwa ni uchakavu wa bandari zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ushindani. Chombo hiki kinachosimamia biashara hii ni vizuri ikajua kwamba wenzetu wanafanyaje? Maana leo hii baadhi ya wengine wanaona wanakuwa na comfort kubwa kuwa kwenye bandari nyingine kuliko kwenye bandari yetu ya hapa Dar es Salaam. Tukifanya hivyo, tutakwenda kuongeza nguvu kubwa ya kuvutia wafanyabiashara kushushia mizigo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye sekta moja ya ujenzi ambayo ni wenzetu wa TBA. TBA ni wakala, anafanya kazi nzuri. Lengo la kuanzishwa kwake ilikuwa ni kusaidia eneo la ujenzi katika majengo mbalimbali ya Serikali yaliyopo hapa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumegundua pamoja na juhudi wanazofanya, wenzetu wa TBA wana upungufu mkubwa wa rasilimali watu, hawana wafanyakazi wa kutosha katika kutekeleza miradi yao. Kwa hiyo, ombi letu wahakikishe kwamba wanaongezewa rasilimali watu ili waweze kufanya kazi yao vizuri na lile lengo la kuanzishwa kwao liwe limetimia kwa sababu wanakwenda kufanya kazi ambayo inaenda kusaidia Sekta ya Ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, ni namna ambavyo menejimenti yao, flow ya fedha na vitu kama hivyo nayo imekuwa ni changamoto katika usimamizi. Ombi letu ni kwamba kupitia Kamati tuliishauri na hapa ninaomba niongezee tena kwamba TBA wakiwezeshwa wanaweza kuwa wanafanya kazi nzuri sana na wakaingia kwenye soko la ushindani katika Sekta ya Ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tena kusema kwamba sisi wote ni Watanzania, tuendelee kwa pamoja kuwa kama Taifa moja, tofauti zetu za kimitazamo zisianze kutuingiza kwenye machafuko ambayo hayana sababu. Ninaamini kabisa wote tuna nia njema ya kuwatumikia Watanzania, lakini kila mmoja ana views zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ombi langu ni hilo tu kama ambavyo leo asubuhi tumejadili baadhi ya wenzetu wanapotuchonganisha na Jumuiya za Kimataifa, nadhani inatuweka katika hali ambayo siyo salama sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naomba kuunga hoja mkono kwa asilimia mia moja. Ahsante sana. (Makofi)