Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019

Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kwa Mwaka 2019 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kwa Mwaka 2019

MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja zilizoko mezani. Nitachangia Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa. Na mimi nianze kuchukua fursa kwa kumpongeza sana Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya ya kuzifikia Halmashauri zote 185 kwa maana ya ukaguzi na Taarifa yake ndiyo msingi kwa kazi za Kamati yetu ya LAAC. Nitakuwa na maeneo makubwa mawili tu ya kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ni mfuko wa wanawake, vijana na walemavu. Eneo la pili ni la uhaba mkubwa wa watumishi katika Mamlaka za Halmashauri zetu nchini. Katika eneo ambalo limekuwa likijionesha kama lina udhaifu mkubwa kwenye halmashauri zetu ni madeni ya mfuko wa wanawake, vijana na walemavu. Halmashauri zetu zilikuwa hazipeleki michango hiyo kwa wakati kwa miaka kadhaa iliyopita lakini niipongeze Serikali ilisikia mapendekezo ya Kamati kwa kutengeneza sheria ambayo sasa imeifanya halmashauri zetu kuchangia kwa lazima katika mfuko huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na sheria hii, madeni ya nyuma yalikuwa ni mzigo mkubwa kwa halmashauri zetu lakini pia Kamati iliona ifike na mapendekezo ya kufuta madeni ambayo yalikuwepo kabla ya kutungwa kwa sheria hii mwaka 2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue tena fursa nyingine kuipongeza Serikali kwa kufuta madeni hayo ambayo yalikuwa ni makubwa sana kwa halmashauri zetu. Mwaka 2019, Serikali ilikuja na regulations za jinsi ya kutoa mikopo kwenye vikundi vya akina mama, vijana na walemavu. Moja ya kifungu katika Kanuni hizi inaihitaji vikundi kurejesha baada ya miezi mitatu. Baada ya kuwa wamepata mkopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekutana na changamoto kwenye baadhi ya vikundi ambavyo vimepata mkopo na kushindwa kurejesha baada ya miezi mitatu kwa maana ya kutokana na asili ya biashara ambayo wanakwenda kuifanya. Kanuni hii imezichukulia vikundi vyote kana kwamba vinakwenda kufanya biashara inayofanana. Kwamba watakwenda kupeleka bidhaa sokoni ambazo ziko tayari lakini kumbe kuna vikundi vingine vinakwenda kuwekeza kwenye biashara ambayo inahitaji kuanza kuzalisha baada ya muda mrefu kidogo, pengine miezi sita au mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, nilikutana na kikundi kimoja ambao wao wanakwenda kuwekeza kwenye ulimaji wa matunda na mbogamboga kwa kutumia kitalu nyumba mpaka kupita miezi mitatu ambayo sheria inahitaji waanze kurejesha walkuwa bado wapo kwenye ujenzi wa kitalunyumba na wanahitaji kwa mujibu wa Kanuni hii ya 10 waanze kurejesha mkopo huo. Kwa hiyo, tunaishauri Serikali wakiangalie kifungu hiki, waweze kuvitenga vile vikundi katika ma-group. Vile vikundi ambavyo vinakwenda kufanya biashara straight away viwe na muda wake na vile ambavyo vina uwekezaji wa m uda mrefu viangaliwe ni kipindi gani vianze kurejesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine sheria hii inahitaji halmashauri ziendelee kuchangia kipindi chote indefinitely na lengo ni kutengeneza mfuko ambao utakuwa ni revolving. Ziko halmashauri zetu zingine zina makusanyo makubwa sana ya ndani, kuzifanya zichangie asilimia 10 kwenye mfuko huu kunatengeneza fedha nyingi sana ambazi zitakuwa zinaweza zikalea matumizi mabaya baadaye. Kwa hiyo, tulikuwa tunashauri Serikali iangalie namna ya kujenga mfuko huu. Iweke labda miaka mitano halmashauri zichangie hizo asilimia 10 kufikia labda miaka mitano, halmashari hizi ambazo zina mapato makubwa zinakuwa zimeshatengenza mfuko mkubwa ambao unaweza kujiendesha. Baada ya hapo hizo asilimia 10 zielekezwe kwenye matumizi mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo nilihitaji kuchangia ambalo pia limejionesha kwa kiasi kikubwa kwenye vitabu vya Halmashauri zetu ni uhaba mkubwa sana wa watumishi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Wakati fulani tunajiuliza kama halmashauri hizi zinaweza kuendeshwa kwa uhaba huo mkubwa wa watumishi, kwa mfano kule kwenye halmashauri yangu ya Wilaya ya Mbinga tuna uhaba wa walimu wa shule ya msingi wapatao 971 lakini watumishi Sekta ya Afya ni zaidi ya 400, huo ni uhaba. Wakati fulani tunajiuliza ni lini Serikali iliamua kufanya utafiti wa kiwango cha huduma ambazo zinatolewa kwa uhaba huo wa watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda wakati fulani Serikali ijiulize kama Serikali za Mitaa zinaweza kujiendesha kukiwa na uhaba huu mkubwa wa watumishi, hizo ikama zilitengenezwa kwa uhalisia wa mahitaji ya hizo Halmashauri zetu? Labda hiyo inaweza ikatuletea ufafanuzi kwamba hayo ma-gap ya watumishi ni halisia au ni hesabu tu ambazo zilitengenezwa bila kuzingatia uhalisia.

Mheshimiwa Naibu Spika, uhaba huo unasababisha nafasi nyingi pia za Wakuu wa Idara kukaimiwa. Katika Taarifa za CAG zilizopita zinaonekana kwamba kuna madeni makubwa ya watumishi waliokuwa wanakaimu kwenye nafasi mbalimbali, unaweza kukurta mtumishi anadai mpaka milioni 50. Halmashauri moja inadaiwa milioni 400, 500 kutokana na posho za kukaimu nafasi mbalimbali za Ukuu wa Idara. Kwa hiyo, tunaishauri Serikali ifanye upekuzi mapema ili kuondokana na madeni ambayo si ya lazima wakati mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine hili la uhaba wa watumishi kwa mfano kule kwenye Halmashauri yetu ya Mbinga umefanya majengo mengi ambayo yamekamilika ya zahanati yasiweze kufunguliwa kwa wakati ni kutokana na uhaba wa watumishi wa Idara ya Afya kwa mfano zahanati ya Lukiti ambayo imepewa jina la Martin Mtonda Msuha haijafunguliwa kwa sababu ya uhaba wa watumishi. Zahanati ya kijiji cha Longa, zahanati ya Matuta na Kijiji na Ruanda. Zahanati hizi zote zimekamilika lakini hakuna watumishi wa kwenda kuanza kutoa huduma katika maeneo hayo. Kwa hiyo, nguvu za Serikali na za wananchi zimebaki hazitumiki ipasavyo kwa sababu ya kutosa watumishi wanaohitajika wa Idara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la mwisho kwa sababu muda bado ninao, nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kuona kuwa ukusanyaji wa mapato ya ndani umekuwa ni changamoto kwa Halmashauri zetu na hivyo basi kutokana na hamashauri zetu kutokukusanya mapato ya kutosheleza matumizi yao imesababisha halmashauri nyingi kubadilisha matumizi. Halmashauri nyingi zimekuwa zikikopa kutoka kwenye akaunti ya amana ili kukidhi mahitaji yake ya ndani. Jambo hili limesababishwa na kutoweza kukusanya mapato yao ya ndani kikamilifu. Niipongeze Serikali imeliona hili, juzi hapa wamegawa mashine za kukusanyia mapato zipatazo 7,229 ambazo zimesambazwa nchi nzima kwenye Halmashauri yetu. Ni imani yetu sasa mashine hizi zitasimamiwa vizuri na TAMISEMI kwa maana ya kwamba zile controls walizoweka ili wale watumishi wasiwe wanachezea tena zile mashine kuziweka offline wakati wakiwa wanaendelea na makusanyo itafanyika hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini uhaba huu wa fedha za ndani umesababisha pia madeni makubwa sana kwa madiwani wetu. Madiwani wetu hawajalipwa posho kwa muda miezi mingi karibu Halmashauri nyingi nchini. Kwa hiyo, naishauri pia Serikali iangalie namna ya kufanya uchambuzi wa madeni ambayo madiwani wetu wanadai tunavyoeleka kukamilisha miaka mitano ya kipindi chetu cha utawala.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa lakini pia Kamati ya PAC. Ahsante sana. (Makofi)