Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Hamida Mohamedi Abdallah

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia. Nianze kwa kumpa pole Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi ndugu yetu Engineer Stella Manyanya kwa msiba ambao ameupata.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nichangie hotuba hii ya Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi. Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba hii ni nzuri, ina mikakati mizuri, yenye utekelezaji wake kwa kipindi hiki tunachokitarajia.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona mambo mengi, mafanikio mengi katika upande huu wa elimu. Tumejenga shule nyingi za msingi, shule za Sekondari, shule za ufundi VETA, Vyuo vikuu lakini uwepo wa vyuo vikuu huria katika Mikoa yetu. Vyuo vikuu hivi vilivyopo katika mikoa yetu kwa kiasi kikubwa vimeweza kuwasaidia vijana wengi, watumishi wengi, kuingia katika kujiendeleza na elimu hii ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mafanikio haya tuliyoyapata, lakini kuna changamoto mbalimbali katika miundombinu ya elimu. Waheshimiwa Wabunge wengi sana jana wamechangia katika changamoto mbalimbali zilizopo katika eneo hili la elimu. Pamoja na kutokuwepo kwa Walimu wa kutosha lakini vitendea kazi tumeona ni changamoto kubwa. Tumefanya jitihada kubwa sana katika kuhakikisha shule zetu za sekondari zinakuwa na maabara katika kila eneo.
Mheshimiwa Naibu Spika, shule hizi zilijengwa kwa changamoto kubwa sana na kwa agizo la Mheshimiwa Rais Mstaafu wa Awamu iliyopita. Hata hivyo, tumeona maabara hizi zimeendelea kubaki hivi hivi, hazina hata samani ndani ya vyumba vile, matokeo yake vyumba vile vimeendelea kukaa hivi hivi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lengo letu kubwa ni watoto wetu wapate masomo kwa nadharia, lakini kwa vitendo pia. Kwa hiyo, ningependa Mheshimiwa Waziri atakavyofanya majumuisho yake hapa leo, atuambie ni mkakati gani ambao ameuandaa katika kuhakikisha maabara zetu tulizozijenga zinafanya kazi kama ambavyo tumetarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina imani kubwa sana na Serikali ya Awamu ya Tano yenye kauli mbiu ya Hapa Kazi Tu. Tumeona jinsi ambavyo Mheshimiwa Rais wetu anavyotekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa kuanza kutoa elimu bure kuanzia shule ya awali, shule ya msingi na shule ya sekondari. Vile vile tumeona jitihada kubwa anayofanya katika kutatua kero hii ya madawati na madawati haya yatakuja katika Majimbo yetu. Tunamwombea kila la heri Mheshimiwa Rais wetu, aendelee na jitihada ambazo anazifanya lakini aendelee kutuongoza Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona katika shule hizi za ufundi, shule za VETA. Sera ya Elimu ilisema kujengwa shule za VETA katika kila Wilaya. Nashukuru katika Mkoa wetu wa Lindi, Lindi Manispaa tunayo shule hii ya VETA, lakini kutokana na sera hii ya ujenzi wa shule hizi za VETA kila Wilaya hatujafanikiwa kwa kiwango ambacho tumekitarajia. Wilaya nyingi zimekosa kuwa na vyuo hivi vya VETA. Kwa hiyo, hii inawafanya vijana wetu wengi wanaomaliza darasa la saba, wanaomaliza form four ambao wamefeli kushindwa kuendelea na shule hizi za ufundi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, zamani tulikuwa na shule za ufundi katika shule zetu za msingi hasa pale kwetu katika Mkoa wa Lindi, tulikuwa na shule za msingi ambazo zina shule za ufundi, lakini baada ya sera hii ya kujenga vyuo katika kila Wilaya. shule zile za ufundi zilifungwa. Tunapata shida sana kwa sababu shule hizi za VETA hazipo katika kila Wilaya, matokeo yake vijana wetu wanaofeli darasa la sababu, wanashindwa kujiendeleza. Shule zile zilikuwa zinasaidia sana katika kuwafanya vijana wetu wanapata fani mbalimbali na hatimaye wanaweza kujiajiri wenyewe.
Mheshimwa Naibu Spika, napenda kumwomba Mheshimiwa Waziri kwamba, shule zile ambazo zilikuwa na shule za ufundi, basi ziweze kuendelea na shule hizo za ufundi ili watoto wetu watakapomaliza darasa la saba na kufeli, basi waendelee kupata elimu hii ya ufundi na hatimaye waweze kujiajiri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Lindi na Mtwara kielimu kwa muda mrefu tuko nyuma sana. Hii imechangiwa na mambo mbalimbali nitasema jambo moja tu ambalo lilisababisha kuwa nyuma kielimu katika Mikoa hii miwili ya Lindi na Mtwara. Katika harakati za ukombozi wa nchi za Afrika, maeneo ya Mkoa wa Lindi na Mtwara, yalikuwa ni maeneo ya mafunzo ya kivita kwa ajili ya maandalizi ya ukombozi huu wa nchi za Afrika. Kulikuwa na makambi ya South Afrika ya Nelson Mandela, kulikuwa na makambi ya Msumbiji ya Samora Mashelu, lakini kulikuwa na makambi ya nchi za Zimbabwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mikoa hii ya Lindi na Mtwara lilikuwa ni eneo linaloitwa danger zone, kwa hiyo, kwa kweli Serikali haikuweza kujenga shule kama ambavyo tulitarajia na kufanya watoto wa mikoa hii miwili waweze kuwa nyuma kielimu. Kwa hiyo, naiomba Serikali, pamoja na jitihada hizi kubwa tulizozifanya za kujenga shule za sekondari kila Kata, lakini tuna changamoto kubwa sana ya ukosefu wa Walimu katika shule zetu. Suala la Walimu kila Mbunge aliyesimama amelizungumzia, pamoja na kuwa na maslahi duni, lakini tumekuwa na ukosefu mkubwa sana wa Walimu hasa Walimu wa sayansi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wetu wa Lindi, mahitaji ya Walimu wa sayansi yalikuwa 726, lakini waliopo ni 262 na pungufu ni 464. Upungufu huu ni mkubwa sana, maana hata nusu ya mahitaji yetu kwa walimu hatukupata. Kwa kweli Serikali haijatutendea haki maana tutaendelea kuwa nyuma mwaka hadi mwaka kwa kiwango hiki cha Walimu tuliowapata.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri wa Elimu atutazame kwa jicho la huruma sana katika Mkoa wa Lindi kuhakikisha tunaongezewa idadi ya Walimu hii hasa wa sayansi ili watoto wetu waendelee kupata elimu iliyo bora kwa kipindi hiki tunachokitarajia.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la maslahi ya walimu limeongelewa karibu na Wabunge wote waliozungumza tangu jana hadi leo, lakini mafao ya Walimu wastaafu pia yamekuwa ni tatizo, kwa hiyo naiomba Serikali yangu sikivu, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kuwaangalia Walimu hao wastaafu…
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana.