Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Namshukuru Mwenyezi Mungu kupata fursa hii kuchangia Mpango huu wa Maendeleo wa mwaka 2020/ 2021. Kwanza kabisa niipongeze Serikali yangu ya Awamu ya Tano inayoongozwa na jemedari wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa mambo makubwa ambayo kipindi cha miaka minne tu tunaona mambo yamefanyika makubwa sana sina haja ya kuyataja wenzangu wameyataja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende ukurasa wa 23 wa Mpango kwa maana ya mapitio ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo. Nizungumzie kidogo eneo la kilimo, niwapongeze sana Bodi ya Korosho kwa maana ndani ya Wizara ya Kilimo, wanajitahidi sana sana kusambaza mbegu, madawa pamoja na utaalam wote unaohusika katika uzalishaji wa korosho. Sisi Manyoni ni wachanga lakini wanaendelea kutusaidia sana lakini na maeneo mengine ambayo hasa wanalima korosho. Bado tatizo liko kwenye mazao mengine, nikizungumzia Mkoa wangu wa Singida sisi tunajulikana kwa kilimo cha alizeti kwa hiyo ni mkoa ambao ni giant kwa uzalishaji wa alizeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri sana Wizara ya Kilimo inapotokea kwamba mkoa ule ambao ni hasa chief producer wa zao fulani wapeleke nguvu basi kwenye mkoa huo, hasa kwenye mbegu, masoko tuna tatizo kubwa sana. Singida tunalia sana suala la mbegu sana tu tunachanganywa sana upande wa mbegu, kuna mbegu sijui zinaitwa Hyssun lakini bei ni kubwa sana zinauzwa kilo moja Sh.35,000, nilizungumza hata kipindi kilichopita. Kwa mkulima wa kawaida ambao tunategemea hawezi kumudu gharama hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye sekta ya elimu kwenye mapitio haya haya. Nijikite zaidi kwenye ukarabati wa shule kongwe za sekondari. Naipongeza sana Serikali yangu ya Awamu ya Tano imezikumbuka shule hizi zilikuwa zimeathirika sana lakini sasa ukienda kwenye shule nyingi hizi 87 zote zingine tayari ukarabati umeshakamilika, zingine ziko kwenye hatua za mwisho, naipongeza sana Serikali imefanya jambo kubwa sana pamoja na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vitu tu niongezee kidogo hapo, tunazo changamoto ndogo, kuna hawa jamaa wakala wa majengo ya Serikali TBA wanapewa tenda hizi za ukarabati za ujenzi, nadhani wajipange kwanza. Tusiwape tenda tena hapa kwa sababu wametuvurugia maeneo mengi sana kwenye ukarabati na kwenye ujenzi, wajipange vizuri, kwa sababu ni shirika la Serikali wanatuaibisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine niliyoiona kwenye maeneo haya, kwa mfano kwenye shule kongwe hizi, naomba sana shule hizi zinavamiwa Serikali ijitahidi kutenga fedha pia kupima maeneo haya, ni fedha ndogo tu. Kwa sababu tunao surveyors kwenye mikoa huko na halmashauri tuwatumie hao hao, wapime watoe hati na kuweka pia hata wigo ili lisivamiwe shule hizi. Tulipita siku moja shule ya Sekondari ya Mirambo kule hali ni mbaya sana uvamizi yaani usiku wanapita watu yaani ni vurumuai, hakuna utulivu wa masomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa Mpango wenyewe ambao unatarajiwa twende ukurasa wa 66,snizungumzie kidogo suala la misitu na nyuki. Profesa mmoja anaitwa Dos Santos Silayo anasema ingeigharimu dunia trilioni 38 dola za Kimarekani kutengeneza oxygen ambayo ingewa-supply na kuwafaa binadamu kwa miezi sita kwa dunia nzima, ni gharama kubwa sana. Trilioni 38 karibu trilioni 40 USD dola kutengeneza oxygen, suppose kama miti ingekuwa haipo kwamba sasa oxygen inatengenezwa ni trilioni karibu 40 kwa miezi sita tu tena kwa binadamu tu sio wanyama wengine, fikiria hiyo gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna Dokta mmoja anaitwa Anne Marie anasema kuwa mtu mmoja huhitaji miti hai saba hadi nane imtolee oxygen kwa mwaka mzima. Nataka kuzungumzia umuhimu wa kutunza misitu yetu siyo oxygen tu na vyanzo vya maji. Manyoni kule sisi tuna Mto mmoja unaitwa Kizigo ambao unaungana na mito 18 ambayo inapeleka kwenye lile bwawa la Mwalimu Nyerere kule Rufiji. Sasa mazingira haya yanaanza kuharibiwa, Sheria ya Misitu, Na.14 ya mwaka 2002 na regulations zake za mwaka 2005 zinatoa asilimia 52 kwenye zile categories, maana kuna categories zimetajwa pale kwamba kuna misitu ya watu binafsi, kuna misitu ya vikundi, kuna misitu ya vijiji, kuna misitu ya Serikali Kuu, kuna misitu ya Serikali za Mitaa na kuna general land. Sasa misitu ya vijiji inachukua asilimia 52 kwenye sheria hii ina-provide na tunawaachia wanavijiji ndio watunze misitu hiyo. Hii ni hatari, wame-prove failure, misitu mingi inateketea kupitia kwenye vijiji, tuiangalie sheria hii upya vinginevyo tutajikuta tuna jangwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kwa sababu hawa wanavijiji hawana elimu yoyote, unamkabidhi asilimia 52 ya misitu yote ya nchi nzima, hapana. Mheshimiwa Dkt. Mpango kwenye vipaumbele waliangalie upya hili la misitu, sheria hii tuibadilishe, tujaribu kuangalia makundi mengine, nadhani Serikali Kuu iwe na dhamana ya kutunza misitu hii, hawa waombe tu kibali kwa sababu ni watumiaji washirikishwe, lakini waombe kibali ila mwangalizi awe Serikali Kuu na sheria iseme hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie tu kwa kusema kwamba Serikali ya Awamu ya Tano inakwenda vizuri naona kampeni kubwa kwenye uchaguzi ni kufanya kazi. Kwa hiyo kampeni kubwa ya Chama cha Mapinduzi imeshafanyika, tunasubiri tu tarehe 24 vijana wachukue nafasi zao, 2020 Mheshimiwa Rais na Serikali yake na Wabunge wa Chama cha Mapinduzi tuchukue nafasi zetu kwa sababu tayari kampeni zimeshafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru sana na naunga mkono Mpango huu ni mzuri sana. (Makofi)