Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii ya Elimu. Kwanza kabisa, naomba ni-declare interest kwamba na mimi ni mmiliki wa shule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, makubwa niliyonayo hapa ni ushauri. Kwa sababu muda wenyewe ni kidogo sana, nikimbie na mwendo wa ushauri. Kwanza kabisa, namshauri Mheshimiwa Waziri, pale Wizarani liko tatizo la watu kujifanyia kutoa maamuzi. Wanatoa maamuzi hata bila kuangalia maamuzi haya yana madhara gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sasa hivi tunajadili suala la ada elekezi. Ada elekezi ukijaribu kufanya utafiti, hayuko hata mtu mmoja anayelalamika, lakini watu wa Wizara wameamua tu kuandika elekezi, wanachanganya vichwa vya watu, Watanzania wanababaika na kuona kwamba kuna hoja ya ada elekezi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba suala hili la ada elekezi Mheshimiwa Waziri alitolee ufafanuzi, Watanzania wajue kwamba ada elekezi unataka kumwelekeza nani? Aliyekwambia umpeleke mtoto shule huko ni nani? Kwani shule ya Serikali iko wapi? Shule ya Umma ipo, mtoto apelekwe akasome. Kama ukipeleka shule ya private maana yake umehiari mwenyewe. Utakayokutana nayo huko, acha yakukute. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, uko mtazamo pale Wizarani kwamba watu wanaamua tu mambo. Kwa hiyo, naomba usimamie utaratibu. Wewe mama nakufahamu, ni mtaalam, unajua jinsi ya kusimamia mambo. Simamia utaratibu watu wafuate utaratibu wa kuandika na kutoa maelekezo ili kusudi tuonekane kabisa kwamba private sector inayotoa elimu ni wadau wa Serikali na Serikali iwe tayari kuwasaidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni ufaulu hafifu katika shule za Umma. Naomba Serikali ijitahidi kwa sababu leo hii tunaswaga hawa watoto wanaendelea kusoma, lakini tukumbuke, Mheshimiwa Waziri wewe ni mtaalam unafahamu, asubuhi umesema kabisa kwamba unasimama ukijiamini kwamba wewe ni msomi na umesoma katika elimu iliyo bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hawa watoto tunaowaswaga leo waende wamalize Kidato cha Nne kwa kuongeza idadi tu, tukumbuke kwamba itafika siku hawa watakuwa watawala. Watoto hawa ndio watakaokuwa Mawaziri, Marais na Wabunge. Hebu tujiulize, Taifa hili litakuwaje? Tutaanza kulalamika huduma hospitalini ni mbovu, huduma kila mahali ni mbovu kwa sababu tu watoto ambao tunawaswaga waende ili tujaze madarasa na wamalize Form Four watakuwa hawajapata elimu iliyo bora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, liko suala la VETA. Kwenye hotuba nimejaribu kupitia na kuangalia, wamejaribu kulieleza, lakini najiuliza, hivi Waheshimiwa Wabunge, nani Mbunge yumo humu ndani mtoto wake anasoma VETA? Maana tunang‟ang‟ania ooh, tuanzishe VETA watu wakasome VETA! VETA tulizonazo hazina ubora.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni fundi, nafahamu fika taaluma inayotolewa kule VETA, tunaamini kuna ufundi, lakini hakuna ufundi wowote wa maana unaotolewa. VETA hawana vifaa, hawana machines; kama wanazo ni za kizamani mno! Tumejenga Vyuo hatukarabati, sasa leo tunataka watoto waende VETA, wakawe mafundi wa nani? Wafanye kazi ya nani? Naomba sana Serikali iangalie kwamba tunahitaji VETA sawa, lakini ziwe ni VETA zenye ubora. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza VETA, watoto hawa wapewe mitaji ya kuanzia ufundi wao huko mitaani. Vile vile lazima tutambue, unapokuwa na Chuo cha VETA, ni vizuri ukawa na kituo kinachoweza kuwa na mitambo kwa ajili ya kusaidia watoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe unamfundisha mtu kushona nguo, halafu unataka akate na mkasi wa mkono, ataendelea saa ngapi? Mafundi wangapi wameendelea mpaka leo? Tuwe tunafanya na utafiti! Kama tunataka watu wawe mafundi wa kushona, tuhakikishe kwamba tuna viwanda vikubwa vya ushonaji ambavyo kazi yake ni kukata nguo wale wachukue wakaunganishe. Sasa wewe unataka mtu akate nguo ile ashone, haiwezekani kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ada elekezi…
MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.