Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. FELISTER A BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa siku ya leo na nikupongeze kwa kusimamia Bunge hili vizuri kwa siku ya leo. Nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Mpango na Naibu wake, mdogo wangu Mheshimiwa Dkt. Ashatu kwa kazi nzuri sana wanayoifanya katika Wizara hii ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa sina fadhila kama sitaishukuru sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa mambo mazuri ambayo yanafanywa katika Mkoa wetu wa Dodoma baada ya Serikali kuhamia Dodoma. Tunaona sasa kuna mipango mikubwa ambayo imewekwa kwa ajili ya kuendeleza Mji wa Dodoma, mashirika mbalimbali yameanza kujengwa na watumishi wameshahamia Dodoma. Kwa hiyo niipongeze sana Serikali ya Awamu ya Tano, lakini zaidi ya yote niwapongeze kwa kuamua kutumia force account, kupunguza gharama kubwa ya ujenzi iliyokuwa inatumika siku za nyuma, majengo au vituo vya afya ambavyo vilikuwa vinajengwa takribani kwa Sh.1,000,000,000 sasa tunajenga kwa Sh.500,000,000. Ni jambo la kuipongeza sana Serikali na tunaona kwa kutumia force account tumeweza kujenga majengo mengi na tumeweza kujenga vituo vya afya vingi na niombe Serikali iendelee kutumia force account katika majengo yake, lakini hata kwa mambo mbalimbali ambayo kwa mipango mbalimbali ya ujenzi tunaona jinsi tulivyopunguza gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali kwamba, kwa sasa Serikali imeagiza kwamba malipo yote yalipwe na kila biashara inayofanyika mwananchi au taasisi yoyote ipate risiti ya elektroniki, lakini naona Serikali inapata sana hasara kwa taasisi aidha za umma au za binafsi na hata baadhi ya maduka makubwa na hata wafanyabiashara, wengine bado wanafanya biashara pasipo na kutoa risiti ya elektroniki, kwa hiyo mapato mengi yanavuja kupitia njia hiyo. Nadhani udhibiti ukiwekwa madhubuti na bado kuna baadhi ya maduka au baadhi ya wafanyabiashara wanakuuliza unataka risiti ya eleketroniki na anakwambia ukitaka risiti ya elektroniki bei ni hii na ukitaka risiti iliyoandikwa kwa mkono bei ni hii na hata vituo vya mafuta usipoangalia risiti yako uliyopewa unaweza ukakuta risiti uliyopewa siyo ya mafuta uliyojaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi tunachukua risiti hizo bila kuangalia fedha uliyolipa, ni sawa na lita ulizopata, kwa hiyo bado kuna loophole sana katika matumizi ya risiti za elektroniki. Nimwombe Mheshimiwa Waziri au niombe sana Serikali yangu sikivu iangalie namna ya kusimamia matumizi ya risiti ya elektroniki. Nchi zingine ukienda huwezi kununua kitu bila kupata risiti iliyo sahihi, lakini Watanzania bado tunakwepa malipo kwa kutumia risiti za elektroniki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze pia Serikali kwa kuanzisha miradi ya mikakati reli ya kati, viwanja vya ndege na ununuzi wa ndege na hata mitambo ya kufua umeme kule Julius Nyerere, kule Rufiji. Ni miradi mikubwa ambayo Watanzania hatukuwaza kuwa nayo leo, hatukuwaza hayo lakini Awamu ya Tano imeleta mambo makubwa hayo kwa Watanzania, itafika muda tukitoka Dar es Salaam tutafika Dodoma baada ya masaa mawili na reli hii itakuwa na faida zaidi kama itabeba mazao ya wakulima katika maeneo mbalimbali itakapopita reli hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali kwamba bandari kavu ipo Dodoma na mizigo mingi itachukuliwa Dodoma. Hata hivyo, mizigo hii reli itapata nafasi kama mazao ya wakulima yatakuwepo na iwe wakati sasa wa Benki ya Kilimo inafanya kazi Dar es Salaam na kama ina matawi sio nchi nzima lakini wakulima wamesambaa nchi nzima. Umesikia Waheshimiwa Wabunge wengi wanazungumza habari ya kilimo, kwa sababu wanaishi na wakulima na 65% karibu 70% ya Watanzania ni wakulima. Kwa hiyo tunaposema habari ya kilimo tuna maana na tunajua sababu ya kuzungumzia habari ya kilimo, kwa hiyo Benki ya Kilimo haijafanya kazi yake inavyotakiwa na kwa sababu ina matawi ambayo hayakusambaa nchi nzima bado ni vigumu kupata mikopo kupitia Benki ya Kilimo na wanaopata mikopo hiyo ni wale wanaoelewa na ni wachache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Benki ya Kilimo ukauliza ni wakulima wangapi wa Dodoma wameweza kukopa, ni wachache mno, sio kwamba hawataki wanataka, lakini kutoka hapa kwenda Dar es Salaam na kulala kwa ajili ya kutafuta mkopo ni kazi na kama tunalo tawi Dodoma, Singida hawana na kama tunalo tawi Dodoma Iringa hawana tawi, Babati hawana tawi, kwa hiyo tuone namna ya kuwaunganisha wakulima wa kati na wakulima wadogo kupata mikopo kupitia Benki ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tukipata mikopo tutaweza kununua pembejeo, tunatamani kulima kwa hali ya juu sana, lakini tunalimaje tunapata mikopo wapi, tunanunuaje pembejeo, ukisema ununue trekta sio chini ya 50,000,000. Kwa hiyo, sasa ni wakati wa Benki ya Kilimo kusambaa katika mikoa yetu na wakulima wakafaidi matunda ya kuwa na sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nizungumzie Sekta ya Mifugo. Tumejaliwa kuwa mifugo Tanzania na Tanzania yetu ni nchi ya tatu Afrika kuwa na mifugo, lakini bado hatujaweza kuwa na viwanda vya kutosha kuchakata mazao ya mifugo. Nakumbuka Bunge lililopita niliuliza swali kuhusu viwanda vyetu vya kuchakata mazao ya mifugo na Mheshimiwa Waziri akaniambia kwamba wana utaratibu wa kuingia ubia na kiwanda kile kilichoko Pwani nadhani, kilichoko Ruvu, lakini michakato hii bado inaendelea. Kiwanda kimoja tu tusikitegemee pamoja na kwamba kuna viwanda vya watu binafsi, tungeweka utaratibu kwamba hata ranch zetu kama ni ranch moja au kama ni ranch mbili tuna ranch nyingi Tanzania, tukaweka ranch moja au mbili au tatu kama mfano, wakaanzisha viwanda au kiwanda kwa ajili ya kuchakata mazao ya mifugo ili Watanzania wapate masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachogomba hapa ni soko, hata ukirudi kwenye mazao watu wa korosho wanalia, watu wa pamba wanalia, tumbaku wanasema, kahawa wanasema, wakulima wa mbaazi wanatafuta soko, sisi wa zabibu ndio hatuna kabisa soko. Kwa hiyo tatizo lililopo ambalo naliona ni masoko, mazao tunayauza wapi, lakini hata mazao ya mifugo tunauza wapi, tuna ASASI Iringa, lakini tuna kiwanda kingine cha maziwa Tanga lakini hapa katikati Dodoma tuna kiwanda gani pamoja na kwamba tuna ranch, nyama tuuzie wapi. Nakumbuka walinifuata vijana wa UDOM hapa, wanataka kuuza nyama nje, lakini namna ya kusafirisha nyama hiyo ifike huko kwanza hawana mtaji, lakini la pili wanafanyaje. Kwa hiyo tungekuwa na kiwanda chetu Tanzania cha kuchakata ngozi nyama maziwa viwanda vya kutosha nafikiri wasingehangaika.

MWENYEKITI: Ahsante sana

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo kengele ya kwanza.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa kengele ya pili imelia Mheshimiwa Felister, ahsante sana nashukuru

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)