Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia Mpango wetu wa Maendeleo pamoja na mwongozo wa bajeti kwa mwaka 2020/21.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na timu nzima ya Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri wanayoifanya. Ukisoma utekelezaji katika ripoti hii, utaona katika maeneo mengi, kwa kweli wamefanya vizuri sana kuliko vile tulivyotarajia na pia hata kwa kutulingalisha na nchi jirani. Kwenye Pato la Taifa, urari wa biashara na kwenye fedha zetu za kigeni tunafanya vizuri. Vilevile ukiangalia hali ya chakula, ndiyo sasa hivi inaonyesha maeneo mengi kuna tatizo lakini kuna maeneo mengi ambayo yana chakula cha ziada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niendeleze tu kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake lakini pia yote haya yanatokana na kazi nzuri anayoifanya Mheshimiwa Rais wetu mpendwa, tunamshukuru sana kwa kazi nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia haya mapendekezo ya mpango utaona kwa kiasi kikubwa yamelenga kukua kwa uchumi katika Sekta ambazo hazitoi ajira kwa Watanzaia walio wengi ambao ni wakulima. Ripoti inaonesha kuwa sekta ya kilimo inaajiri zaidi ya 65% ya Watanzania, lakini inachangia 28% tu na ukuaji wake ni wastani wa 6%. Sasa ukiangalia katika hali ya namna hiyo ina maana Watanzania walio wengi hawashiriki katika kuchangia kukua kwa uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pendekezo langu kwa Mheshimiwa Waziri aangalie ni kwa jinsi gani uwekezaji kwenye sekta ya kilimo uongezeke. Uwekezaji kwenye sekta ya kilimo ningependekeza nchi yetu ya Tanzania imejaliwa ardhi nzuri sana maeneo mengi lakini kuna upungufu wa mvua na mvua zikija zinanyesha nyingi kunakuwa na mafuriko. Ningependekeza huu mpango pamoja na bajeti uangalie kuongeza sekta ya umwagiliaji na ujenzi wa mabwawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hilo kwa makusudi kwa sababu nchi nyingi zinazotuzunguka, majirani zetu wanategemea zaidi kilimo cha umwagiliaji na sisi Tanzania ndio tuna maji mengi hapa kwetu Afrika hata duniani sisi tulijaliwa, Mwenyezi Mungu ametupa akiba kubwa sana ya maji lakini hayo maji tumekuwa hatuyatumii. Namwomba Mheshimiwa Waziri pamoja na Serikali waangalie namna gani washiriki katika kukuza na kuboresha sekta ya umwagiliaji pamoja na ujenzi wa mabwawa ambayo yatasaidia kwa ajili ya binadamu na pia kwa ajili ya mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizalisha vilevile utahitaji ni namna gani upate masoko ya hayo mazao. Masoko ya mazao yetu kwa kweli hayako katika hali nzuri. Ukitulinganisha sisi na nchi jirani uchukulie zao kama la kahawa, zao la kahawa sisi tuna soko letu ambalo tunatumia minada inayoendeshwa na Bodi ya Kahawa, lakini hii kahawa kwa mfano kahawa ya arabika ambayo na nchi ya Kenya, Ethiopia na Rwanda wanailima, bei ya kahawa kwa hapa kwetu ni shilingi dola 100 kwa mfuko wa kilo 50 lakini wenzetu Kenya ni zaidi ya kilo Dola 250, wenzetu Ethiopia ni zaidi ya hapo. Sasa angalia kwa nini Tanzania sisi tupate bei ndogo, tukipata bei ndogo ina maana vilevile inaathiri ukuaji wa uchumi wetu kwenye sekta ya kilimo na hizi ndio pesa tunazozihitaji kwa ajili ya kuboresha urari na vilevile pesa tunazozihitaji kwa ajili ya kuboresha mapato ya nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia pendekezo langu ni namna gani tuimarishe maghala ya kisasa, mazao yetu mengi tunayoyazalisha yanaharibika, kunakuwa na uharibifu mkubwa wa wadudu. Ningependekeza uwekezaji vilevile uende kwenye maghala ya kisasa na biashara ya masoko sasa hivi inaendana pamoja na maghala ya kisasa. Ukiwa na warehouse receipt system ambayo inafanya kazi ndio soko la bidhaa linaweza kufanya kazi, kukiwa na soko la bidhaa bila warehouse receipt system hilo soko la bidhaa haliwezi kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa mazao yetu sasa hivi tukitaka tufanye vizuri katika mazao yote ya nafaka na mazao ambayo tulizoea kuita ni mazao ya biashara inabidi tuimarishe soko la bidhaa TMX ili lifanye kazi yake vizuri na ili lifanye kazi vizuri hili linahitaji kuwe na maghala, kuwe na warehouses ambazo zitatusaidia. Kwa sasa hivi bila hivyo hili soko letu haliwezi kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye kilimo kunahitaji miundombinu ambayo ni mizuri. Miundombinu yetu huko vijijini haiko vizuri, barabara haziko vizuri, ziko katika hali mbaya sana na hawa wanaozihudumia hizo barabara bajeti wanayopewa ni kidogo sana. Sasa napendekeza, ili tuboreshe kilimo, ili tuboreshe barabara miundombinu ya vijijini, hawa TARURA wangeongezewa bajeti katika mwaka unaokuja ili waweze kuboresha miundombinu ya barabara za vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika miundombinu ukiangalia reli, naishukuru kwanza Serikali kwa ujenzi wa SGR, SGR katika awamu hizi mbili inaonesha itafika Makutupora, lakini kuwe na mpango mahususi ambao unaonesha ni lini hiyo reli itafika katika matawi yake ya Mwanza na tawi la Kigoma. Bila hivyo kazi itakuwa kubwa sana ya mizigo yetu ambayo sasa hivi inasafirishwa kwa barabara na kuna uharibifu mkubwa sana wa barabara zetu, bila kumalizia SGR mpaka Mwanza, mpaka Kigoma bado tutakuwa hatujafikisha lengo la matumizi mazuri ya hii reli ya kisasa ya SGR na hii itasaidia vilevile utendaji mzuri wa Bandari yetu ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii reli nayo inahitaji iwe na matawi; kuwe na tawi la kuunganisha na TAZARA kwa upande wa Tunduma kuwa na reli ya kutoka Tunduma mpaka Ziwa Tanganyika lakini vilevile katika mpango imeonesha kuwe na reli ya kuanzia ra mpaka Mbambabay. Hii reli itakuwa na manufaa zaidi vilevile, kukiwa na kipande kingine cha reli kitakachotoka Mbeya ambacho kinaunganishwa na TAZARA kinakuja mpaka Itungi Port au Kiwila Port kwenye Ziwa Nyasa. Hapa utakuwa umekamilisha network yote ya reli zetu zitakuwa zimeunganishwa vizuri na kwa sababu ukiangalia tunapojenga SGR huku na reli ya TAZARA vilevile ni iko kwenye standard ya SGR, kwa hiyo utakuwa umeiunganisha Tanzania vizuri kwa kuwa na reli za kisasa na itatusaidia hata katika kuimarisha biashara ya sisi na nchi za jirani yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna matumizi bora ya ardhi; matumizi bora ya ardhi ni muhimu sana katika kuendeleza kilimo, lakini vilevile ni muhimu sana katika ufugaji, lakini ni muhimu vilevile katika makazi. Ardhi yetu, maeneo mengi ya mijini hayajapimwa, kwa hiyo miji iko holela, sasa na kwa vijiji vinavyoizunguka hii miji, vingi sasa kutokana na miji imejaa watu wanahamia huku vijijini na wanahamia kwa ujenzi holela, kwa hiyo huu mpango ungeonesha ni namna gani kuwe na mpangilio mzuri wa ujenzi wa miji.

Kwa hiyo, mipango miji nayo iongezewe pesa kwa makusudi kwa sababu bila kupangilia ardhi kwa kweli matumizi yetu ya ardhi ambayo haiongezeki yatakuwa sio mazuri. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Oran Njeza.