Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai, na pili nikushukuru wewe kwa kunipatia nafasi ili na mimi niweze kushiriki katika kuchangia hotuba ya Waziri wetu mpendwa, Waziri wa Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kusema naunga mkono hoja asilimia 100 kwa 100, na nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali yake yote kwa ujumla kwa utendaji wake mzuri wa kazi. Pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango, Naibu Waziri wake, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Katibu Mkuu na wataalam mbalimbali wa Wizara hii kwa umahiri wao wa utekelezaji wa mipango yote ambayo tumeanza nayo ya miaka mitano. Hongereni sana kwa consistency ambayo mmekuwa nayo. Tumeanza na mpango wa mwaka wa kwanza, wa pili, wa tatu, sasa wa nne; utekelezaji wa mipango ya maendeleo katika sekta mbalimbali za vipaumbele hauna mashaka unatekelezwa kwa kiwango ambacho kinaridhisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa reli ya kisasa uko vizuri, ujenzi wa Bwawa la Umeme la Stiegler’s Gorge au Bwawa la Mwalimu Nyerere unakwenda vizuri; upanuzi wa bandari zetu unakwenda vizuri, ujenzi wa meli katika maziwa makuu; Ziwa Victoria, Tanganyika na Nyasa mambo yanakwenda vizuri; ujenzi wa Daraja refu kabisa ambalo litakuja kuwa la kihistoria la Kigongo – Busisi mpango unakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ununuzi wa ndege za kisasa umeendelea kutekelezwa vizuri; yote haya yamo katika mipango yetu ambayo tumeanza nayo tangu uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano ulipoingia madarakani. Miradi mbalimbali inatekelezwa, mpango wa elimu bila malipo kuanzia darasa la kwanza mpaka kidato cha nne unatekelezwa bila wasiwasi na Watanzania wanafurahia; uboreshaji wa huduma za afya na wenyewe unatekelezwa na tunashukuru na ninaipongeza Serikali sana kwa sababu Watanzania sasa afya zao zinaimarika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema maneno haya napenda sasa niendelee kuchangia katika baadhi ya maeneo. Eneo mojawapo ambalo ninapenda kuchangia ni kuhusiana na suala zima la ujenzi wa wilaya hizi mpya na mikoa mipya. Wilaya yangu ya Mbogwe ni miongoni mwa wilaya mpya; niipongeze sana Serikali kwa sababu imeendelea kufanya kazi zake vizuri inatupatia pesa tunajenga makao makuu ya wilaya kwa maana ya halmashauri na ofisi za mkuu wa wilaya na tumepewa pia pesa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali, naomba tu Serikali iendelee kutupatia pesa ili tuweze kukamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kuchukua nafasi hii kuipongeza Serikali kwa uamuzi wake wa uhakika kabisa na wa thabiti wa kuhamishia Makao Makuu ya Serikali hapa Dodoma na ninaamini kabisa kila mmoja ni shuhuda kwamba ofisi mbalimbali za Wizara mbalimbali zimejengwa kupitia mipango hiihii ya Serikali ambayo tunaendelea kuitekeleza. Niombe Serikali iendelee na mkakati wake sasa wa kumalizia ujenzi wa Uwanja wa Msalato ili kwamba Makao Makuu yetu ya nchi yaweze kufikika kwa kufikia hata ndege na usafiri wa kimataifa kutoka mataifa mbalimbali ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kuipongeza Serikali kwa uamuzi wake wa kuyapandisha mapori ya akiba kuwa hifadhi za Taifa; Mapori ya Kigosi, Mto Ugala, Selous, Ibanda, Burigi Chato, mapori haya yanahitaji sasa uwekezaji mkubwa. Tuiombe Serikali itenge pesa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu katika mapori haya ili sasa huduma za utalii ziweze kufanyika kwa wepesi zaidi na uchangiaji wa Pato la Taifa kupitia hii Sekta ya Utali iweze kuonekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa kilimo ninapenda kuishauri Serikali iendelee kuwekeza katika viwanda vya utengenezaji wa mbolea kwa sababu Watanzania walio wengi wanashiriki katika shughuli za kilimo, na kwa maana hiyo tuiombe Serikali iwekeze zaidi katika kuvutia wawekezaji wa viwanda vya mbolea ili uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara uweze kuimarika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ikijitosheleza kwa chakula ninaamini kabisa hata ukuaji wake wa uchumi utakuwa ni wa uhakika zaidi kwa sababu wazalishaji mali wenyewe watakuwa wana nguvu za kutosha na kwa hakika wataweza kufanya uzalishaji katika sehemu mbalimbali za Serikali na hata katika viwanda na maeneo mbalimbali ya uzalishaji mali watafanya kwa uhakika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe tena kuishauri Serikali sasa kuwekeza zaidi katika eneo la upimaji wa ardhi. Nchi yetu ina tatizo kubwa la ujengaji holela katika miji yetu, niombe kabisa Serikali ilipe kipaumbele suala zima la upimaji wa ardhi katika maeneo mbalimbali ya miji inayochipukia na miji mikubwa ambayo tayari tunayo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia habari ya maendeleo hatuwezi kuzungumza maendeleo bila kutaja suala zima la mawasiliano kwa njia ya barabara. Niombe Serikali iendelee kutoa pesa katika wakala mbalimbali ikiwemo TANROADS na TARURA ili ujenzi wa barabara za lami kuunganisha maeneo mbalimbali kwa maana ya mikoa na makao makuu ya wilaya uendelee kwenda kwa kasi inayokubalika. Pia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini na wenyewe ujengewe uwezo, vitafutwe vyanzo mbalimbali vya mapato ili kuweza kuisaidia wakala hii ambayo ni changa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini kabisa kwamba REA inafanya vizuri kwa sababu imekuwa na chanzo cha uhakika cha tozo ya mafuta. Tumejikuta kwamba sasa hiki chanzo kinausaidia sana Wakala wa Umeme Vijijini kuweza kufanya mageuzi makubwa sana ya upatikanaji wa umeme katika vijiji vyetu na kwa maana hiyo ninaamini kabisa kwamba hata TARURA ikiwezekana kitafutwe chanzo kingine ambacho kitauwezesha kuwa na pesa za uhakika za kuweza kutekeleza miradi yake kwa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakala mwingine ni Wakala wa RUWASA ambao na wenyewe ni Wakala wa Maji Mijini na Vijijini. Wakala huu na wenyewe ni wakala ambao ndiyo umeanza, niiombe Serikali na yenyewe iendelee kuujengea uwezo wakala huu ili uweze kusambaza maji kwa uhakika kwa Watanzania ili waweze kupata maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaamini kabisa kwamba watu wakipata maji safi na salama afya zao zitaimarika na magonjwa mbalimbali ambayo yanatokana na maji yanaweza yakazuilika tunaweza tukajikuta hata bajeti ya matumizi ya afya inaweza ikashuka kwa sababu kama tusipokuwa na wagonjwa wengi maana yake sasa hata mahitaji ya madawa yatapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema maneno hao napenda kushukuru, ahsante sana kwa kunipata nafasi na Mungu awabariki.