Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutujalia zawadi ya uzima. Nitumie fursa hii kwanza kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Wizara yake na watendaji wote wa Wizara ya Fedha. Pia niwashukuru na kuwapongeza sana Serikali yetu chini ya Rais wetu John Pombe Magufuli na watendaji wote, tumefanya kazi vizuri kwa pamoja katika Mpango uliopita na matokeo yameonekana na sasa tunaenda kujadili mpango kwa ajili ya mwaka wa fedha unaofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la kilimo. Kilimo ndiyo uti wa mgongo wa nchi yetu na Waziri katika kitabu chake ameeleza kwamba mafanikio ya kilimo yamekwenda zaidi ya asilimia 100 lakini kusema kweli ni jambo la kusikitisha sana. Kilimo hiki ambacho kimetufikisha hapa tulipo kwamba nchi ina chakula cha kutosha na kimekwenda zaidi ya asilimia 100 si kilimo kile ambacho kimezalisha kwa nafasi ambayo tunasema ni sahihi, ni kwamba watu wamefyeka sana misitu, wamepanua sana mashamba lakini mashamba yenyewe tija kwa eka iko chini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini hali iko namna hii? Hali iko namna hii kwa sababu, moja, udongo wa nchi yetu haujapimwa. Wananchi wanatibu udongo kwa maana ya kutia mbolea ya kukuzia mazao yao lakini hawajui kama hitaji la udongo ni nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mbili wananchi hawa hawana Maafisa Ugani. Wizara ya Kilimo kama sikosei kuna kipindi haikuajiri Mabwana Shamba zaidi ya miaka 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni zana za kufanyia kazi. Tumeshuhudia makampuni mbalimbali ya matrekta mengine ya umma yameleta matreka katika nchi yetu matrekta yale mabovu, yamewatia hasara wananchi. Haiwezekani trekta unalimia msimu mmoja halafu inakufa. Tunashuhudia kabisa matrekta ya siku za nyuma yamekuwa imara na yamekuwa yakisaidia sana katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe tunapokwenda kuandaa Mpango mwingine, tujipange vizuri tuhakikishe kwamba tunapata Maafisa Ugani wa kutosha katika maeneo yetu ya kilimo ili kusudi wananchi wapate wataalamu wa kutosha. Ni jambo muhimu sana wakulima wapate wataalamu wa kutosha tujipange tupime udongo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye kitabu inaeleza kwamba kutakuwa na upimaji wa matabaka ya udongo basi hilo jambo lifanyike kwa sababu litaenda kuwasaidia wakulima. Mafanikio yake tuyaone kwamba wakulima sasa watumie eneo dogo halafu wazalishe zaidi lakini wanafyeka sana misitu na wanapanua sana mashamba ili kusudi wapate mazao mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwa taasisi zinazoleta vitendea kazi kama matrekta naomba Serikali iangalie. Kama kweli tunataka kuinua kilimo na kusaidia wakulima tuhakikishe kwamba zana za kilimo zinazoletwa kwenye nchi yetu ni imara na zinaweza zikawasaidia wananchi kwa muda mrefu kuliko sasa leo hii ni kilio, madeni waliyokopeshwa wananchi kwa ajili ya yale matrekta hayalipiki, taasisi zilizoleta matrekta zinalia hasara, mabenki yanalia hasara lakini matrekta ni mabovu. Huu ndiyo ukweli wenyewe, yale matrekta ni mabovu. Najua nayasema haya kuna watu watachukia lakini wacha wachukie tu, matrekta yale ni mabovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni suala la masoko. Tutakapokuwa tumewawezesha wakulima tujitahidi kuongeza masoko. Leo hii tunazungumza habari ya soko la Congo lakini tunalenga upande mmoja zaidi upande wa kusafirisha mizigo tu lakini tukumbuke kabisa kwamba mazao ya kilimo vilevile yana soko Congo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini tunaomba sana ile bandari ikamilike. Mtakapokuwa mnapanga mipango hiyo sasa tunawashauri mkamilishe bandari ile na iweze kufanya kazi vizuri kusudi tuanze kupeleka mazao Congo. Siku mzigo wa Congo utakapokuwa haupo, mazao yetu ya kilimo yatakwenda Congo na kwa idadi ya watu ina maana wao ni wengi kuliko sisi kwa hiyo ina maana wanahitaji kula kuliko sisi ni soko mojawapo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni Mchuchuma na Liganga. Mchuchuma na Liganga hata ukiangalia kwenye Hansard za Bunge sidhani kama kuna kipindi cha Bunge kiliwahi kupita bila kuongelea Mchuchuma na Liganga. Hebu sasa Serikali ifanye maamuzi ambayo yataifanya Mchuchuma na Liganga iweze kufanya kazi. Mmesema mmetenga fedha kwa ajili ya kulipa fidia kwa wananchi lakini vilevile mnasema mnataka kulipa fidia sehemu ya kupitisha njia ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke umeme utakuwa ni zao la Mchuchuma ili uende Liganga lakini kuna barabara zinazokwenda kule, iko barabara ya Itoni - Manda mpaka leo tunasema kilometa 30 tunapanga mpango wa maendeleo hapa naomba basi tukamilishe hii barabara kuanzia Itoni - Manda barabara ikamilike. Tunachoambiwa kila siku ni kwamba ile barabara ni ndefu sana ya zege nchi nzima hakuna barabara ndefu kama ile, haiwezi kutusaidia kama hii barabara haijaanzia Itoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sasa kama tunataka kufanya uwezeshaji migodi ile iweze kufanya kazi basi tujipange tuweze kutengeneza na barabara iweze kufika maeneo yale. Imekuwa ni bahati mbaya sana wataalamu wetu wanapopanga mipango unasikitika kuona kwamba wanaweza wakapanga kujenga, nichukulie mfano mmoja tu pale Njombe wamejenga Mahakama ya Mkoa lakini mradi ule ulikuwa ni wa kujenga Mahakama tu hakuna hata barabara kuifikia hiyo Mahakama yenyewe. Mkandarasi anapita porini mpaka kuifikia hiyo Mahakama yenyewe, hata itakapokuwa imekamilika hakuna fungu la kutengenezea barabara. Kwa hiyo, nafikiri tunapopanga mipango tuhakikishe kwamba kama tunajenga mradi kama Mahakama basi na mipango yake ya kujenga barabara kuifikia Mahakama hiyo iwepo kusudi itakapokuwa imekamilika iweze kusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nasema hata Mchuchuma, tunaiendea Mchuchuma tutakapokuwa tunakamilisha kumpata huyo mbia ambaye atashiriki katika kuchimba madini haya basi aikute na barabara iko tayari lakini barabara hii ni barabara ya kiuchumi itasaidia sana kuhakikisha kwamba Mkoa wa Njombe unazidi kuleta uchumi wa kutosha ndani ya nchi. Huu ni mkoa unaozalisha chakula kwa wingi na itasaidia wananchi kufanya kazi zao vizuri lakini ndiyo maendeleo yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine kwenye suala la barabara ambalo napenda kuishauri Serikali ni kwamba tunaposema tunataka barabara za kuunganisha mikoa kwanza tujiulize tunaunganisha huo mkoa na mkoa ili tupitishe kitu gani? Wakati mwingine tunaunganisha barabara mkoa na mkoa kwa wiki linapita gari moja tu lakini tumeacha barabara inayounga wilaya na wilaya na inapitisha mazao ya kutosha, inachangia uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani mtizamo huo tuuangalie upya kwamba tunajenga barabara ambazo zitapitisha mazao, tuangalie zinapitisha nini. Tusijenge tu barabara sababu tu watu wapite, waseme tu kwamba tumeunganisha mkoa na mkoa, mmeunganisha so what, ili kifanyike nini? Itakuwa siyo msaada. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuishauri Serikali ni suala la huduma za matibabu ya UKIMWI. Leo hii asilimia kubwa sana ya fedha au ya dawa wanazotumia waathirika wa UKIMWI ni za msaada. Tutambue moja huu msaada iko siku utakuwa na ukomo, ni lazima kwenye mipango yetu tuhakikishe kwamba tunajiwekea utaratibu wa namna gani tutajimudu wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la pekee kabisa kwenye suala la UKIMWI liko suala la watoto waliojikuta wamezaliwa na maambukizi ya UKIMWI, watoto hawa wana hali mbaya sana ya lishe. Kama Serikali kwenye mipango yetu ambayo tunaenda kuipanga sasa kwa ajili ya bajeti ijayo tulione hilo na tuhakikishe kwamba tunatenda kiwango kwa ajili ya kusaidia watoto ambao wameathirika na UKIMWI kwa sababu wamepata UKIMWI kutoka kwa wazazi wao. Watoto hawa wanapokuwa shuleni lishe ni duni sana na wanashindwa kusoma vizuri na magonjwa nyemelezi yanawasumbua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutokuwa na bajeti ya Serikali kwenye jambo la kuhudumia watoto waliothirika na UKIMWI watoto hao wengi sana tunawapoteza. Leo hii wagonjwa pekee waliobaki wanaumwa zaidi kutokana na tatizo la UKIMWI ni watoto ambao wamejikuta wana maambukizi kutokana na kuzaliwa na wazazi ambao walikuwa na maambukizi.

Kwa hiyo, ni ushauri wangu kwa Serikali itakapokuwa inapanga bajeti ihakikishe kwamba inaangalia kwa jicho la pekee kwamba tuwe na fedha ya kuweza kusaidia watoto hawa ili kusudi waweze kupata huduma bora ya chakula ili afya zao ziweze kuimarika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo nashukuru sana kwa fursa. (Makofi)