Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika hoja iliyoko mbele yetu ya Mpango wa Taifa kwa Mwaka wa 2020/2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia kwenye Mpango na nimetazama baadhi ya maeneo mahususi kama maeneo ya vipaumbele na hasa nikavutiwa na mirdi mikubwa ya kielelezo, ni mingi, lakini napenda kutaja umeme wa maji wa Nyerere National Park, reli ya standard gauge, Shirika la Ndege kuimarishwa, bomba la mafuta, gesi asilia na huu mradi wa makaa ya mawe ya Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi ambayo sasa hivi yanasababisha kuweko kwa upungufu mkubwa wa rasilimali ya nishati mbadala kama kuni na uhalisia wa kuhitaji uhifadhi mazingira na haja ya sisi kupiga marufuku ukataji wa mkaa hovyo, napenda kuishauri Serikali kwamba, hii miradi miwili mikubwa ya nishati mbadala, gesi asilia pamoja makaa ya mawe ingepewa kipaumbele kikubwa kabisa. Serikali ingefanya kila liwezekanalo hata kama ni kukopa fedha hii miradi itekelezwe kwa kasi Watanzania waanze kubadilika sasa na kutumia gesi kwa wingi zaidi na makaa ya mawe ili tuondokane na athari za kuharibu mazingira, kuchangia katika hali mbaya ambayo tayari tunayo inayoletwa na mabadiliko ya tabianchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipengele kingine nilipoangalia ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda, nimeguswa sana kutaka kusemea maeneo mawili; eneo la kilimo cha mazao na mifugo na eneo la wanyamapori. Kwa upande wa kilimo cha mazao, katika karne hii ya 21 tuliyopo kwa kweli matamanio yangu ni kuona Tanzania ikiondokana na kutegemea kilimo cha jembe la mkono na jembe la kukokotwa na wanyama. Tuondokane sasa katika hiyo sayansi ya karne zilizopita tuwekeze na Serikali ifanye kila liwezekanalo katika kilimo cha kisasa zaidi kinachotegemea matrekta na power tillers.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuishauri Serikali waanze tena kama zamani nilipokuwa mdogo, kuna wakati matrekta ya vijiji yalikuwa yanatolewa. Wapeleke matrekta vijijini hata wakopeshwe vijiji matrekta na power tillers tuweze ku-phase out kilimo cha jembe la mkono na jembe la kukokotwa na wanyama ili kilimo chetu kiweze kuwa na tija zaidi tuzalishe kwa wingi zaidi. Sambamba na hilo, Serikali iwekeze kwa kila hali katika kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika sekta ya mifugo nimeona kwamba kuna mipango mizuri inayowekwa ya kuongeza tija, masoko, uzalishaji, maeneo ya malisho, lakini naomba suala la maji lizingatiwe. Asilimia kubwa ya mifugo ambayo ndiyo inabeba uchumi wa wafugaji katika nchi hii ni mifugo ya asili ambayo mingi ndiyo ambayo inaiingizia Serikali mapato kwa mifugo inayouzwa ndani na nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta hii ya mifugo, naishauri Serikali kwamba, waangalie katika zile nyanda za malisho za wafugaji, waweke kabisa nguvu katika kuweka maji; maji ya mabwawa, visima virefu, sambamba na kuhakikisha masoko yetu ambayo nimeona wameweka mkazo kwamba, kuna uboreshaji wa masoko na viwanda vya kuchakata nyama na bidhaa za mifugo, masoko yetu yahakikiwe yaweze kutoa bei yenye tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi mifugo mingi ya nchi yetu inapelekwa nchi za jirani na hasa Kenya. Endapo tutakuja kutengeneza viwanda, tusipokuwa na mkakati wa kuweka bei inayofanana na ile ambayo wenzetu wanaopeleka mifugo Kenya wanaipata, tutaendelea kupoteza mazao ya mifugo kwa sababu wafanyabiashara wa mifugo wataendelea kutamani kupeleka nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali itendee Sekta ya Mifugo kama kile kinachofanyika kwenye Sekta ya Mazao ya nafaka kama korosho, kahawa na chai, wawe wanawekewa bei elekezi ambayo ninaamini huwa inatengenezwa kitaalam kwa kuangalia hali halisi ya bei za mazao hayo katika Soko la Dunia. Mifugo pia ifanyie hivyo ili mfugaji aweze naye kupata bei ambayo inamvutia, apende kuuza kwenye masoko ya ndani na apate faida ambayo ataipata tu popote atakapokwenda na asiwe na hamu ya kutaka kupeleka mifugo nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilikuwa nimeangalia katika suala la kufungamanisha uchumi na maendeleo ya watu, nikatamani sana nitoe maoni kwa Serikali na ninaomba niishauri Serikali kwenye suala la ardhi. Ardhi ndiyo mama yetu sisi wote, ndiyo chimbuko la kila kitu; na ardhi ya Tanzania haiongezeki, sisi tu binadamu ndio tunaongezeka na viumbe wengine walioko katika hii ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itilie mkazo sana suala la upangaji, upimaji na umilikishaji wa ardhi kuhakikisha kwamba tunawasomesha wataalam wa kutosha, tunawekeza katika kuweka vifaa vya kutosha na kuhakikisha kwamba hii ardhi inapangwa na ipangwe mapema kuepuka adha tunayopata ya makazi holela na migogoro ya ardhi isiyoisha. Hii itatusaidia sana kuondokana na migogoro na katika kuhakikisha kwamba Watanzania wa kesho watakuta ardhi iliyopangiliwa na ambayo matumizi yake yameshabainishwa na tutaondokana na adha kubwa tuliyonayo kwa sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa suala la wanyamapori, kwa kuwa naona muda wangu umeisha, nilikuwa naomba kwa sababu wanyamapori wameongezeka baada ya uhifadhi kuimarika, Serikali sasa iwekeze katika kuweka packages, mafungu yenye kuvutia ya kufidia au kutoa vifuta machozi na vifuta jasho vitakavyowafanya Watanzania waendelee kuthamini rasilimali yawanyamapori tuliyonayo. Hilo likifanyika, uhifadhi wa wanyama utaweza kuwa guaranteed. Kwa sababu sasa hivi mgongano wa wanyamapori na binadamu unazidi kwa sababu wanyama wamehifadhiwa na sisi pia tunaongezeka; na suluhisho la hilo ni kuwafanya wananchi wawe wavumilivu kwa kuwapa mafao mazuri kutokana na hifadhi ya wanyamapori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, napenda kusema kwamba naunga Mpango mkono na ninaipongeza Serikali yangu kwa kazi kubwa inayoendelea kufanya katika kutekeleza Mpango wetu wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)