Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza naomba nianze kwa kusema kwamba naunga mkono hoja iliyo mbele yetu. Naunga mkono hoja kwa sababu mbalimbali na nitazitaja chache. Hoja iliyo mbele yetu imeeleza vizuri katika paragraph ya kwanza kwamba tunatarajia kuandaa Mpango wa Maendeleo wa Tatu wa Miaka Mitano kwa sababu sasa tunamalizia huu tunaoutekeleza kwa sasa. Sasa kilichonivutia zaidi kuunga mkono hoja hii ni kwamba dhima inayotarajiwa katika mpango wa tatu utakaoandaliwa ambao inabidi sasa katika mapendekezo tunayoyapitisha leo tuanze sasa kuweka mambo ya msingi yatakayotusaidia kuwa na mpango mzuri wa miaka mitano mingine; na dhima hiyo inasema kama ilivyobainishwa katika paragraph ya kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuongeza mauzo nje na uwezo wa ushindani Kikanda na Kimataifa. Hili ni jambo jema na dhima hiyo itatusaidia kwa sababu tunapokamilisha huu mpango wa miaka mitano ambao tulijielekeza katika kujenga Tanzania ya viwanda, sasa tukielekea sasa kuongeza mpango wa tatu ukijikita kwenye kuongeza mauzo nje na uwezo wa ushindani Kikanda na Kimataifa itakuwa ni jambo jema. Kuna mambo ya msingi ambayo itabidi yawepo kwenye mpango wetu wa mapendekezo sijayaona na ningependa Mheshimiwa Waziri baadaye angalie ni jinsi gani anaweza akachukua mapendekezo hayo nitakayoyapendekeza kuwa sehemu ya mpango wetu tutakaoupokea na kuupitisha katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo ni muhimu sana kama tukitaka kujenga, kuongeza uwezo wa mauzo ya nje na kujenga ushindani lazima tuanze kwa kujenga ushindani wa ndani. Kwa nini ushindani wa ndani ni muhimu? Ni muhimu kwa sababu huwezi ukauza nje, huwezi ukajenga uwezo wa ushindani kama hujajenga uwezo mkubwa wa ushindani wa ndani, nitatumia mfano mmoja tu, mfano wa wine, uzalishaji wa wine; ukiangalia Sekta ya Wine kidunia kwa mfano ukiangalia Italy wao wanazalisha chupa za wine bilioni sita. Tanzania ukichukua kwa makadirio ya juu kabisa tunazalisha chupa za wine laki mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiwa unazalisha chupa za wine laki mbili, ukitaka kujenga uwezo wa ushindani kwamba tuwezeshe sasa wine yetu iweze kushindana hata ndani ya Afrika Mashariki, basi lazima tuanze kujenga ushindani wa ndani kwanza. Sasa kujenga ushindani wa ndani wa wine peke yake ukiangalia kwa mfano wine tulizonazo hapa Dodoma ukiangalia chupa sitataja aina ya wine na kampuni kwa sababu unaweza ukajikuta labda kampuni ukiitaja kwamba haifanyi vizuri inaweza isijisikie vizuri, kwa hiyo sitataja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, ukiangalia hizi chupa utakuta kuna nyingine ina lebo ambayo ni water proof hapa hapa Dodoma, lakini utakuta wine nyingine ina lebo ambayo mvua ikinyesha hiyo lebo inaloana hapo hapo. Sasa namna hiyo, ukiangalia Sekta ya Wine tu kwa hapa Dodoma ni kwamba, ukisema unataka kusaidia wine iweze kushindana maana yake uangalie je unawezeshaje hii Sekta ya Wine kwa mfano, kuwawezesha kupata lebo ambazo zinaweza zikajenga ushindani, lakini kwa kuanzia lazima ujenge ushindani wa ndani wakishindana ndani ndiyo unaweza ukapata mtu wa kuweza kushindani nje kwenda kwenye soko la nje. Kwa hiyo huo ni mfano mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mfano mwingine mdogo, kuhusu soko la kahawa la ndani na soko la pamba la ndani, lazima tujenge ushindani wa ndani, kwa mfano, kwenye kahawa ushindani wa ndani maana yake ni nini? Lazima tuangalie katika mpango huu tunaokuja nao tuangalie nini tunaweza tukafanya kujenga ushindani wa ndani wa ununuzi wa mazao yetu, kushindana ndani. Kwa mfano, mkulima wa kahawa yeye anapenda akiuza kahawa yake apate fedha yake pale pale. Natambua kuna hii dhana kwamba hela itapitia kwenye akaunti, watu wafungue akaunti, lakini mkulima anaangalia, yeye kama anazalisha kilo 10 au 20, unapomwambia utalipwa kupitia benki anakushangaa kwa sababu anaona gharama ya kufuatilia hiyo hela ni kubwa kuliko kile ambacho atakuwa anakifuatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kuna uwezekano wa kuweka mazingira ya ushindani ndani. Kwa hiyo ili tufanye hivyo mkulima huyu angependa awezeshwe aweze kuzalisha kwa tija, akiweza kuzalisha kwa tija utaweza kujenga ushindani. Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba katika mapendekezo haya sijaona vizuri inavyoweka mazingira ya kujenga ushindani wa ndani kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa nilizungumzie kwa haraka haraka ili kujenga ushindani tunahitaji mkulima kumwezesha kwa mfano, kupata viuatilifu. Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba Wizara yake walitenga bilioni kumi nafahamu, lakini baada ya kutenga bilioni kumi LC ikafunguliwa pale BOT, Kampuni ya TFC ikapewa jukumu la kuagiza hiyo viuatilifu. Viuatilifu hivyo mpaka ninavyozungumza hivi sasa viko pale bandarini, bilioni kumi zimetoka lakini viuatilifu mpaka sasa hivi vinaozea bandarini na bilioni kumi zimetumika. Sasa mambo ya namna hiyo hayajengi ushindani, kwa nini? Kwa sababu hivyo viuatilifu vikitoka bandarini vimekuja havijatoka bandarini maana yake tunaendelea kumkwamishwa mkulima na hilo siyo lengo letu. Kwa hiyo Mheshimiwa labda atapokuwa anatoa ufafanuzi nitaomba atueleze hizo bilioni kumi alizotoa na mpaka sasa hivyo viuatilifu viko pale bandarini vimelala pale ni jitihada zipi ambazo amezichukua za makusudi, fedha alitoa lakini viuatilifu vinaozea pale bandarini mambo ya namna hiyo hayatusaidii kujenga ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kuzungumzia kwa ufupi kwenye kujenga ushindani kuhusu kilimo. Natambua pale tuna Mkulazi one na Mkulazi two, lakini ukisoma kwenye mapitio ya utekelezaji kwenye vitabu alivyotupa Mheshimiwa Waziri, ukisoma pale huoni kama kuna kitu kinachoendelea kwenye Mkulazi one na Mkulazi two kuhusu uzalishaji wa miwa. Ukisoma pale unaambiwa ekari 3,500 zimelimwa na ekari 750 zimepandwa. Sasa unajiuliza kama umelima 3,500 umepanda 750 maana baada ya miezi sita na zile ulizolima zitakuwa zimeshaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi unapolima miwa halafu kiwanda hakijajengwa wala mitambo haijaja, baada ya miezi 12 miwa iko tayari kiwanda hakipo, maana yake hiyo miwa huwezi kuitumia tena. Ningeshauri kwa kweli Mheshimiwa Waziri umefika wakati Serikali ikajiondoa masuala ya kujenga viwanda badala yake iachie Private Sector. Hapa Tanzania tuna viwanda ambavyo vinafanya vizuri sana katika sukari sitaki kutaja ni kipi, lakini ni vizuri tungeiachia Private Sector ikafanya hivyo na hii Mifuko ya Hifadhi tuiachie iendelee na shughuli zake za mambo ya hifadhi, kwa sababu kwa kuendelea kuiambia Mifuko ya Hifadhi ifanye shughuli za uzalishaji wa miwa tunajenga mazingira ambayo hayana tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema tunajenga Tanzania ya viwanda lazima tuweke mazingira mazuri ya kuwa na mikopo ya uhakika, natambua tunayo TIB lakini ukiiangalia unakuta kwamba hii Tanzania Investment Bank uwezo wake ni mdogo, lakini tunayo mabenki mengi huko ya nje ya nchi ambayo yako tayari kuja Tanzania kuwekeza. Nadhani katika Mpango huu wa Maendeleo ujao tungeweka vivutio vya kuwezesha kuvutia investment banks kuja hapa Tanzania kuwekeza na kwa kufanya hivyo tutasaidia kuweka mazingira mazuri ya kuendelea kujenga Tanzania ya viwanda na pia kujipanga vizuri katika kutekeleza ule mpango wa tatu tutakaouandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika taarifa tuliyopewa ya utekelezaji wa mpango wa maendeleo uliopita, utaona kwamba tulitenga bilioni 123.9 kwa ajili ya kilimo, lakini zilizotoka ni bilioni 56.5 ambazo ni sawasawa na asilimia 45.46. Pamoja na kutenga fedha kidogo na tukatoa kidogo, lakini kilimo ndicho kimechangia kwa asilimia kubwa kwenye pato la Taifa, kimechangia asilimia 28.6. Hii maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba tukitenga fedha nyingi zaidi kwenye kilimo tunaweza tukapata matokeo makubwa zaidi na uchumi wa nchi unaweza ukanufaika zaidi, hiyo ndiyo maana yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama hivyo ndivyo ilivyo, nimejaribu kusoma kwenye mapendekezo ya Mwongozo, sioni popote ambapo mapendekezo yametolewa moja kwa moja kuagiza sekta mbalimbali, kuagiza Idara mbalimbali, kuagiza halmashauri zetu ili kutenga fedha za kutosha kuelekea kwenye kilimo, sioni ikijitokeza moja kwa moja. Kwa hiyo katika mpango wetu lingekuwa ni jambo jema kama jambo hilo lingeangaliwa na likajitokeza moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo ningependa niongelee kabla muda wangu haujakwisha, tunayo East Africa Master Railway Network natambua kwamba tunazungumza hii SGR tunaendelea kuijenga ni jambo jema, natambua kwamba itatoka Isaka itaenda Kigari, lakini ningeshauri ikifika maeneo ya Runzewe au Biharamulo i-branch pale ielekee Kagera, ikifika Kagera ielekee Kampala, ikifika Kampala ielekee South Sudan. Tukifanya hivyo tutakuwa tumejenga uchumi nzuri kwa nchi yetu, pia tutawezesha hata Mkoa wa Kagera kuuandaa kushiriki katika uchumi shindani na kuongeza mauzo yetu ya nje ya nchi na tufikie hata viwanda vyetu mbalimbali vilivyo katika Mkoa wa Kagera viweze kuibuka na kufanya vizuri zaidi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wako umekwisha.