Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa uliokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2020/2021

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami nitoe maoni kwenye hoja iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani kuna mahali tumekosea kwa sababu miaka ya nyuma tulikuwa tunafanya semina Wabunge wote tunapitishwa kwenye Mpango kabla hatujaanza kuujadili. Vilevile tulikuwa tunapewa walau ABCD ya tathimini ya Mpango uliopita na yote hiyo ni ili kujiweka sawa tu ili mjadala uweze kunoga vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote hayo, naomba nijadili kwa kuzungumzia mambo matatu. Jambo la kwanza ni kilimo. Miaka baada ya uhuru tulikuwa hatujaanza kuvuna madini katika nchi yetu na kwa sababu hiyo uchumi wa nchi yetu ulibebwa na kilimo. Mazao ya biashara wakati huo pamba, kahawa, korosho, katani, pareto na kadhalika ndiyo yaliyobeba uchumi wa nchi hii sasa mazao haya yanakufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama sote tutakumbuka wakati wa Mwalimu katika maeneo ambayo mazao haya yalikuwa yanapatikana kwa wingi kulikuwa pia kuna viwanda vya ku-process mazao haya. Tulishuhudia Mwatex, Mutex, Coffee Curing kule Moshi na kadhalika sasa vyote hivi vimekufa na sijui nini kilitokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri kwa sababu asilimia 65 ya Watanzania wamejiajiri katika kilimo, basi huu Mpango uje na kitu tofauti kuhusu kilimo. Sote ni mashahidi kwenye bajeti tunayomaliza fedha zilizotengwa kwa ajili ya kilimo karibu Wabunge wote tulikuwa tunapiga kelele kwamba ziongezwe katika kilimo, ufugaji, na katika uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba fedha za kutosha zitengwe kwenye kilimo ili kuimarisha miundombinu ya kilimo. Ni muhimu sana tuone kuna mpango ambao uko wazi wa namna ambavyo nchi hii sasa tutakuwa na viwanda vya kutosha vya mbolea. Fedha za kutosha ziingizwe kwenye Mpango tuone ni namna gani sasa tunapata masoko ya ndani na hata ya nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaposema hivi siyo kwamba nabeza kazi ambayo imeshaanza kufanywa, kuna kazi inafanyika, lakini nachosema iimarishwe ili wakulima wawe na hakika ya kupata kipato cha kutosha na kizuri kutokana na jasho lao. Wewe ni shahidi mzuri sana na Waheshimiwa Wabunge jinsi tulivyohangaika hapa na mahindi, wakulima Sumbawanga, Mbeya na maeneo mengine walivyopata shida ya kuuza mahindi yao. Sasa hivi gunia la mahindi kwa mfano Kaskazini huku imevuka laki moja na kitu, wakati huo huo mahindi gunia yaliuzwa shilingi 20,000, shilingi 25,000 au shilingi 30,000. Sasa tutengeneze utaratibu ambapo kutakuwa hata na security kwa mkulima huyu ili wakati mazao yakipatikana kwa wingi awe na hakika basi baadaye kunaweza kukawa na nafuu na yeye akapata kipato cha kutosha kutokana na nguvu zake alizotia kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna soko nataka nilitolee mfano, kwa mfano soko la Kibaigwa hapa lilikuwa la Kimataifa watu walikuwa wanatoka Rwanda, Burundi na maeneo mengi ya nchi hii wanakuja kununua mahindi, alizeti na kadhalika lakini sa sahivi linaelekea kufa. Kwa hiyo, masoko ya aina ya Kibaigwa Serikali ingeona uwezekano wa kufanya utafiti masoko haya yawepo katika maeneo mbalimbali kusaidia kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la viwanda vya kati kama ambavyo vilikuwepo hapo zamani. Nchi hii kuna maeneo ambayo kuna matunda mengi sana kwa mfano Muheza na Korogwe, machungwa ni mengi sana lakini wakulima wanaonewa kwa sababu yanakuja kwa wingi halafu hatuna hata viwanda vidogo vidogo vya kutengeneza concentrate za machungwa au kuhifadhi yale machungwa yaweze kutumika kipindi kingine ambacho siyo cha msimu. Hivi vitu hivi ndiyo vinakuza thamani ya yale mazao na wakulima wananufaika kutokana na mazao yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuongeze fedha kwenye taasisi za kilimo ili ziweze kufanya utafiti wa kutosha kuhusu mbegu bora kwa ajili ya wakulima, tuweze kupata mbegu zinazoweza kuendana na hali ya hewa. Vyuo vingi sasa hivi vinapata shida ya kufanya utafiti kwa sababu fedha zinazoingizwa kwenye utafiti wa kilimo vilevile zinakuwa za mashaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia tuanze kufikiria kuongeza pesa za kutosha kwenye kilimo cha umwagiliaji. Nchi hii ina maji mengi sana, mvua ikinyesha sote ni mashuhuda kwa mfano barabara hii ya Dodoma maji yamekuwa yanatoka Kiteto na maeneo mengine yanafunga kabisa barabara lakini tungeweza yale maji kuyahifadhi na kuyatumia kwa ajili ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Rombo kwa mfano mvua zikinyesha na sasa hivi Rombo tunapata mvua nyingi sana za vuli, maji yanateremka kutoka Kilimanjaro yanavuka kwenye mito yetu ya asili kule yanaenda Kenya na kule Kenya wameya-tape yale maji. Kuna eneo kule Kenya linaitwa Chumvini, wanalima mbogamboga, nyanya, vitunguu na kadhalika, wanakuja kutuuzia sisi ambao maji yanatoka kwetu. Kwa hiyo ilikuwa ni rahisi tungeweza kwenye makorongo ya ile mito ya misimu tukaiziba namna fulani na mawe yapo ya kutosha tukahifadhi yale maji, baadaye tukayatumia kwa ajili ya kilimo kuendelea kufikiria kuangalia anga mvua zitakuja lini na kadhalika, tutazidi kupata shida na kama nilivyosema nchi hii watu wetu walio wengi wamejiajiri katika kilimo na hakika kabisa kwamba kilimo kikiboreshwa kwa namna kubwa sana tutakuwa tumesaidia watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha mazao ya biashara kuna mazao mchanganyiko kama mbaazi, kunde, mahindi na kadhalika, tuimarishe pia masoko kwa ajili ya haya mazao, kwa sababu haya mazao yana masoko ndani, yana masoko nje na wakulima wetu wengi wanalima mazao ya namna hii. Kwa hiyo kuhusu kilimo nafikiri nimeongea vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye ufugaji, ngombe wetu wanabaki ni ngombe wale wa asili na hapa Bungeni tumekuwa tukizungumza namna ya kubadilisha wale ngombe waweze kuwa bora zaidi na wakulima waweze kufuga ngombe wachache lakini wenye kipato cha kutosha. Sasa ni rai yangu kwamba Serikali iangalie namna sasa ya mawazo haya kutekelezwa. Zamani kulikuwa na vituo vya uhamilishaji katika baadhi ya vijiji, madume bora yalikuwa yanapatikana kwenye centre moja kwa ajili ya kubadilisha ile mbegu kwa ngombe na hata kwa mbuzi. Sasa baadhi ya hizi centre zimekufa na hatujui zimekufa namna gani. Kule kwetu Rombo centre kama hizi zilikuwa nyingi kabisa mimi nikiwa mdogo, nilikuwa naambiwa chukua ngombe peleka, napeleka, lakini sasa hivi vimekufa. Hivi ni vitu vya kawaida, lakini ni vitu muhimu sana kwa sababu ngombe hawa maziwa na mazao mengine ya maziwa yanasaidia sana katika kipato cha wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hawa ngombe wengi tunaopata Umasaini, Usukumani na kadhalika bado hatujafanya vya kutosha. Mazao yanayotokana na ngozi, mazao yanayotokana na pembe na kadhalika bado ni shida, wenzetu Kenya hapa wana Kiwanda cha Nyama cha Thika, ngombe wanatoroshwa kupitia mpaka wa Loliondo, wanaenda wanachinjwa Thika na matokeo yake nyama inabaki huko, ngozi inabaki huko na kadhalika. Kama nchi hatujashindwa kujenga kiwanda cha kisasa cha kimataifa kinachohusiana na mazao ya mifugo, tunaweza kwa sababu kama mengine yamewezekana kwa nini hili lishindikane na likifanyika ina maana tunawasaidia wakulima na wenyewe wanapata faida kutokana na kazi wanayofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni uvuvi. Sasa hivi watu wamehamasika kufuga samaki na mimi nina diwani wangu mmoja ambaye amesoma hapo Sokoine anawafundisha watu namna ya kujenga mabwawa wanafuga samaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua hata Waziri Mheshimiwa Mpango ana bwawa lake kubwa sana la samaki, ndiyo mimi najua hatujafahamiana barabarani na huyu mzee, ana bwawa kubwa sana la samaki. Sasa uangaliwe uwezekano wa Watanzania kufundishwa namna ya kufuga samaki kwa sababu watapata kipato kibiashara vilevile wataongeza afya zao, manaa yake tukizungumza samaki tunazungumza samaki wa baharini na kwenye maziwa yetu makubwa tu, lakini Watanzania wanaweza wakafuga samaki kama sehemu ya ajira na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo tuangalie uvuvi wa bahari kuu tumeiongela sana hili. Uvuvi wa bahari kuu unaweza ukatuletea kipato kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, ambalo ningependa kuzungumza pia bajeti iongeze fedha za kutosha katika miradi ya maji. Huwezi kuamini sisi tuna ule mlima, chemichemi zilikuwa nyingi sana, lakini na vijiji karibu 41 havina hakika ya maji, yaani kilio cha maji ni kikubwa katika Jimbo langu la Rombo kuliko kitu kingine chochote. Nashukuru kuhusu umeme bado vitongoji kadhaa, lakini kuhusu maji shida ni kubwa sana naomba Mheshimiwa Mpango atakapokuja bajeti yake katika miradi ya maji iimarishwe kwa sababu kwa kweli maji ni uhai na kelele nyingi sana za Watanzania sasa hivi unaona hapa kila Mbunge akisimama anazungumza kuhusu maji katika eneo lake. Nadhani kama tukiweza kukazana kwenye maji kama tulivyokazana kwenye mambo mengine sasa watu wanaweza wakafikia mahali wakatulia na wakafanya mambo yao sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Ahsante sana.