Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Kilimo

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie hoja iliyo mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza viongozi wa Wizara hii, Mheshimiwa Waziri Mheshimiwa Hasunga, Manaibu wake Mheshimiwa Bashungwa na Mheshimiwa Mgumba; kwa kweli wote tumejionea ni jinsi gani wanavyohangaika kusukuma sekta ya kilimo. Wamekuwa wakihangaika usiku na mchana kuhakikisha yale mazao yetu ya kimkakati yanapata ufumbuzi wa changamoto zilizopo, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu unajikita katika maeneo matatu; kwanza zao la korosho, umwagiliaji na sekta ya ushirika. Nikianza na korosho, nichukue nafasi hii kipekee kumpongeza Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa maamuzi ya kijasiri ambayo aliyafanya mwaka jana kwa kuamua kununua korosho baada ya soko la korosho kuanza kuyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anayeitakia mema sekta hii ya korosho hawezi kubeza juhudi zilizofanywa mwaka jana. Sekta ya Korosho inahitaji fedha nyingi na ndiyo maana hata baada ya kufanya maamuzi yale aliamua kuvunja Bodi ya Korosho na kuagiza Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko isimamie zoezi lile. Nichukue nafasi hii kuipongeza Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko kwa kazi ambayo waliifanya lakini pia na Benki ya Maendeleo ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwapongeze Wakuu wa Mikoa kwa mikoa ambayo inalima korosho, kwa changamoto ya mwaka jana walisimama kidete kuhakikisha kwamba wakulima wanapata haki yao na kusimamia mazoezi mbalimbali yaliyokuwa yanaendelea likiwemo na zoezi lile la uhakiki ambalo Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa walishirikiana kuhakikisha kwamba wakulima ambao ni wakulima wa korosho kweli ndiyo wanaolipwa fedha za korosho na siyo wengineyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee niipongeze Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji, ilifanya ziara kwenye mikoa ya kusini na kusaidia kuisimamia Serikali kufanya malipo haraka kwa wakulima wa korosho ambao bado walikuwa wanadai fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi bado kuna changamoto. Sasa hivi bado kuna wakulima ambao bado wanadai fedha zao takribani bilioni 100. Mimi naamini kwa sababu Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo mahsusi alipokuwa kwenye ziara ya mikoa ya kusini, naamini kwamba Wizara ya Fedha na Wizara ya Kilimo wataweka mikakati ya kutekeleza agizo hili ili wakulima hawa waweze kulipwa pesa zao kabla ya msimu mpya haujaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, nishauri mambo yafuatayo kuhusu zao la korosho. Kwanza tunapomaliza msimu huu, kwa sababu kuna watu bado wanadai, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kama ulivyohamia wakati ule tunaanza kununua, hebu tengeneza timu ya wataalam na watu waadilifu kwa sababu wewe mwenyewe ulishuhudia kwamba katikati pale wakati wa uhakiki kuna vijana wako hawakuwa waaminifu; na nikupongeze kwamba ulichukua ulichukua hatua za makusudi mapema ili kuzuia zile dalili za rushwa ambazo zilitaka kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili tumalize msimu vizuri, unda timu ndogo izunguke kila wilaya kusikiliza manung’uniko ya wakulima. Kuna wakulima bado wana manung’uniko, kuna mkulima alipeleka kilo 500 amelipwa kilo 300, akienda kwa viongozi wa AMCOS anaambiwa kwamba mwaka huu sisi hatukusimamia. Kwa hiyo, timu yako itasaidia ku-clear doubts za wakulima kabla ya msimu mpya haujaanza, nakuomba sana ufanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili; kuna changamoto zingine, kuna maeneo, mimi kesi yangu naifahamu kuna Mwenge AMCOS kuna akaunti za wakulima 200 zimefungwa, wanatupiana lawama kwamba amefunga fulani. Kwa hiyo, timu yako kama hiyo itatoa suluhisho kwa matatizo madogo madogo ambayo yamebaki katika sekta hii ili tuanze msimu mpya na mambo mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri pia kuhusu suala la ubanguaji. Changamoto nyingine tunazipata kwenye zao la korosho kwa sababu bado tunapeleka nje korosho ghafi.

Wenzetu wa Msumbiji wamekaza kamba kuhusu ubanguaji na wanafanya vizuri. Ni muda umefika sasa hivi tujikite katika ubanguaji. Tuna viwanda 12 vya awali vile ambavyo vilijengwa bado havifanyi kazi na wanunuzi wengine wamefanya maghala, kwa hiyo wanyang’anywe. Hata hivyo kuna wawekezaji wapya wameanza kujitokeza sasa hivi kutaka kujenga viwanda vipya vya ubanguaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali yangu sikivu kwanza iweke vivutio kwa wawekezaji hawa lakini pili ipunguze kodi kwa mitambo na mashine mpya wanazoingiza ili gharama za uwekezaji zisiwe kubwa; tukifanya hivyo korosho yetu nyingi tutabangua. Kwanza tutaongeza ajira na tuta-add value kwenye korosho zetu na hivyo mkulima atapata fedha ambayo itaongeza kipato chao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye tasnia ya korosho kuna mambo mengi na bado tasnia ya korosho inahitaji usimamizi mkubwa. Kwa hiyo nikuombe Waziri wa Kilimo mwaka jana kwa sababu ya uzembe wao ambao walifanya Bodi ya Korosho ilivunjwa, niombe sasa kwamba muda umefika tuunde hiyo Bodi ya Korosho ili isimamie tasnia yetu ya korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko ilifanya jukumu lile kwa wakati ule kwa dharura iliyojitokeza lakini sasa hivi utafute watu waadilifu, na Tanzania wapo waaminifu, ili waanze kusimamia sekta hii ya korosho ambayo takwimu zipo wazi kwamba inaingiza fedha nyingi katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye ushirika. Ushirika kama alivyosema mzungumzaji aliyepita, Mheshimiwa Jitu Soni, tulitarajia kwamba ingekuwa mkombozi kwa mkulima kwa ni ukweli usiopingika kwa Tanzania ushirika bado unamuumiza mkulima, watumishi wa ushirika hawasaidii wakulima. Kwenye zao la korosho ukifuatilia ubadhilifu mwingi unafanywa watumishi wa ushirika wamo ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi katika sekta hii ya ushirika sijui kwa nini; ukienda kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa watumishi wa ushirika na ardhi zamani utakuta wamejitenga pembeni, siku hizi Mheshimiwa Lukuvi amefanya mabadiliko makubwa sana, watumishi wa ardhi wanafuatiliwa. Mheshimiwa Hasunga muda umefika sasa, wafuatilie watumishi wa ushirika, fanya mabadiliko makubwa, wahamishe. Haiwezekani Afisa Ushirika ameanza kusimamia korosho tangu akianza kazi mpaka anastaafu. Mpeleke kwenye pamba akasimamie tasnia ya pamba na pareto atakuwa active, lakini Afisa Ushirika amezaliwa kwenye korosho mpaka anastaafu yupo kwenye korosho hata tija yake na ufanisi utakuwa umepungua. Fanya maamuzi magumu wa Mtwara peleka Musoma akasimamie pamba na wa Musoma peleka Songea akasimamie kahawa na hivyo wataongeza tija lakini watakutana na mazingira mapya ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikushauri sana Mheshimiwa Hasungam pamoja na mambo ambayo yanatakiwa ufumue, fumua ushirika, ushirika bado kuna uozo haumsaidii mkulima, ni mzigo kwa mkulima. Mheshimiwa Hasunga tunakuamini na uwezo huo unao; na ulivyoingia tu kwa sababu umeapa tu ukaenda kusimamia korosho, Inshallah utafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la umwagiliaji. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hatua alizochukua juzi kwa kuwasimamisha wale viongozi wa Tume ya Umwagiliaji. Mheshimiwa Hasunga unga mkono pale alipoishia Mheshimiwa Waziri Mkuu, bado kwenye ngazi ya kanda nako kuna madudu vitu, nenda kafumue kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tume ya Umwagiliaji kama ingekuwa inafanya kazi yake vizuri tusingehangaika sasa hivi kutafuta chakula kutoka maeneo mengine. Sisi Mtwara tuna Ruvuma Basin, Kitere, Rufiji Kusini lakini hayatumiki ipasavyo. Haiwezekani mradi wa mwaka mmoja lakini watu wa tume wanauandaa kwa miaka mitatu na watu wa tume kwa sababu tuna organization structure ambayo ni ya kizamani, wapo kwenye kanda. Kanda ya Kusini ashughulikie Mtwara, Lindi na Ruvuma, hawezi kuwa na ufanisi. Hii tume ivunjwe sasa hivi wawepo kwenye mikoa, yule wa mkoa awajibike kwa RAS na wawepo watendaji kwenye Wilaya wawajibike kwa wakurugenzi; lakini sasa hivi wapo wapo tu, wakiwa kwenye kanda hawajibiki kwa RAS yeyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Chikota kwa mchango wako.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)