Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa
Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii nimpongeze sana sana Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Kwakweli tunampongeza sana Dkt. Mwinyi kwa kazi nzuri anayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza Mkuu wetu wa Majeshi nchini, mmeona kabisa kwa siku hizi zote za karibuni nilisema hapa asubuhi, Sera yetu ya Ulinzi na Usalama imejikita katika maeneo kadhaa kama manne hivi. Ukiangalia la kwanza ni ulinzi wa mipaka yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Waheshimiwa Wabunge hatutakuwa na moyo wa shukrani kama siku hii ya leo hatutalipongeza Jeshi letu la Ulinzi kwa ulinzi mkubwa unaofanywa kwenye mipaka ya nchi hii na hiyo imesababisha nchi yetu kuendelea kubaki ni nchi pekee sisemi kwenye mataifa mengine, sijui kinachoendelea huko, lakini mmeona ulinzi wa Taifa letu kwenye mipaka yetu ni imara kweli kweli na tuko salama kweli kweli. (Makofi)

Kwa hiyo, ni lazima kwakweli siku hii ya leo ilikuwa ni siku yetu sisi Wabunge wote kwa pamoja kuungana kwanza kulishukuru Jeshi letu la Ulinzi na kulipongeza kwa kiasi kikubwa na kiasi cha kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera yetu ya Ulinzi na Usalama inasema Jeshi hili la Ulinzi na Usalama katika hali moja ama nyingine litashirikiana na raia katika masuala mbalimbali. Mmeshuhudia Jeshi hili, tulipopata m aafa kwenye kivuko, Jeshi letu la Ulinzi na Usalama na Jeshi la Polisi walifanya kazi kubwa kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mmeona nilisema hapa asubuhi sitaki kurudia yale yaliyokuwa yanasemwa lakini pale ilipotokea kuna umuhimu wa Jeshi letu la Ulinzi na Usalama na Jeshi letu la Polisi kufanya kazi kwa pamoja wamefanya kazi nzuri Njombe, wamefanya kazi nzuri kule Kibiti na maeneo mengi tu wamefanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwakweli nasimama hapa kulipongeza Jeshi letu la Ulinzi na Usalama, lakini tumeona kabisa kwamba Jeshi hili lina kazi na limeendelea kurithi maono na maoteo mazuri ya Baba wa Taifa kudumisha ushirikiano na mahusiano mema na nchi nyingine na hasa katika Bara la Afrika. Mmeshuhudia Wanajeshi wetu wakijitoa kweli kweli kwenye ulinzi na usalama hata kwenye mataifa mengine nje ya Taifa letu na hiyo ndiyo Sera yetu ya Ulinzi na Usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali tunachokisema hapa tunampongeza kwanza Amiri Jeshi Mkuu, Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa sababu kama leo wote sisi Wabunge tunakubaliana na kuungana mkono kwamba kazi nzuri inafanywa na Jeshi letu la Ulinzi na Usalama ina maana Amiri Jeshi Mkuu anafanya kazi yake sawa sawa kulisimamia Jeshi letu. Kwa hiyo ni lazima na yeye tumpongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa sisi tunachokichukua kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge ni ushauri ambao, ushauri mwema, ushauri wenye msingi ambao Bunge linatushauri Serikali namna nzuri ya kuliboresha Jeshi letu, ya kuhakikisha Jeshi letu linaendelea kufanya kazi yake vizuri tena kwa weledi mkubwa na hiyo hatuna shaka, tumekuwa tukishuhudia lakini tunaendelea kupokea ushauri wa Waheshimiwa Wabunge wa kuhakikisha kwamba Watanzania wanaungana mkono na Jeshi letu na wanaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kwa Jeshi letu ili liendelee kuwa Jeshi la mfano na liendelee kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya ambayo hata ungeniamsha kwenye usingizi ningeyasema tu, ninaomba nichukue nafasi hii kuunga mkono hoja, kumpongeza Waziri, kulipongeza Jeshi letu na kumpongeza Amiri Jeshi Mkuu Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)