Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, Kiwanda cha MUTEX Musoma kilichokuwa kinazalisha kanga na vitenge, kilitoa ajira 1,000, lakini tangu kibinafsishwe kiwanda hiki hakifanyi kazi hivyo kufifisha uchumi kwa Mkoa wa Mara na Taifa kwa ujumla. Kiwanda hiki kwa sasa kimekosesha ajira kwa Wanamara na hasa wanawake walikuwa wakifanya kazi kwenye kiwanda hiki. Je, ni lini kiwanda hiki kitarudishwa Serikalini au kutafuta muwekezaji mwingine?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia zipo taarifa kwamba mashine mpya zilizokuwepo katika kiwanda hiki kwa sasa hazipo tena na ziling’olewa. Je, Serikali wanazo taarifa za kiwanda hiki kuharibiwa miundombinu yake?

Mheshimiwa Naibu Spika, taulo za wanawake, watoto wa kike zinauzwa bei ghali hivyo wanawake na watoto wa kike wenye kipato cha chini kushindwa kumudu gharama na hata kuhudhuria masomo yao kikamilifu. Katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana alifuta kodi kwenye malighafi zilizotumika kutengenezea taulo za kike. Je, tangu tumeondoa kodi hizo ni viwanda vingapi vimejengwa hapa ndani kwa ajili ya kutengeneza taulo hizi? Kwa sasa bei imeshuka kwa kiasi gani ili kuleta unafuu kwa wanawake na wasichana?

Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda vya kutengeneza madawa hapa nchini; Tanzania tunatumia pesa nyingi katika kuagiza madawa kutoka nje ya nchi. Ningependa kujua ni viwanda vingapi vimejengwa mpaka kufikia sasa? Serikali ina mpango gani wa kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje ili kuwekeza hapa nchini badala ya kutegemea viwanda vya nje?