Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, niombe kutamka kuwa naunga mkono hoja hii kwa asilimia 100. Napenda Waziri wa Viwanda na Biashara Mheshimiwa Joseph Kakunda (Mbunge) anipe ufafanuzi katika maeneo yafuatayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bodi ya Usimamizi wa Stakabadhi za Ghala imeleta waraka wa kununua mazao ya ufuta, soya, alizeti na choroko kwa mfumo wa stakabadhi ghalani katika kipindi cha uvunaji wa mazao hayo hususan zao la ufuta katika Wilaya ya Namtumbo bila maandalizi yoyote. Hakuna maghala yaliyoandaliwa wala Vyama vya Msingi vya Ushirika havina maandalizi yoyote. Kwani suala hili ni la dharura au ni njama za Bodi hiyo kuwagombanisha wananchi na Serikali yao?

Mheshimiwa Naibu Spika, Vyama vya Msingi vilivyopo Namtumbo vinajihusisha na zao la kimkakati la tumbaku na wananchi wana uzoefu mbaya wa kuibiwa mauzo ya tumbaku yao na hivyo wana uoga ulio dhahiri wa kupeleka ufuta wao kwa Vyama hivyo vya Msingi bila kulipwa fedha zao kutokana na walivyodhulumiwa siku za nyuma. Tunalazimisha na matokeo yake sisi viongozi wao wa kuchaguliwa tunachukiwa. Naomba Waziri mwenye dhamana na biashara usitumie nguvu ya sheria kijeshi, badala yake wasiliana mapema na Waziri mwenzako mwenye dhamana ya ushirika na kilimo mpange na kufanya maandalizi ya utekelezaji wa sheria yoyote ile ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa wakulima kabla ya msimu wa mavuno kuwadia.

Mheshimiwa Naibu Spika, biashara ya korosho kwa msimu huu unaomalizika haijaisha vizuri pamoja na uamuzi wa Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wa Serikali kununua korosho kwa bei nzuri ya Sh.3,300 kwa kilo moja. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais lakini Mawaziri mnaohusika na biashara hiyo mmetuangusha. Mpaka leo hii wananchi 76 wa Tarafa ya Sasawala, Wilaya ya Namtumbo hawajalipwa jumla ya Sh. 344,800,500/=. Wananchi hao ni wakulima waliozalisha na kuuza zaidi ya kilogramu 1,500 kwa kila mkulima. Dhana ya “kakumba” iliyotumika kuchelewesha malipo kwa wakulima hao imesababisha mateso makali kwa wakulima hao na kwa msimu huu wamenyimwa fursa ya kupalilia na kupuliza viualitifu katika mikorosho yao kwa kukosa uwezo. Tafadhali wakulima hao walipwe ili wajikimu na kuendeleza kilimo cha korosho.

Mheshimiwa Naibu Spika, wana Namtumbo kupitia Chama Kikuu cha Ushirika (SONAMCU) tumefanikiwa kumpata mnunuzi wa tumbaku, lakini kuna changamoto mbili kubwa Serikali isaidie kutatua. Moja, soko la tumbaku yetu ya Moshi (DFC) liko zaidi nchi za kiarabu kupitia mlango wa nchi ya Misri. Kwa kutokuwa wanachama wa COMESA, tumbaku yetu inaingia Misri kwa bei kubwa kutokana na ushuru unaotozwa na hivyo kushindana na washindani wetu ambao ni wakulima wa tumbaku hiyo na ni wanachama wa COMESA, ambao huingiza tumbaku yao bila kutozwa ushuru. Pendekezo, Serikali iingie “bilateral agreement” na Misri ili tumbaku yetu iingizwe nchini Misri bila ushuru kama ilivyo kwa nchi za COMESA vinginevyo turudi kuwa wanachama wa COMESA.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbili, mnunuzi wetu kampuni ya Premier Active Tanzania Ltd. wanaidai Serikali shilingi bilioni 12 zilizohakikiwa kama marejesho ya VAT. Hawarudishiwi, hivyo uwezo wa kampuni wa kuendelea kununua tumbaku ya wakulima wetu unapungua na nia yake ya kufufua kiwanda cha kuchakata tumbaku cha Mjini Songea haitekelezeki na hivyo kutunyima fursa za ajira na soko la uhakika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni biashara, hivyo Waziri shirikiana na Waziri wa Kilimo na Waziri wa Fedha na Mipango haki ya kampuni ya kulipwa marejesho ya VAT yaliyohakikiwa ipatikane ili nasi wakulima wa tumbaku tuendelee kunufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa na za kutukuka anazozifanya. Namtumbo tumeshuhudia maendeleo makubwa katika nyanja mbalimbali ikiwemo na upatikanaji wa soko la tumbaku na soya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsanteni sana. Naunga mkono hoja kwa asilimia 100. Nawasilisha.