Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. OSCAR R. MUKASA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa ya kuzungumza leo kwa niaba ya wananchi wa Biharamulo, lakini nawashukuru Wabunge wote waliotangulia kuzungumza kwa michango yao mizuri sana ya kuisimamia Serikali yetu, Wizara hii ya Elimu, Teknolojia na Ufundi. Kwa namna ya pekee pia nakupongeza Waziri na timu yako kwa kazi nzuri, lakini nina haya ya kukuambia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yako makubwa, watu tuna matumaini na wewe Mheshimiwa Waziri, lakini unaingia kwenye Wizara ambayo yako hata madogo ambayo umekuta haiwezi kuyafanya. Sasa una kazi kubwa mbele hapo! Naanza na mfano mdogo tu halafu nitakuja kwenye hotuba yenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2014 kijana aitwae Kuzima Suedi wa Biharamulo, Shule ya Sekondari Kagango, alikuwa miongoni mwa vijana kumi bora wa masomo ya sayansi Kitaifa. Akafurahi sana na sisi tukafurahi sana! Wizara ikamwalika kwenye Wiki ya Elimu mwaka 2015 hapa Dodoma, akaja mzazi, Afisa Elimu, chereko chereko nyingi! Mgeni Rasmi akatoa zawadi kwa watu wachache, akasema waliosalia akiwemo wa Biharamulo, zawadi yao ya laptop na cheque itawafuata. Mpaka leo ni kuzungushana! Afisa Elimu wa Mkoa, wa Wilaya! Hayo ni madogo tu, nakuja lingine la utangulizi kabla sijaja kwenye hotuba. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii habari ya watoto wetu wa kike wanapopata ujauzito kuondolewa shuleni, nafikiri tusilitazame kwa namna tu ya haki yao ya kusoma, nadhani tulipe picha ya ziada. Hii ni habari ya mfumo dume ambao tunauendeleza kwa kiwango kikubwa sana. Mimi najiuliza jambo moja, linapofanyika lile tendo, ni mmoja tu ambaye masikini matokeo yake yanaonekana hadharani, tumbo linakuwa kubwa. Kungekuwa na utaratibu kila mwanaume anayempa mtu ujauzito naye anavimba nundu tunaona, tungejua na mtu mwingine wa kufukuza; kwamba wa kike anafukuzwa shule, wa kiume kama ni mwanafunzi mwenzake naye anafukuzwa; kama mwanaume ni Mwalimu, ama Mbunge, ama Polisi naye anakamatwa siku hiyo kwa sababu ana nundu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunawaonea hawa kwa sababu sisi ushahidi wa kwamba tumeshiriki kwenye hilo, hauonekani mara moja, mpaka tutafute tafute, tunakaa kubishana jambo ambalo liko wazi. Hebu tuwape haki wanawake! Tutafute namna ya kuwezesha watoto wetu wa kike wasipate ujauzito; hiyo ndiyo kazi ya kwanza, lakini inapotokea bahati mbaya limetokea hilo, tusiwahukumu peke yao. Huo ndiyo ujumbe wangu wa kwanza. (Makofi/Vigelegele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja sasa kwenye mchango. Ukiangalia kitabu cha hotuba pale sura ya kwanza, picha ya kwanza kabisa, umeweka picha ya Mheshimiwa Rais na kuna nukuu ya maneno anayoyasema kuhusu elimu; anamalizia, “Serikali ya Awamu ya Tano, itajielekeza katika kuongeza ubora wa elimu inayotolewa, ni pamoja na kuongeza mkazo katika masomo ya Sayansi. Hiyo ni nukuu. Tunapozungumza hivi, Biharamulo Wilaya nzima, tuna Walimu 560; Walimu wa Sayansi 30; lakini ukiangalia ukurasa wa 19 wa hotuba hii, umeeleza, “katika udhibiti wa ubora wa elimu kwa mwaka wa fedha huu unaokuja, Wizara imepanga kufanya yafuatayo.” Yametajwa mengi pale, lakini sioni mkakati wa kushughulika na suala la Walimu wa Sayansi. Hakuna hata pale! Sasa tunaongea tu nadharia lakini hatuweki mikakati; hatuwezi kutoka hapo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dunia ya sasa kama tutaendelea na Walimu 30 wafundishe shule 18 zenye wanafunzi 8,900, Walimu 30 wa Sayansi, hatuwezi kutoka tulipo. Inabaki ni jitihada za Afisa Elimu tu kule Biharamulo masikini anahangaika, hivi tunavyoongea ana Walimu wanane wanaojitolea. Amenituma nikuombe uhakikishe kwenye mgao unaokuja kwa sababu ni walimu na wana degree na walishajitolea pale, usiwatoe pale. Usije na ubabe baadaye kwamba sisi tunakupangia uende tunakotaka sisi, wakati wamejitolea mwaka mzima pale kabla wewe hujaweza kulipa. Nitakupa majina uwaweke pale, kwa sababu wameshajitolea na wanaipenda Biharamulo na wana sababu kwa nini walijitolea bila kulipwa wakiwa Biharamulo? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije habari ya mitaala. Mwaka 2014 kama siyo mwaka 2015 mlibadilisha mitaala kwa Darasa la Kwanza na la Pili, mkaondoa masomo sita, mkaleta kusoma kuandika; KKK tatu zile. Hivi tunavyozungumza, watoto walio Darasa la Tatu, Walimu wa Kiingereza hawajui wawafundishe kuanzia wapi, kwa sababu walisoma Kiingereza mpaka mwezi wa Tano mwaka 2015, wakiwa la Pili. Mtaala mpya wa Darasa la Tatu unaochukua hali ya sasa, kwamba Kiingereza kianze Darasa la Kwanza haupo. Kwa hiyo, Walimu wanabahatisha tu; na watakaoingia Darasa la Tatu mwaka 2017 wana habari hiyo hiyo. Hatuwezi kufika kwa mtindo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninapozungumza, nina vitabu vitatu; viwili vya sayansi Darasa la Saba; kimoja cha sayansi Darasa la Sita. Nchi hii ukiwa Darasa la Sita ubongo wako una sehemu tatu, ukiwa Darasa la Saba ubongo una sehemu nne. Tutakwenda kweli? Hebu imarisha hivyo vitengo vya ukaguzi, tujue tunawafundisha nini wanafunzi kwa standard na consistence. Tutapanga mipango mikubwa kabisa, ambayo ukisoma kwenye makaratasi inaingia akilini, lakini uhalisia kule chini ni shida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu Wizara, hebu tusikie, Waheshimiwa Wabunge wamesema sana kuhusu Walimu, ni Sekta ya Elimu tu ambayo ukitaka kujenga darasa ni lazima Mtendaji wa Kata amkimbize mwananchi kuchanga, lakini sijawahi kusikia Mtendaji wa Kijji anamfuata mwananchi kumkamata achange pesa ya umeme wa REA. Tumeweka kwenye mfumo. Sijawahi kusikia Mtendaji wa Kijiji anamfuata mwananchi kumkamata achange mfuko wa barabara ili tujenga lami; hakuna! Hata hivyo anachanga na tumeweka kwenye mfumo. Ni darasa tu na nyumba ya Mwalimu ndiyo lazima wakimbizwe na Mtendaji wa Kata, hebu tuondoke kwenye ujima, tutafute tozo kwenye kodi ambazo tutakamata Sekta ya Elimu na mundombinu yake, tushughulike nayo kama Taifa, ndiyo tutaondoka kwenye hali hiyo.
Napenda pia kuongelea kidogo COSTECH, Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia. Hebu tuiwezeshe! Tunataka huo ubunifu waanze kuufanya kuanzia kwenye Shule za Sekondari, wawezeshwe waende kule; wawezeshe Walimu kutambua vipaji mapema, namna gani tutashughulika navyo, kikiwa kipaji bado kiko Biharamulo, kiko kidato cha pili, kipaji kiko kidato cha tatu, tunakijua kipo na tunapanga mpango wa kukiendeleza na kukikamata kitakapofika Chuo Kikuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi tena kwenye hoja ambayo nilitaka kuisahau kuhusiana na vitabu vyetu mashuleni. Kuna kitabu kimoja nimekutana nacho kwenye shule moja huko, kimoja kinasema tuna sayari tisa, kingine tuna sayari kumi. Sasa mimi nikachanganyikiwa, hawa watoto wakitoka hapo unataka huyu huyu ndiye aje kushiriki kwenye dunia ya sayansi na teknalojia? Haiwezekani na hatutafika kwa mwendo huo, nashukuru. (Makofi)
MHE. OSCAR R. MUKASA: Ni kengele ya kwanza?
MWENYEKITI: Ya pili Mheshimiwa