Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, naomba niunge mkono hoja. Nawapongeza Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Mheshimiwa Naibu wake, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuhamasisha viwanda. Viwanda ni ajira, kwa sababu viwanda vikifanya kazi vitatumia malighafi inayotokana na wakulima kwa maana hiyo wanawake, vijana wataweza kupata kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili viwanda viweze kufanya kazi ni lazima malighafi nyingine itokane na kilimo. Kwa maana hiyo basi, nashauri kwa sababu viwanda vinahitaji malighafi kutoka katika sekta mbalimbali kwenye kilimo, uvuvi na mifugo, ni vizuri Serikali ikaweza kushirikiana ili sekta ya viwanda pamoja na kilimo vyote vikaenda kwa pamoja. Mfano, ili viwanda vya nguo viweze kufanya kazi ni lazima pamba ipatikane, wakulima waweze kulima pamba na pamba iweze kupelekwa viwandani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye viwanda vya viatu tunapata mabegi, viatu, kwa hiyo, ngozi itatokana na wagufaji wa ng’ombe na kadhalika. Pia kwenye uvuvi tunapata viwanda vya samaki, kwa mfano, vile viwanda vilivyoko Mwanza vinatokana na uvuvi. Kwa maana hiyo, viwanda pamoja na sekta ya kilimo, ufugaji na uvuvi ni vitu ambavyo vinatakiwa viende sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, katika viwanda vya mafuta ni lazima tuwekeze kwenye kilimo cha mchikichi, alizeti na kadhalika. Katika ujenzi wa viwanda ni muhimu sekta ya kilimo nchini ikazingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanikisha mambo haya yote tukiwahamasisha wananchi wakaweza kulima kilimo cha mchikichi na Serikali ikawasaidia wananchi kuwapelekea pembejeo na miche naamini tutaweza kufanya vizuri katika zao hili na viwanda vya mafuta vitaweza kufanya kazi kutokana na malighafi tunayoizalisha sisi wenyewe kupitia kwa wakulima wetu. Kwa mfano, katika Mkoa wa Kigoma, naomba Serikali iwasaidie wananchi wa Kigoma kupata miche ya michikichi na pembejeo ili waweze kulima kilimo chenye tija katika zao la mchikichi na baadaye tuweze kupata viwanda vinavyoweza kutengeneza mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote niendelee kuomba Serikali iweze kuhamasisha wawekezaji wa ndani na nje kwenda kuwekeza viwanda Kigoma ili wananchi wakilima watapata sehemu ya kuuzia lakini pia ajira zitaweza kuongezeka. Naomba Serikali iweze kuongeza bajeti ya Wizara ya Biashara na Wizara ya Kilimo kufikia malengo tuliyojiwekea ya ujenzi wa viwanda. Bajeti ya Wizara ya Viwanda kwa kweli ni ndogo. Kwa hiyo, naomba Wizara ya Viwanda na Biashara iweze kuongezewa bajeti ili iweze kufanya vizuri katika dhana ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna moja nililotaka kulizungumzia kuhusu OSHA. Naomba Serikali iandae mpango wa blue print ili tuweze kufanya vizuri katika nyanza hii kwa sababu malalamiko yamekuwa ni mengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu SDL wanayokatwa wafanyabiashara na wenye viwanda yote inapelekwa kwenye ujuzi. Naomba kiasi hiki kinachokatwa kiweze kurudishwa kipelekwe Wizara ya Viwanda na Biashara kwenda kuwasaidia watu wa SIDO na TIRDO ili kuongeza uwezo katika taasisi hizi. Kwa maana hiyo, naomba kabisa hayo yote niliyoyasema yaweze kuzingatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa naomba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)