Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

Hon. Julius Kalanga Laizer

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Monduli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Viwanda na Biashara

MHE. JULIUS K. LAIZER: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea na maeneo mengine, naomba Waziri wakati anakuja kuhitimisha anipe maelezo kuhusu Mradi wa Magadi wa Engaruka. Wananchi wetu wametoa eneo la kubwa sana karibu eka 100,000 kwa ajili ya mradi huu na katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi pamoja na Mpango wa Maendeleo wa 2015-2020 wamesema mradi huu ni wa kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma katika kitabu cha Waziri katika ukurasa wa 17 maneno ya Waziri anasema: “Mradi wa Uchimbaji Magadi Soda katika Bonde la Engaruka, Wilaya ya Monduli unahusu ujenzi wa kiwanda cha kuzalisha magadi soda tani milioni moja kwa mwaka kwa ajili ya matumizi ya viwanda hususan vya dawa, vioo na sabuni. Utafiti wa kina (techno-economic study) utakaojumuisha utafiti wa maji safi (detailed hydrological study), mazingira (ESIA), na upembuzi yakinifu (feasibility study) umeanza kufanyika”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana ilikuwa ni bajeti ya Wizara ya Uchukuzi lakini hata kilometa moja ya lami kwenda kwenye Mradi wa Engaruka kilometa 70 kutoka Mto wa Mbu kwenye bajeti ya Serikali hakuna. Sasa mimi nataka niulize hivi ushirikiano wa Wizara za Serikali katika kutekeleza miradi ya maendeleo uko wapi? Kwa nini Wizara ya Biashara inazungumza ya kwake na Wizara ya Ujenzi inazungumza ya kwake. Unatekelezaji Mradi wa Engaruka bila miundombinu wenzeshi, maji lakini tunasema ni mradi wa kimkakati. Mmewazuia wananchi wetu wasiendeleze maeneo yao katika eneo lile hata fidia hamjalipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Wizara ituambie barabara ya kutoka Mto wa Mbu kwenda Engaruka ili eneo lile liwe accessible, muweze kufika unaanza lini? Kama mradi huu mnashindwa kuutekeleza tuwaachie wananchi wetu waanze kufuga ng’ombe wao katika maeneo yale. Tumetoa maeneo yale kwa bei kutupwa Sh.200,000 kwa eka moja lakini mpaka leo hamjaanza. Leo hakuna hata mradi wa barabara katika eneo lile, halifikiki, ni mwekezaji gani ataenda kufanya investment Engaruka wakati barabara ya kufika tu haipo? Ni miujiza gani yule anayefanya utafiti kule kuchukua yale magadi anachukua material yake aje apeleke kwenye bandari ya Dar es Salaam asafirishe? Let us be serious katika miradi hii, kama mradi huu umefeli tuuache. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo niende katika eneo la ngozi. Amesema kaka yangu hapa kwamba katikati ya Bunge hili tuna watu tofauti tofauti, lakini sisi tunaotokana na jamii ya ufugaji maisha yetu ni ng’ombe, uchumi wetu ni ng’ombe, kuvaa kwetu ni ng’ombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka nitofautiane na baadhi watu. Mnasema mnazuia ngozi isiende nje kwa sababu ya kulinda viwanda vya ndani lakini uzalishaji wa ngozi ya ng’ombe kwa mwaka ni milioni 3,500,000 lakini viwanda vyetu vya ndani havichukui ngozi hata 200,000, kwa nini mnatengeneza gharama ya kulinda viwanda vya ndani kwa gharama zetu sisi wafugaji wa nchi hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wenye viwanda na vinavyofanya kazi ni karibu vinne tu nchi nzima, ukipeleka kuuza ngozi kwao wananunua Sh.300 kwa piece mpaka Sh.1,200, lakini yeye aki-process ile ngozi anakuuzia kwa Sh.100,000, haki iko wapi katika eneo hili? Kwa sababu ninyi mmeweka kodi katika usafirishaji wa ngozi nje na kwa sababu hakuna mahali pa kuuza wao wameamua kutokununua kwa bei ya kawaida kwa sababu wanajua hakuna mahali pa kupeleka kwa sababu mmetuwekea kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakubaliana kulinda viwanda vya ndani lakini nataka Waziri aniambie unalinda viwanda vipi ambavyo hauna? Unalinda kiwanda kipi cha ngozi ambacho kinaweza kuchukua ngozi 3,000,000 kutoka kwa wafugaji wa nchi hii? Kwa nini mnatengeneza gharama ambayo inatuumiza sisi wafugaji? Tunataka Serikali iruhusu upelekaji wa ngozi nje mpaka viwanda vya ndani vitakavyotengemaa ili tuweze kupata mahali pa kuuza, sasa hivi hakuna mahali pa kuuza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumza hapa Mbunge mmoja kuhusu 10% ya wet blue lakini 80% ya ngozi ghafi zimewekwa ili kulinda viwanda vya ndani na viwanda vyenyewe vya ndani havipo. Tunaomba Serikali kwa unyenyekevu kabisa isivilinde viwanda vya ndani kwa gharama za wafugaji wakati ngozi tunazalisha sisi hatuna mahali pa kuuza kwa sababu viwanda vya ndani havinunui na mmezuia visiende nje kwa sababu mmeweka kodi kubwa. Ni muhimu kuliangalia jambo hili ili kuwasaidia wafugaji wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, ukiangalia kama ambavyo wengine wasema tatizo hili la ngozi hata sera na usimamizi wa viwanda hivi haupo. Kwa mazingira kama haya lazima ngozi yetu ikose thamani. Sasa hivi wanasema soko limepatikana Nigeria kwa sababu wao wanakula ngozi lakini kama Serikali inaona kwamba soko hilo ni kubwa kwa nini isingewasaidia wafugaji kupata soko la uhakika kuliko ku- discourage exportation wakati ndani ya nchi hakuna uwezo wa ku-accommodate ngozi zilizopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali itoe maelekezo kwenye taasisi zake kama Majeshi na Polisi, bidhaa zinazotengezwa na viwanda vyetu hasa viatu wanunue. Kuna kiwanda kinaitwa Bora wanasema wanazalisha viatu vizuri sana lakini bado Serikali katika Majeshi yetu ya Polisi na Jeshi la Kujenga Taifa tunaagiza viatu nje. Kama hatuwezi kuthamini cha kwetu unategemea nani anunue bidhaa za ndani kama sisi Serikali hatununui bidhaa zinazozalishwa na viwanda vya ndani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kulinda viwanda vya ndani ni pamoja na kutafuta soko la ndani na Serikali kupitia Majeshi inaweza ikawa ni sehemu ya soko kwa viatu vinavyotengenezwa ndani ya nchi. Wenyewe hatununui, kwa nini tusifanye kama Waziri wa Nishati alivyoagiza kwamba trasfoma zote za TANELEC zinunuliwe kuliko kuagiza nje. Tukienda huko tutakuwa tumesaidia viwanda vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo tunaliona, tatizo kubwa ambalo viwanda vyetu linakumbana nal ni kodi kubwa katika bidhaa na mitambo ya kujenga viwanda vya ndani, vilevile kodi kubwa ya umeme. Mimi nilikuwa nafikiri katika maeneo ambako tuna viwanda vya ndani tuondoe kodi kwenye umeme ili viwande vile viweze kuzalisha na kuleta faida kwa taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)