Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kutoa mchango wangu katika hoja hii muhimu ya Wizara ya Ujenzi inayosimamia miundombinu ya barabara na mawasiliano nchini.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa afya na uzima na kupata nafasi ya kuwa mmojawapo wa Waheshimiwa Wabunge kutoa mchango wa kuboresha kazi nzuri inayofanywa na Serikali ya hii ya CCM ya Awamu ya Tatu kupitia Wizara hii ya Ujenzi. Nachukua nafasi hii kuipongeza Serikali kwa utekelezaji wa miradi mikubwa ya miundombinu ya usafiri nchini. Naipongeza Serikali kwa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) ya reli ya kati toka Dar es Salam mpaka Kigoma.

Mheshimiwa Spika, nashukuru Serikali kwa sababu reli hii ujenzi wa Awamu ya Kwanza toka Dar es Salam mpaka Morogoro unakamilika mwaka huu Desemba, 2019 na kwa kiasi kikubwa barabara hii inapita katika Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, Jimbo ambalo naliongoza mimi. Reli itakuwa na msaada mkubwa wa kuinua hali ya vipato na uchumi wa wananchi wa Morogoro Kusini Mashariki na Morogoro kwa ujumla kwa kuwa itapunguza gharama ya usafiri wa mazao ya wakulima wa Ngerengere, Mikese, Kinole, Tegetero, Tununguo, Mkuyuni, Kiroka, Tomondo, Mkulazi na Vijiji vya Kata zote za Morogoro kwa ujumla na kupunguza gharama za usafiri na kuongeza vipato vya wananchi wa Morogoro.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio hayo ya Serikali ya CCM inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Magufuli kwa kuweka katika bajeti barabara ya Bingwa - Kisaki kuanza kwa ujenzi na kuanza kilometa 50 kwa kiwango cha lami. Naipongeza Serikali kwa sababu ni sikivu, baada ya kusikiliza maombi yangu ya ujenzi wa barabara kuanza ujenzi kila Bunge la bajeti tangu kuingia katika Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi na shukrani hizo kwa Serikali kuiweka katika bajeti barabara ya Bingwa - Kisaki lakini kiasi kilichotengwa ni kidogo sana cha shilingi milioni mia moja arobaini na tano (145,000, 000) kwa kujenga barabara ya kilometa hamsini ni kiasi kidogo sana ambacho hakiwezi kutosha kulipa hata fidia tu kwa wananchi waliopisha ujenzi wa barabara hii ya Bingwa Kisaki. Ushauri wangu kwa Serikali kuongeza kiwango cha fedha katika bajeti ya ujenzi wa barabara hii ya Bingwa - Kisaki ili ujenzi wake uanze mwaka ujao wa fedha unaanza mwezi Julai baada ya bajeti hii kupita.

Mheshimiwa Spika, kiasi hiki ni kidogo ambacho pia hakiwezi kutosha kulipa mkandarasi malipo ya awali ya asilimia 15 kwa mujibu wa sheria. Naomba Serikali iongeze fedha ili ujenzi uanze.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili naomba Serikali kutupatia minara ya mawasiliano katika Kata ya Tegetero, Rudewa, Seregete, Mkulazi, Tununguo, Kidugalo na Matuli na Vijiji vyote vya Kata hiyo pamoja na Vijiji vya Luholole, Mwarazi na Kibuko Kata ya Kibuko. Pia mnara katika Vijiji vya Newland Lubungo, Mhunga Mkola katika Kata ya Mikese. Pia naomba ujenzi wa madaraja katika Mto Ruvu kuunganisha Tarafa ya Mvuha na Tununguo kupitia Mbarangwe, Tununguo mpaka Kisanga Stendi. Pia naomba daraja la kuunganisha kati ya Kata ya Matuli na Kidugalo kwenye Mto Ngerengere.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.