Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, naomba nianze mchango wangu kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na afya njema. Pia, nachukua fursa hii kuwapongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri, Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu, Wenyeviti wa Bodi zote zilizoko kwenye Wizara hii na Wakurugenzi Watendaji wote wa Taasisi zote zilizopo kwenye Wizara hii kwa kazi kubwa ya kumsaidia

Mheshimiwa Rais katika kuwatumikia Watanzania. Nawaombea dua kwa Mwenyezi Mungu awape umri mrefu ili waweze kutimiza ndoto ya Mheshimiwa Rais ya kuona Tanzania mpya. Mwenyezi Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Nachingwea – Liwale ni barabara muhimu sana kwa Wilaya ya Liwale, kwani ndiyo barabara pekee inayoiunganisha Wilaya ya Liwale na Makao Makuu ya Mkoa wa Lindi. Naishukuru Serikali kwa kuanza upembuzi na usanifu wa kina kwa barabara hii. Nashauri kazi hii iambatane na utafutaji wa fedha ili kuweza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Nangurukuru – Liwale ni barabara ya kiuchumi kwa Wilaya ya Liwale. Usafirishaji wa mazao kutoka Liwale hadi Dar es Salaam kupitia Lindi kuna kilometa zaidi ya 750 ukilinganisha na kilometa 500 ukipitia barabara ya Liwale to Nangurukuru. Hivyo, utaona umuhimu wa barabara hii ni mkubwa sana kwa uchumi wa Wana-Liwale na nchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, nashukuru tena kuona kwenye bajeti hii kumetengwa shilingi milioni 300 ili kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kama ilivyo barabara ya Nachingwea – Liwale. Hii pia Wizara ianze kutafuta fedha ili hatimaye nayo pia iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa mawasiliano, nashukuru kwa kupatiwa mawasiliano kupitia kampuni ya Halotel kwa kutujengea minara kwenye kata tisa ambapo sasa kwa kiwango kikubwa upo unafuu kidogo, lakini bado kuna shida ya mawasiliano katika Vijiji vya Ndapata, Mkutano, Kikulyungu, Nahoro, Kipelele, Mtungunyu na Mtawatawa. Vijiji hivi hali ni mbaya sana katika mawasiliano ya simu.

Mheshimiwa Spika, Reli ya TAZARA bado ni reli muhimu sana kwa nchi yetu. Kwa upande wa Zambia wao kwa reli hii siyo kipaumbele chao tena pamoja na kuwa uongozi wa reli hii kwa kiasi kikubwa unamilikiwa na upande wa Zambia. Wazambia wamekuwa wakifanya vitendo vya kuhujumu reli hii kwa makusudi. Hivyo basi, imefika wakati Serikali yetu ifanye mapitio ya Sheria ya Uendeshaji wa Reli ya TAZARA. Hatua hii ni muhimu na iende sambamba na kuifutia madeni au kuipa mtaji ili iweze kujiendesha.

Mheshimiwa Spika, Chuo cha Mabaharia (DMI) ni chuo kilichosahauliwa kwa muda mrefu ndiyo maana uwepo wa chuo hiki hata kwa jamii hautambuliwi pamoja na kuwa nchi yetu imezungukwa na bahari na maziwa makuu. Sekta ya Uvuvi na Usafiri wa Majini una mchango mdogo katika nchi yetu kutokana na kupuuza chuo hiki muhimu kwa uchumi wa nchi yetu. Nashauri Serikali ianze sasa kuimarisha chuo hiki ikiwa ni pamoja na kukitangaza, kwani sasa chuo hiki hakitambuliwi katika jamii ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, Chuo cha Usafirishaji (NIT) ni chuo muhimu sana kwa sasa, hasa kwa kuwa nchi yetu inakwenda kuimarisha Sekta ya Uchukuzi kwa kujenga reli ya kisasa, ununuzi wa ndege na ujenzi wa meli kwenye maziwa makuu. Hivyo basi, Serikali ione umuhimu wa kuimarisha chuo hiki, kwani ndiyo chuo kinachokwenda kupika wataalam katika Sekta ya Uchukuzi. Chuo hiki ni lazima kipewe fedha za kutosha ili kiweze kujiimarisha kupata wataalam.

Mheshimiwa Spika, sera ya kuunganisha mikoa yetu kwa barabara za lami ni jambo linalopaswa kupewa kipaumbele kwa mikoa yote kwani bado kuna mikoa ambayo hadi leo haijaunganishwa siyo tu kwa barabara za lami, hata kwa barabara za changarawe. Mfano, Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Lindi, mikoa hii, pamoja na kuwa mikoa jirani lakini pia ni mikoa muhimu sana kwa kukuza uchumi wa mikoa hiyo miwili. Hivyo, naiomba Serikali kufanya kila iwezavyo kutekeleza sera hii ya kuunganisha Mikoa ya Lindi na Morogoro kwa barabara ya Liwale – Mahenge (Ulanga).

Mheshimiwa Spika, Uwanja wa Ndege wa Lindi, pamoja na kuwa moja ya viwanja vya zamani nchini, hakijapewa kipaumbele. Hii ni kudumaza maendeleo ya Mkoa wa Lindi sambamba na Bandari ya Lindi. Nashauri Bandari ya Uvuvi ya Kanda ya Kusini ikajengwe Lindi ili kuinua uchumi wa Mkoa wa Lindi.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo yote hapo juu, naunga mkono hoja hii muhimu kwa uchumi wa nchi yetu.