Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Waziri pamoja na timu yake yote kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, ndani ya Wilaya ya Lushoto hasa katika Jimbo la Lushoto, barabara za Lushoto siyo siasa tu, ni zaidi ya maisha ya watu hasa barabara ya Mlalo – Ngwelo – Mlola – Makanya - Mlingano - Mashewa yenye kilometa 57. Barabara hii nimeizungumzia kwa muda mrefu sana kuwa ni barabara ya kiuchumi yenye wakulima wengi wanaozalisha mazao ya kibiashara.

Mheshimiwa Spika, kwa masikitiko makubwa, barabara hii inapigwa danadana na TARURA wanasema ipo TANROADS nao TANROADS wanasema ipo TARURA. Naomba Mheshimiwa Waziri barabara hii muichukue iwe ya TANROADS ili wananchi wa maeneo hayo niliyotaja waweze kunufaika. Kama hili Mheshimiwa Waziri haliamini, atume timu yake iende ili ajue ukweli wa haya niliyoyaandika.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, kuna barabara ya kuanzia Dochi - Ngulwi – Mombo. Kama unavyofahamu Lushoto kuna barabara moja kubwa tu na barabara hii ni nyembamba na imejaa mawe yanayoning’inia juu ya barabara na ndiyo sababu mvua ikinyesha mawe yanaporomoka na kuziba barabara.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2017, barabara hii iliziba kwa siku zaidi ya 21 (wiki tatu) hali iliyosababisha usumbufu mkubwa sana na kupelekea wakulima wa mboga mboga na matunda kupata hasara kubwa sana pamoja na huduma za jamii kukosekana. Niiombe Serikali yangu Tukufu, kwa kuna kuna barabara hii ya Dochi - Mombo kilometa 16 tu itengenezwe ili iwe barabara mbadala lakini siyo kwa kupitika tu ila pia ni barabara yenye mazao mengi na pia kuna wananchi wengi wanaoishi katika maeneo hayo na kwa sasa wanakosa huduma za afya pamoja na za kijamii. Pamoja na hayo, barabara zote hizi mbili siyo lazima ziwe na lami. Wananchi wanataka zipitike tu kwa mwaka mzima yaani ziwe za changarawe tu.

Mheshimiwa Spika, pia kuna barabara ya TANROADS inayoanzia Nyasa – Mshizi - Gare - Magamba. Barabara hii kwa kweli nimshukuru Meneja wa TANROADS Ndugu Ndumbali kwa kazi kubwa. Barabara hii ina maeneo ya kujenga madaraja mawili; Daraja la Mshizi na Daraja la Kongei pamoja na kuweka zege maeneo hatarishi kama vile Mlima wa Yamba. Hili nalo niiombe Serikali yangu itenge fedha ili barabara hii iweze kurekebishwa na kujenga hayo madaraja mawili.

Mheshimiwa Spika, pia niendelee kuipongeza Serikali yangu tukufu kwa kutupatia kilometa 1 kila mwaka kwa barabara iliyoanzia Magamba kwenda Mlola na Magamba kwenda Mlalo. Niiombe Serikali yangu ituongezee angalau kilometa 3 ili ziwe 4 ili kuharakisha maendeleo ya Wilaya ya Lushoto na huduma kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, kama mnavyofahamu kuwa Tanga ni Jiji lakini tunayo changamoto za uwanja wa ndege. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu iupanue Uwanja wa Ndege wa Tanga ili ndege kubwa ziweze kutua.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hayo, mwaka jana tuliomba Bombardier iweze kutua Tanga na Waziri alikubali lakini mpaka leo ndege haijatua. Naomba nikumbushie tena kuwa Bombardier itue Tanga sasa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia 100.