Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hii kwa asilimia 100 na niombe yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, mkongo wa Taifa. TTCL na Tume ya TEHAMA iimarishe kwa kuwekeza mtaji wa kutosha ili sekta ya mawasiliano ichangie zaidi katika uchumi wa Taifa na ukuaji wa sekta ya viwanda.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya yangu ya Namtumbo kuna maeneo yenye wakazi wengi lakini hayana mitandao ya mawasiliano ya simu. Ni maeneo yote ya Kata za Msindo, Mgombasi na Lisimonji. Aidha, vijiji vya Mtewamwachi, Likusanguse, Limamu na Mtakuja navyo havina usikivu wa mawasiliano ya simu. Naomba Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote utusaidie kukamilisha na kufungua mawasiliano ya simu na data katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuisemea barabara ya kuunganisha Mikoa ya Ruvuma na Morogoro ya Lumecha - Kitanda-Londo - Kilosa Kwa Mpepo – Lupiro - Ifakara - Mikumi. Mheshimiwa Rais ameliisemea barabara hii wakati akifungua Daraja la Kilombero na Kituo cha Mabasi cha VETA cha Namtumbo au tuseme alipokuwa kwenye ziara Mkoani Ruvuma kuanzia tarehe 4 hadi 09 Aprili, 2019 lakini katika kitabu naona shilingi milioni 80 tu ambazo haziwezi kujenga barabara kati ya Lupilo- Kilosa Kwa Mpepo-Londo - Lumecha kupitia Kitanda. Hii ni sawa kweli? Namwomba Mheshimiwa Waziri aliangalie suala hili.

Mheshimiwa Spika, kwa wana Ruvuma barabara ya kuunganisha Mikoa hii inaanzia Kilosa Kwa Mpepo - Londo - Kitanda. Kipande hiki cha kilometa 121.5 hivi ndiyo inaweza kuitwa kiungo cha mikoa hiyo miwili. Naomba fedha zilizotengwa zishughulikie kipande hiki cha barabara vinginevyo tafsiri ya bajeti hii ni kujenga barabara ya Mikumi - Ifakara - Mlimba na kuelekea Njombe badala ya barabara yetu wana Namtumbo.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kutufikiria wana Namtumbo kwa barabara zetu za kutoka Naikesi - Mkonga na Namtumbo – Likuyu –Namabengo – Mbimbi - Libango - Namtumbo na nyinginezo kwa kuzitengea fedha za matengenezo hususani lami nyepesi ya mita 100 katika barabara ya Naikesi - Mtonya.

Mheshimiwa Spika, aidha, kupitia Waziri, nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wetu mpendwa kwa kuitengea fedha ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara ya Mtwarapachani - Likusanguse - Nalasi jumla ya shilingi milioni 450 na hivyo kumfanya Mhandisi Mshauri aendeleze na kukamilisha kazi iliyoanza.

Mheshimiwa Spika, TARURA na TANROADS, taasisi hizi mbili zinapata fedha kutoka Hazina na Road Fund Board (RFB) kwa kuwa taasisi hizi ni za kushughulikia barabara. Naomba taasisi zote za TANROADS, RFB na TARURA ziwe chini ya usimamizi wa mamlaka moja ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Kuziweka taasisi hizo katika Wizara mbili tofauti inaongeza gharama za utawala na uendeshaji na kugawana wataalam hususani Wahandisi wa sekta ya barabara wachache tulionao nchini. Hoja za kupandisha hadhi barabara pamoja na kuiongeza TARURA mgao wa fedha za Mfuko wa Barabara zitaondoka ikiwa taasisi hizi za TARURA na TANROADS zitawekwa chini ya Wizara moja yenye wajibu wa kujenga na kukarabati barabara.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kunipa pumzi. Aidha, nimpongeze Waziri na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuiwezesha mihimili ya utawala na Bunge kufanyakazi kwa umakini na kwa umoja kwa kiwango cha kutuwezesha wana Namtumbo kuanza kuona maendeleo katika sekta mbalimbali hususani barabara, mawasiliano ya simu, umeme na kadhalika. Ahsanteni sana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia 100 na naomba kuwasilisha.