Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Spika, niipongeze sana Wizara hii na Mheshimiwa Waziri kipekee na Naibu Mawaziri wake kwa kazi nzuri wanayofanya ili kuunganisha nchi yetu kwa barabara, reli na kimawasiliano, hongereni sana.

Mheshimiwa Spika, barabara yangu ya Ikungu - Malampaka ilitengewa bajeti ya shilingi milioni 800 ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami mwaka wa fedha 2018/ 2019 lakini ujenzi huu haujaanza mpaka leo. Katika bajeti ya 2019/2020, Wizara imetenga shilingi milioni 300 kwa ajili ya barabara hii. Je, ni lini sasa barabara hii itaanza kujengwa ikiwa tumebakia na mwezi mmoja tu mwaka wa fedha 2018/ 2019 uishe? Barabara hii ni muhimu sana kwa ajili ya kuunganisha na bandari kavu ya Malampaka ambayo itakuwa ni lango la bidhaa na biashara kwa Mikoa ya Simiyu, Mara na maeneo ya Kenya.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ulilenga kuboreshwa kwa barabara na kurahisisha usafiri ili uwe wa haraka zaidi na kufanya watu na usafirishaji mizigo ifike mapema zaidi na hatimaye kuchochea shughuli za uchumi ziende kwa kasi zaidi. Cha kushangaza muda wa kusafiri kutoka Dar es Salaam mpaka Mwanza umebaki kuwa ni uleule kama wakati ule ambapo barabara hazikuwa za lami. Mabasi yalikuwa yanatoka saa 11.00 alfajiri Dar es Salaam kabla ya lami na kufika Mwanza saa 5.00 au saa 6.00 usiku. Sasa tuna barabara za lami lakini muda unaotumika kwa mabasi kusafiri bado ni uleule na wakati mwingine ni zaidi.

Mheshimiwa Spika, sasa barabara za lami zimetusaidiaje ikiwa hazijapunguza muda tuliokuwa tunapoteza barabarani? Ni shughuli ngapi za kiuchumi zinachelewa? Ni fedha kiasi gani zinapotea kwa kupoteza muda barabarani? Wizara hii inafanya kazi nzuri lakini tafuteni ufumbuzi wa tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja.