Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, Wizara hii ina umuhimu sana kwa uchumi wa Taifa letu. Hakuna nchi iliyoendelea duniani bila uwepo wa mawasiliano ya barabara, reli, anga na majini. Katika nchi inayoendelea kama Tanzania ambayo uchumi wake unategemea kilimo kwa asilimia 75 ni muhimu sana usafiri wa reli na barabara ukawepo ili kufikisha mazao sokoni.

Mheshimiwa Spika, pamoja na ujenzi unaondelea ni muhimu sana barabara zijengwe kwa kiwango kinachostahili. Ikumbukwe kuwa zaidi ya 40% ya fedha za miradi yote imewekezwa kwa Wizara hii, hivyo, ni muhimu sana fedha hizi zikatumika ipasavyo. Kibaya zaidi fedha hizi zinanunua malighafi za ujenzi kutoka nje huku tukiwa na malighafi hizi kutoka nchini kama vile chuma cha Liganga ambacho kingesaidia mataruma ya reli na pia makaa ya mawe na madini mengineyo.

Mheshimiwa Spika, ni jambo la ajabu kuona kuwa ATCL haina sera madhubuti na mpango mkakati, jambo linalosababisha shirika kuendelea kupata hasara kubwa. Pamoja na mpango wa biashara bado tumeshindwa kushika soko la utalii kutoka nchi mbalimbali kutokana na kutokuwa na uwanja wa ndege maeneo ya karibu na mbuga kama Serengeti hivyo, watalii hao kwenda Kenya na baadaye kusafirishwa na magari hadi mbugani, jambo linalotukosesha mapato mengi. Nashauri uwanja wa ndege wa Seronera ukarabatiwe ili watalii watue hapo na iwe rahisi kwenda kutalii.

Mheshimiwa Spika, kuna kilio kikubwa cha wananchi wa Dar es Salaam, hasa Ubungo - Kibamba, waliovunjiwa nyumba na cha ajabu tunaelezwa barabara ya Dar es Salaam – Chalinze (Express Way), haitajengwa kwa sasa. Jambo hili limetonesha vidonda kwa wale waliovunjiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu Uwanja wa Ndege wa Msalato umekuwa ukizungumziwa lakini cha ajabu pamoja na Makao Makuu kuhamia Dodoma uwanja umekuwa ni huu ulio katikati ya Jiji na ni mdogo. Mwanzoni tuliambiwa ni wa muda tu lakini tumeshuhudia ukiendelea kupanuliwa na watu wakivunjiwa nyumba zao. Hivyo, nataka kujua ile ahadi ya Uwanja wa Msalato ni lini itatimia?

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Hali ya Hewa nayo imekuwa na shida kubwa sana. Sielewi ni vifaa vya kizamani au ni utaalam hafifu. Inashangaza tunapopewa forecasts ambazo haziendani na uhalisia. Mfano kile Kimbunga Keneth kilivyotangazwa na hali ilikuwa sivyo kabisa, matokeo yake madhara yakawa mikoani na si kule Mtwara. Ni aibu kubwa sana katika ulimwengu huu wa digitali bado forecasts zinakuwa hazieleweki. Iko siku tutaambiwa kutakuwa na jua kali ghafla mnapata mvua za mafuriko, hivyo inakuwa janga kubwa na vifo.

Mheshimiwa Spika, kule Marangu kuna barabara kutoka Mtoni – Kirua, ujenzi ni kama umesimama lakini cha ajabu hata zile sehemu ambapo ujenzi umekamilika madaraja hayajajengwa. Hali hii ni hatari sana kwa kuwa barabara ni pana lakini kwenye madaraja ni nyembamba kuweza kupitisha gari moja tu, hivyo kwa madereva wageni kuna hatari ya kupata ajali. Mfano Mto Ghona/Wona, Mto Makoa, kwa kifupi mito yote toka Marangu Mtoni mpaka Kilema madaraja yake ni tishio kwa watumiaji.

Mheshimiwa Spika, ni wazi kuwa Dar es Salaam ni jiji kubwa kuliko majiji yote na lenye kuiingizia nchi pato kubwa sana. Hali ya msongamano Dar-es-Salaam inapoteza kwa kiasi kikubwa pato hilo. Haiwezekani gari kutoka Ubungo hadi Kibaha kilometa 30 litumie saa 2 – 3 wakati kwa hali ya kawaida ni dakika 30 – 45. Hali hii imekuwa mbaya zaidi kutokana na ujenzi wa barabara unaoendelea. Hivyo basi, ni muhimu sana malori ambayo ndiyo chanzo kikubwa cha foleni kutokana na ama kuharibika na ukubwa wake yatafutiwe njia mbadala au dry port eneo la Mlandizi au Ruvu kupunguza adha hii kubwa ili kuongeza pato la Taifa.

Mheshimiwa Spika, suala la mawasiliano ya simu ni muhimu sana. Hivyo ni muhimu miundombinu ya minara iboreshwe ili kupata usikivu mzuri. Imekuwa ni kilio kikubwa kwa tatizo la usikivu wa simu kutoka eneo moja kwenda lingine.