Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Kwa kweli nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa hii ya kuwa hai na kuchangia leo hii. Kwa sababu muda ni mfupi, naomba sana nianze na suala moja la taasisi mbili za TARURA na TANROADS. Kwa hivi sasa kwa mfumo tulionao, TARURA iko chini ya TAMISEMI na TANROADS iko chini ya Wizara hii tunayoiongelea leo.

Mheshimiwa Spika, hawa wote wanapata fedha kutoka Mfuko wa Barabara unaosimamiwa na Bodi ambapo mgawanyo wake TANROADS wanapata asilimia 62.46, TARURA wanapata asilimia 26.77, Ujenzi wanapata asilimia 6.94, TAMISEMI wanapata asilimia 2.97 na mfuko wenyewe wa barabara kwa maana ya taasisi inayosimamia inapata asilimia 0.86.

Mheshimiwa Spika, wajibu wa road fundboard ni pamoja na kusimamia au kufuatilia utekelezaji au matumizi ya fedha zinazokwenda katika taasisi ya TARURA, Ujenzi na TANROADS. Wakati huo huo TAMISEMI wanapata hiyo asilimia 2.97 kwa ajili ya ufuatiliaji wa miradi hiyo hiyo na Ujenzi wanapata asilimia 6.94 kwa ajili ya ufuatiliaji wa ujenzi wa barabara hizo hizo.

Mheshimiwa Spika, kwa maana nyingine Ujenzi, TAMISEMI na mfuko wa barabara wote wanasimamia barabara zinazoshughulikiwa na TANROADS na TARURA. Naomba, ni mawazo yangu kwamba TANROADS na TARURA wawe chini ya Wizara moja na kwa sababu Wizara inayohusika na barabara ni Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, basi ningependa TARURA maadam imeshaundwa chombo kinachojitegemea, basi sasa isimamiwe na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano badala ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii haina maana kwamba D by D itakuwa imekufa, hapana. Bado watu wa TAMISEMI suala la eyes on, hands off litabakia pale pale, linaendelea. Ni kama ilivyo katika barabara za TANROADS, nazo zinasimamiwa na TAMISEMI hata kama hawapati fedha na wala hawawajibiki, kuisimamia lakini wana eyes on katika shughuli zote zinazofanywa na TANROADS. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba vilevile eyes on iendelee na watu wa TAMISEMI kwa maana ya Wizarani pamoja na mkoani katika barabara za TANROADS wanavyofanya sasa na wafanye sasa na TARURA, lakini suala la usimamizi lirudishwe liwe chini ya Wizara moja, chini ya Waziri mmoja ambaye ni Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Hii itasaidia mambo mengi. Kwanza hizi hela zote za usimamizi asilimia 6.94, 2.97 na 0.86 zote zitaungana zitafanya kazi kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, halafu na mgawanyo wa bajeti hiyo suala la asilimia 70 kwa 30 halitakuwa na mvutano tena na wala hatutakuwa na mvutano tena wa kusema kupandisha barabara hadhi lakini sababu tu ni kutaka hizo barabara zishughulikiwe na TANROADS. Mvutano huo hautakuwa tena kama taasisi zote hizo mbili zitasimamiwa na Wizara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuliongea hilo, naomba tena upande wa mawasiliano TTCL, Mkongo wa Taifa, Tume ya TEHAMA, pamoja na Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote. Taasisi hizi nimeangalia kwenye vitabu vya Mheshimiwa Waziri, sijaona kama amezipa mtaji wowote. Tatizo la taasisi hizo ni mtaji. mimi nina uhakika taasisi hizi zina wataalam wa kutosha, lakini hawafanyi kazi yoyote kwa sababu hawana mtaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri, ni vizuri kutoa zile trilioni kwa upande wa uchukuzi pamoja na ujenzi lakini upande wa mawasiliano hajapewa fedha ya kutosha au hajaomba fedha ya kutosha. Ni fedha ndogo sana na kwa hiyo, haiwezi kufanya kazi kubwa inayotakiwa katika kutuimarishia mawasiliano na tunashida kubwa katika uimarishaji wa mawasiliano pande zote; mawasiliano ya simu pamoja na data. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana taasisi hizo zipate fedha za kutosha, zipate mtaji ili ziweze kujiendesha na kushindana na taasisi nyingine.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)