Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu kabisa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Manaibu Waziri pamoja na watumishi wote wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya tunashuhudia jinsi ambavyo kazi kubwa inafanyika katika Taifa hili, barabara zinajengwa, flyover zinajengwa lakini barabara mbalimbali za mikoa zinajengwa. Nichukue nafasi hii kipekee kupongeza kwa kazi nzuri inayofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze na barabara muhimu kabisa katika Mkoa wetu wa Geita barabara ya kutoka Kahama kwenda Bukoli mpaka Geita, ni barabara muhimu sana kiuchumi, kumbuka katika Mkoa wa Geita na Mkoa wa Shinyanga ni mikoa ambayo imebobea katika masuala mazima ya madini, na kwa sababu hiyo tunahitaji barabara hii iwe ya lami ili iwezeshe shughuli za uchiumbaji wa madini ziende vizuri zaidi usafirishaji wa mizigo mbalimbali. Kwa hiyo niseme tu kwamba barabara hii ni muhimu sana na kila bajeti barabara hii huwa inakuwepo kwenye bajeti lakini kwenye utekelezaji sijawahi kuiona. Kwa hiyo nitumie fursa hii kuiomba Serikali iwekeze fedha sasa nimeona kwenye bajeti imeweka fedha kiasi fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaomba barabara hii ianze kujengwa sasa kwa kiwango cha lami, barabara hii ni barabara ya kiuchumi, barabara hii imekuwepo kwenye bajeti kuanzia wakati wa Awamu ya Nne ya Mheshimiwa Rais Kikwete katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi barabara hii imekuwepo kila Ilani inakuwepo barabara hii kuwekewa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa Serikali awamu hii barabara hii ianze kujengwa kwa kiwango cha lami kwa kuanzia Geita kwenda Bukoli mpaka Kahama. Kwa kuwa tunafahamu kuna mradi mkubwa mgodi mkubwa wa Geita lakini pia kuna mradi mkubwa mgodi wa Bulyang’huru, ambao wote hawa wanafanya shughuli za uchumbaji wa madini katika mikoa yetu, kwa hiyo, tukiimarisha barabara hizi nina uhakika shughuli hizi za uchimbaji zitaweza kunufaisha Taifa letu kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna barabara muhimu kabisa ya kutokea Katoro - Bukombe ambapo barabara hii pia ni muhimu sana kiuchumi katika Mkoa wetu wa Geita niombe Serikali pia iangalie uwezekano wa kuiwekea barabara hii lami ili kuwezesha uchumi ndani ya Mkoa kuwa mchumi mzuri. Ninafahamu sera yetu ya Taifa inasema kwamba mikoa yote itaunganishwa kwa kiwango cha lami, jambo ambalo ni la msingi sana na ndio maana ninatolea msisitizo kwamba tuunganishe Mkoa wa Geita na Mkoa wa Shinyanga ili hatimaye uchumi wetu uweze kwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika upande wa barabara ziko barabara ambazo zimekuwa ni muhimu sana kuchumi kwa mfano, kuna barabara ya kutokea Katoro kwenda Nyang’wale kupitia Kamena - Nyalwanzaja- Busanda ni barabara ambayo kwa muda mrefu tumeiomba iwe barabara ya mkoa imekuwa ni barabara ya halmashauri lakini sasa hivi naiombea iwe barabara ya mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa bahati nzuri mwaka jana kuna watu walitoka Wizara ya Ujenzi walikuja kuikagua barabara hii lakini kwenye bajeti sijaweza kuiona haijapandishwa hadhi mpaka sasa. Niombe barabara hii pia kwa umuhimu wake niombe ipandishwe hadhi iwe barabara ya Mkoa ili hatimaye iweze kuwahudumia wananchi waliowengi kwa sababu tunatambua kabisa vijijini wananchi tunahitaji barabara nzuri ambazo ziwezeshe katika kuimarisha uchumi wa wananchi katika maeneo yote kwa ajili ya usafirishaji wa mizigo mbalimbali, mazao, kupeleka katika viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba sana Serikali iangalie barabara hii ni muhimu kuweza kuipandisha kutoka halmashauri kwenda kwenye kuwa barabara ya Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna barabara zingine ambazo tunaishukuru Serikali kwamba imeweza kupandisha hadhi barabara ya kutokea Mbogwe kupitia Bukoli kwenda mpaka Bujula kuwa barabara ya Mkoa ninaishukuru sana Serikali na naipongeza kwa hatua hiyo niombe sasa mwaka huu barabara hii ianze kutengenezwa vizuri ili wananchi waweze kunufaika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kuhusiana na suala la mawasiliano. Mawasiliano ni jambo la msingi na ni suala muhimu sana kwa ajili ya wananchi hasa waishio vijijini. Nitumie fursa hii kuiomba Wizara iangalie sana maeneo ya vijijini. Natambua kwamba Mheshimiwa Waziri alituambia tupeleke majina ya kata zote ambazo hazina mawasiliano ya simu. Na mimi nilipeleka majina ya kata mbalimbali ikiwemo Kata ya Nyamalimbe, ikiwemo Kata ya Bujura ambazo zina matatizo makubwa sana ya mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitumie fursa hii kuiomba Serikali iangalie maeneo haya. Najua kibiashara pengine hayalipi sana, lakini kwa kuwa kuna Mfuko ule wa UCAF naiomba Serikali iwekeze zaidi vijijini kupeleka mawasiliano ili hatimaye kuimarisha zaidi wananchi waweze kufanya kazi zao kwa mawasiliano. Tunatambua mawasiliano ni kitu muhimu. Kupitia mawasiliano tunarahisisha biashara mbalimbali na zinaweza kufanyika bila shida yoyote. Kwa hiyo, naiomba Serikali iangalie sana katika suala hili la mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ziko kata mbalimbali ambazo zinahitaji mawasiliano kama ambavyo nimezitaja kwenye Jimbo la Busanda, lakini pia na maeneo mengine ya vijijini, kwani maeneo ya vijijini mengi yanahitaji mawasiliano ya simu ili kuweza kuimarisha na kuwezesha kustawisha zaidi hali ya uchumi katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, natumia fursa hii kuiomba Serikali iwekeze zaidi katika Mfuko wa UCSAF ili hatimaye kuweza kuyafikia maeneo mengi ya vijijini ambayo yamekuwa na changamoto kubwa sana ya mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika upande huo wa mwasiliano napenda kuomba Serikali iangalie minara. Minara mingi ambayo imesimikwa katika maeneo mengi wanakuwa hawalipi kwenye vijiji wanapochukua yale maeneo kwa ajili ya kusimika minara. Kuna changamoto kubwa, watu wengi wanafuatilia sana, lakini hawapati haki zao. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie pia suala hili hasa wananchi ambao ni wanyonge ambao wame… (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Lolesia Bukwimba. Mheshimiwa…

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Nashukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)