Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Daniel Edward Mtuka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DANIEL E. MTUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ili nami angalau kwa dakika chache hizi nitoe mchango wangu katika Wizara hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. Kwanza nimpongeze Rais wangu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anachapa kazi. Ukiitazama nchi hii ya Tanzania ni kubwa, lakini ninavyozungumza kila mahali naona barabara zinajengwa; madaraja, flyovers zinajengwa; na mabwawa, visima, naona vinajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hospitali, vituo vya afya, zahanati naona zinajengwa; ukienda Kinyerezi Bonde la Mto Ruvu kule mitambo ya umeme inajengwa; REA nguzo naona zinatambaa kila mahali, kila kona ya nchi hii zinachimbiwa na umeme unakwenda; Viwanja vya ndege vinakarabatiwa, vingine vinajengwa vipya; lakini kuna ujenzi wa meli, vivuko, magati kwenye maziwa, bahari pamoja na mito yanajengwa; lakini kuna ujenzi wa reli ya kisasa unaendelea; vyumba vya madarasa vinajengwa; matundu ya vyoo yanajengwa; ukarabati wa shule kongwe unaendelea; ujenzi wa vituo vya VETA unaendelea; ujenzi wa viwanda mbalimbali unaendelea; lakini bajeti ya dawa imepanda, kutoka bilioni 31 mpaka 270; lakini elimu bure pia shule ya msingi mpaka Form Four.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile amedhibiti matumzii ya fedha; kwa hiyo anapodhibiti matumizi ya fedha maana yake ni kwamba ameokoa fedha nyingi. Kwa mfano amedhibiti sana rushwa, amedhibiti wafanyakazi hewa, kwa hiyo pesa ile imeongezeka inakwenda kwenye kazi; naona kasi ya Mheshimiwa Rais ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi niwapongeze pia Waziri na Naibu Mawaziri pamoja na timu nzima ya Wizara. Nilete maombi machache kabla sijapigiwa kengele; kule Jimboni kwangu Manyoni kuna kituo kikubwa sana kile cha kati cha ukaguzi wa mizigo ya magari makubwa, pale Mhalala. Naona kwenye ukurasa wa 256 wametenga bilioni nne sawa, lakini ule ujenzi umesimama tangu Septemba, mwaka jana, naomba ile kasi iongezeke, tunataka kile kituo kikamilike.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuhusu Daraja la Sanza; nimeona kuna milioni 60 imetengwa hapa. Upembuzi yakinifu umeshafanyika, lakini imebakia tu ile process ya ujenzi ianze na mwaka huu tulitegemea kwamba fedha zile ziwekwe ujenzi uanze, lakini sioni fedha yoyote hapa, milioni 60 si kitu, yaani ni kama hakuna. Watutenge fedha watuongezee kwenye lile daraja, lile daraja ni muhimu kwa sababu ile barabara inayotoka kule Manyoni kwenda Sanza na kuvuka lile daraja kwenda Dodoma ni ya kiuchumi kwa Wilaya ya Manyoni kwa sababu lile eneo lote ndilo linalozalisha chakula kwa Mkoa wa Singida na Mkoa wa Dodoma sehemu pia wanapata. Kwa hiyo hilo daraja ni la msingi na la muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimeangalia barabara yetu ya Rungwa – Mkiwa; wenzetu kule wa Chunya tayari wameshapewa hela Chunya – Makongorosi, lakini Mbalizi – Makongorosi pia wameshapewa fedha nimeziona hapa, lakini sijaona Mkiwa kwenda Noranga, hakuna fedha pale, sijui kwa nini na ilikuwa tupewe fedha hizi tangu mwaka jana, hakuna fedha, hatuzioni. Kwa nini sisi hawajatenga ile fedha wanawatengea wenzetu wa upande ule? Nadhani utaratibu ulikuwa wakandarasi wakutane katikati, lakini wanatenga upande mmoja, watenge na huku basi ili wakutane katikati.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, minara ya simu; nimekuwa nikuliza mara nyingi sana, kuna Kata yangu moja inaitwa Makuru, hasa Kijiji kimoja kinaitwa Hika, kule tunahitaji minara. Njia ile ya kutoka Manyoni kwenda Sanza, mule njiani ukisafiri hakuna minara, kwa hiyo mawasiliano yanakatika, naomba sana Wizara hii iniangalie. Nimeshauliza mara nyingi sana hapa Bungeni, wameshajibu kwamba wataleta minara, lakini nimetazama sioni fedha yoyote iliyotengwa, naomba sana sehemu hii ya minara na mawasiliano ili tuweze kuwasiliana kwa sababu mawasiliano ni maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo machache, nashukuru sana, naunga mkono hoja asilimia mia kwa mia. (Makofi)